TUME ya Mipango Zanzibar (ZPC) imetia saini hati ya makubaliano na taasisi nne za kitaaluma na utafiti kwa ajili ya kuanzisha jukwaa la pamoja la fikra, tafiti na ushauri wa kisera, hatua inayolenga kuharakisha utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo wa Zanzibar (ZADEP III).
Taasisi zilizosaini makubaliano hayo ni Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA), Taasisi ya Utafiti wa Kiuchumi na Kijamii (ESRF), Policy Innovation Lab Africa (PIL-A) pamoja na Africa School of Economics (ASE).
Akizungumza katika hafla hiyo, Katibu Mtendaji wa Tume ya Mipango Zanzibar, Dk. Josephine Rogate Kimaro, alisema, dhamira kuu ni kujenga uwezo wa ndani na kuhakikisha Zanzibar inakuwa na wataalamu wenye uwezo wa kushughulikia masuala mbalimbali ya maendeleo.
“Dhamira yetu ni kujenga uwezo wa ndani. Makubaliano haya yanakusudia kujenga uwezo katika masuala mbalimbali ya maendeleo kwa wataalamu wa Zanzibar.
Aidha alisema wamekuwa wakitekeleza dira ya Serikali ya kujenga uwezo wa ndani tukiwa katika maandalizi ya utekelezaji wa ZADEP III na kusema kuwa kazi hiyo itafanywa hapa nchini kwa kutumia wataalamu waliopo Zanzibar, hatua ambayo itasaidia kuongeza matumizi ya utaalamu wa ndani katika kupanga na kutekeleza miradi ya maendeleo.
Dk.Kimaro alisema mipango yenye matokeo inapaswa kujengwa kwa kuzingatia ushahidi, akieleza kuwa ushirikiano huo ni sehemu ya hatua zinazochukuliwa na Tume kuhakikisha kila kipaumbele cha ZADEP III kinaambatana na uchambuzi wa kiuchumi, takwimu sahihi na tathmini ya kina.
Kwa upande wake, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) Profesa Said Ali Hamad Vuai amesema Zanzibar ina wataalamu, watafiti na wanafunzi wenye uwezo mkubwa ambao wanaweza kuchangia katika utekelezaji wa mipango ya maendeleo.
Alisema kupitia ushirikiano huo, maarifa yanayozalishwa katika vyuo vya elimu ya juu yataweza kufikishwa moja kwa moja katika ngazi za kufanya maamuzi ya kitaifa, huku wahitimu wakipata fursa ya kushiriki kwa vitendo katika utekelezaji wa ZADEP III.
Aidha alisema ushirikiano huo unaunganisha uwezo wa sekta ya umma, taasisi za elimu ya juu na taasisi za utafiti nchini katika mfumo mmoja, hatua inayolenga kuiwezesha Zanzibar kupanga, kufadhili na kutekeleza vipaumbele vyake vya maendeleo kwa kutumia rasilimali, maarifa na utaalamu wa ndani.
Makubaliano huo na taasisi hizo zitawaunganisha uwezo katika sekta mbalimbali, ikiwemo elimu ya juu na maandalizi ya wataalamu, utafiti wa kiuchumi na uchambuzi wa sera, ubunifu wa sera, mitandao ya kitaalamu barani Afrika, pamoja na matumizi ya takwimu na tathmini ya matokeo ya miradi na programu za maendeleo.
Sambamba na hayo, ushirikiano huo utajikita katika maeneo mbalimbali, yakiwemo utafutaji wa rasilimali fedha, ushirikishwaji wa wataalamu bobezi, mpango mkakati wa ufikishaji wa taarifa, utafiti na uchambuzi wa sera, pamoja na kujenga uwezo wa watumishi na wadau wa maendeleo.

















0 Comments