6/recent/ticker-posts

mkutano wa kuwasilisha matokeo ya mradi wa ZAN-TOTO, uliolenga kuimarisha matumizi sahihi ya dawa za antibiotiki, hususan kwa watoto.

Na.Mwandishi wa Wizara ya Afya. 

WIZARA ya Afya Zanzibar kupitia Taasisi ya Utafiti wa Afya Zanzibar (ZAHRI), kwa kushirikiana na wadau mbalimbali, imefanya mkutano wa kuwasilisha matokeo ya mradi wa ZAN-TOTO, uliolenga kuimarisha matumizi sahihi ya dawa za antibiotiki, hususan kwa watoto.

Akizungumza katika mkutano huo, Mkurugenzi Mkuu wa Wizara ya Afya Zanzibar, Dkt. Mariyam Seif Hemed, amesema matumizi sahihi ya antibiotiki ni muhimu katika kulinda afya ya wananchi, huku matumizi yasiyo sahihi yakisababisha madhara kwa afya ya mtu binafsi na kuongeza gharama kwa Serikali.

Amesema matumizi holela ya antibiotiki yanaweza kufanya baadhi ya magonjwa kuchukua muda mrefu kupona, pamoja na kusababisha vijidudu vinavyosababisha magonjwa kuzoea dawa hizo na hivyo kuwa vigumu kutibiwa.

Dkt, Mariyam amewataka wananchi kutumia antibiotiki kwa usahihi na kwa kufuata ushauri wa wataalamu wa afya, huku akitoa wito kwa wadau kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali katika kukabiliana na matumizi yasiyo sahihi ya dawa hizo.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) kwa upande wa Zanzibar, Dkt Ndoungou Salla Ba amesema wataendelea kushirikiana na Serikali ya Zanzibar katika kuimarisha matumizi sahihi ya antibiotiki hasa kwa watoto, kwa kuweka mkazo katika kuongeza uelewa kwa wataalamu wa afya pamoja na jamii kuhusu matumizi sahihi ya dawa hizo.

Amesema WHO itaendelea kusaidia juhudi za Serikali katika kukabiliana na changamoto ya usugu wa vimelea dhidi ya antibiotiki, ikiwemo kuimarisha mifumo ya matumizi na usimamizi wa dawa, ili kuhakikisha antibiotiki zinatumika kwa usahihi na zinaendelea kuwa na ufanisi katika kutibu magonjwa na kuwa na taarifa sahihi.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu katika Taasisi ya Afya Zanzibar ZAHRI, Dkt Mayasa Salum Ali amesema kuwa mradi wa Zan Toto Project umemalizika baada ya kutekeleza kampeni ya kukabiliana na matumizi mabaya na holela ya dawa za antibayotiki Zanzibar.

Amefahamisha kuwa mradi huo ulisaidiwa kutekelezwa na ICARS umetumia takriban shilingi bilioni 1.5 na kutekelezwa katika hospitali tano za Zanzibar, ikiwemo Hospitali ya Mnazi Mmoja na Kivunge kwa upande wa Unguja, pamoja na hospitali tatu za Pemba ambazo ni Kinyasini, Vitongoji na Abdalla Mzee na ulihusisha utafiti kuhusu matumizi ya dawa za antibayotiki kwa watoto walio chini ya umri wa miaka mitano, sambamba na kutoa elimu na uhamasishaji kuhusu matumizi sahihi ya dawa hizo.

Amesema usugu wa dawa za antibayotiki ni miongoni mwa changamoto kubwa za kiafya zinazoikabili dunia kwa sasa, huku matumizi ya dawa hizo kiholela yakitajwa kuwa moja ya sababu zinazochangia kuongezeka kwa usugu hali hiyo husababisha baadhi ya bakteria kutokubaliana na dawa zinazotumika kutibu maambukizi, jambo linalofanya magonjwa kuwa magumu kutibiwa na kuongeza hatari ya madhara makubwa pamoja na vifo.

Nae Mkuu wa Taasisi ya ICARS Afrika Dkt Titha Dzowela   amesema wameshirikiana na Zanzibar katika kuimarisha juhudi za kukabiliana na matumizi yasiyofaa ya dawa za antibayotiki, kupitia mradi wa Zan Toto Project huku mradi huo ukiwezesha kufanyika kwa tafiti na kampeni za uhamasishaji, hususan kwa kuangalia matumizi ya dawa hizo kwa watoto walio chini ya umri wa miaka mitano dhidi ya usugu wa dawa za antibayotiki.

Kwa upande wa Mratibu wa Mradi wa Zan Toro Project, Muhidin Omar, amesema kuwa mradi huo wa miaka mitatu ulitakiwa kutekelezwa kwa kiwango cha asilimia 30, lakini kupitia utekelezaji wake wamefanikiwa kupunguza changamoto zilizokuwa zikikabili huduma hizo kwa asilimia 25.

 Aidha, amesema mradi huo umeongeza kwa kiasi kikubwa uelewa na ujuzi kwa madaktari wanaohusika na matibabu ya watoto, hatua ambayo imekuwa na mchango mkubwa katika kuimarisha utoaji wa huduma za afya kwa watoto na kuhakikisha wanapata matibabu kwa ufanisi zaidi.

Aidha, washiriki wa mkutano huo wameeleza umuhimu wa kuendelea kutumia teknolojia na mifumo ya kusambaza taarifa za matumizi sahihi ya antibiotiki katika hospitali na vituo vya afya, ili kuhakikisha wataalamu na wananchi wanapata elimu sahihi kuhusu matumizi ya dawa hizo.

Mwisho.

Post a Comment

0 Comments