Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema Tanzania iko tayari kuimarisha zaidi ushirikiano na Serbia katika biashara na uwekezaji, kilimo, utalii, elimu na Uchumi wa Buluu kwa manufaa ya wananchi wa nchi hizo mbili.
Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo tarehe 02 Septemba 2026, jijini Belgrade, Serbia, alipokutana na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Serbia, Mhe. Prof. Đuro Macut, katika hitimisho la ziara yake nchini humo.
Amesema ziara hiyo imefungua fursa mpya za kuendeleza ushirikiano wa kiuchumi, hususan katika kilimo kupitia upatikanaji wa mbolea, mbegu, teknolojia na uchakataji wa mazao, pamoja na kuimarisha biashara na uwekezaji.
Aidha, amesisitiza umuhimu wa kuongeza utalii kati ya nchi hizo mbili, akieleza kuwa kuanzishwa kwa safari za ndege za moja kwa moja kati ya Serbia na Tanzania kutasaidia kuongeza watalii, biashara na uwekezaji.
Kwa upande wa Uchumi wa Buluu, Rais Dkt. Mwinyi amesema Zanzibar ina fursa kubwa katika uvuvi, uzalishaji wa mwani na shughuli nyingine za baharini, hivyo kuna umuhimu wa kutafuta masoko zaidi ya bidhaa hizo nchini Serbia na Ulaya.
Rais Dkt. Mwinyi ameipongeza Serbia kwa kufungua Ubalozi wake wa kudumu nchini Tanzania na kuishukuru Serikali hiyo kwa fursa za ufadhili wa masomo kwa wanafunzi wa Tanzania.
Kwa upande wake, Waziri Mkuu Prof.Macut amesema Serbia inathamini urafiki wa kihistoria na Tanzania uliojengwa tangu enzi za Yugoslavia, akieleza kuwa bado kuna fursa kubwa za kupanua ushirikiano katika biashara, utalii, kilimo, uvuvi na uchakataji wa mazao.
Kabla ya kuondoka Serbia, Rais Dkt. Mwinyi ametembelea Makumbusho ya Yugoslavia, katika eneo la House of Flowers jijini Belgrade, na kuweka shada la maua katika kaburi la aliyekuwa Rais wa Yugoslavia na mmoja wa waasisi wa NAM, Josip Broz Tito.
Rais Dkt. Mwinyi anatarajiwa kuondoka Serbia tarehe 02 Septemba 2026 kurejea Zanzibar, baada ya kukamilisha ziara iliyohusisha kushiriki Mkutano Maalum wa Ngazi ya Juu wa Kumbukumbu ya Miaka 65 ya NAM pamoja na shughuli za kidiplomasia na kuimarisha uhusiano kati ya Tanzania na Serbia.









0 Comments