Chama cha ACT-Wazalendo kimeondoa rufaa iliyowasilishwa kupinga uamuzi wa Mahkama Kuu ya Zanzibar katika mashauri tisa ya Uchaguzi yaliyokuwa yameunganishwa, hatua inayofanya kutokuwa na rufaa inayoendelea mahkamani kati ya chama hicho na Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) kutokana na mashauri hayo.
Hayo yameelezwa na Mkuu wa Kurugenzi ya Huduma za Sheria ndugu.Maulid A. Mohammed wakati wakuwasilisha taarifa ya Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar katika Mkutano na Waandishi wa Habari uliofanyika makao makuu ya ZEC - Maisara Wilaya ya Mjini Unguja.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar, rufaa hiyo ilisajiliwa kama Civil Appeal No. 04 of 2026, na ilihusu uamuzi wa Mahkama Kuu uliotolewa Februari 19, 2026 katika mashauri tisa ya Uchaguzi yaliyowasilishwa na ACT-Wazalendo katika majimbo tisa ya Pemba.
Tume imesema taarifa ya kuondoa rufaa hiyo iliwasilishwa Mahkamani Septemba 1, 2026 kupitia Notice of Withdrawal of Appeal, iliyowasilishwa na Mwanasheria wa Chama cha ACT-Wazalendo katika Masjala ya Mahkama Kuu ya Zanzibar, Tunguu.
Mashauri hayo yalitokana na hatua zilizochukuliwa baada ya kumalizika kwa Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar wa mwaka 2025, ambapo baadhi ya Wagombea kupitia ACT-Wazalendo waliwasilisha mashauri kupinga matokeo ya Uchaguzi wa Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi na Udiwani, wakidai kuwepo kwa ukiukwaji wa taratibu za Uchaguzi katika vituo vya Kupigia na Kuhesabu kura.
Kwa mujibu wa Tume, jumla ya mashauri 26 yalifunguliwa katika Mahakama Kuu ya Zanzibar, ambapo mashauri kumi na saba yalihusu Unguja na tisa kwa upande wa Pemba. Mashauri hayo yalisikilizwa na majaji tofauti na Mahkama ilikubaliana na hoja zilizowasilishwa na Tume pamoja na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, na kuyaondoa mashauri hayo kutokana na kasoro za kisheria zilizojitokeza.
Baada ya uamuzi huo, baadhi ya wagombea waliwasilisha nia ya kukata rufaa. Kwa upande wa mashauri nane ya Unguja yaliyosikilizwa na Jaji Mohd A. Mohd, rufaa ilisikilizwa na jopo la majaji watatu wa Mahkama Kuu.
Tume imesema kuwa tarehe 31 Agosti 2026, jopo hilo lilitoa uamuzi wa kukubaliana na uamuzi wa awali na kuifuta rufaa hiyo. Aidha, Mahkama iliamuru ACT-Wazalendo kuwalipa wapinga rufaa, ambao ni Afisi ya Mwanasheria Mkuu na Tume ya Uchaguzi, gharama zilizotumika katika uendeshaji wa mashauri hayo kwa mujibu wa uamuzi na amri za Mahkama.
Kwa upande mwingine, mashauri tisa ya Unguja yaliyosikilizwa na Jaji Salma A. Hassan yalitolewa uamuzi Agosti 26, 2026, huku hadi sasa Tume ikisema haijapokea taarifa ya kukata rufaa kutoka kwa wagombea hao.
Kanuni za Uendeshaji wa Mashauri ya Uchaguzi za mwaka 2025 zinaeleza kuwa mtu asiyeridhika na uamuzi wa Mahakama anatakiwa kuwasilisha nia ya kukata rufaa ndani ya siku saba baada ya kutolewa kwa uamuzi.
Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar imesema imepokea na kutambua hatua ya ACT-Wazalendo kuondoa rufaa hiyo, huku ikisisitiza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya mchakato wa kisheria unaosimamiwa na Mahkama.
Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar, imesema itaendelea kuheshimu mamlaka, taratibu na maamuzi ya Mahkama katika masuala yote yanayohusu Uchaguzi. Kwa sasa, Tume imewajulisha wadau wa uchaguzi kuwa
hakuna rufaa inayoendelea Mahakamani kati ya ACT-Wazalendo na ZEC inayotokana na mashauri yaliyotajwa katika taarifa hiyo.
Tume imewataka Wawakilishi wa Vyama Vya Siasa, Wagombea, Waandishi wa Habari, Waangalizi wa Uchaguzi na Wadau wengine wa Uchaguzi kuwa na uelewa sahihi kuhusu hali ya mashauri hayo na kuepuka kusambaza taarifa zinazoweza kupotosha umma kuhusu mwenendo au matokeo ya mashauri.
Tume imesisitiza kuwa itaendelea kutekeleza majukumu yake kwa mujibu wa Katiba, Sheria za Uchaguzi na taratibu zinazotumika, bila upendeleo kwa Chama, Mgombea au upande wowote.
Aidha, Tume, imewahakikishia wananchi na Wadau wa Uchaguzi kuwa itaendelea kutoa taarifa sahihi na kwa wakati kuhusu masuala yenye umuhimu kwa umma, huku ikisisitiza misingi ya uadilifu, uwazi, uhuru na uzingatiaji wa Sheria katika utekelezaji wa majukumu yake.

0 Comments