6/recent/ticker-posts

SMZ Itaendelea Kuthamini na Kuimarisha Ushirikiano na China Katika Kuhakikisha Wananchi Wanapata Huduma Bora za Afya Kupitia Madaktari Bingwa kutoka China

Na.Mwandishi Wizara ya Afya Zanzibar.

SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya Afya Zanzibar imesema itaendelea kuthamini na kuimarisha ushirikiano na Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za afya kupitia Madaktari kutoka China wanaotoa huduma katika Hospitali mbalimbali pamoja na katika jamii za Unguja na Pemba.

Hayo yameelezwa na Kaimu Waziri wa Afya Zanzibar, Dkt Saada Mkuya Salum, wakati wa hafla ya kuwaaga madaktari wa Timu ya 35 kutoka China pamoja na Timu ya 3 ya wataalamu wanaoshughulikia mapambano dhidi ya ugonjwa wa kichocho hapa nchini.

 Amesema kwa kipindi ambacho madaktari hao wamekuwa wakifanya kazi Zanzibar, Serikali na wananchi wamefaidika kwa kiasi kikubwa, ambapo wananchi wamepata matibabu ya magonjwa mbalimbali, huku wataalamu wa afya wazawa wakinufaika kupitia mafunzo na uzoefu walioupata kutoka kwa madaktari hao.

Amesema madaktari hao wametoa huduma katika Hospitali ya Mkoa Rufaa ya Lumumba na Hospitali ya Jitimai kwa upande wa Unguja, pamoja na Hospitali ya Abdalla Mzee kwa upande wa Pemba, huku wakishirikiana na wataalamu wazawa katika kutoa huduma na kuwajengea uwezo katika maeneo mbalimbali ya kitaalamu.

Aidha, amesema madaktari hao wamefanya kazi kubwa katika jamii kwa kutoa huduma katika vijiji 186, sambamba na kusaidia Zanzibar kupiga hatua katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa kichocho.

Amefahamisha kuwa  mafanikio hayo yameonekana zaidi Pemba, ambapo hatua kubwa imefikiwa katika udhibiti wa ugonjwa huo, huku Serikali ikiendelea kujiandaa kuwapokea wataalamu wengine mwezi Machi kwa ajili ya kuimarisha mapambano hayo, pamoja na Timu ya 36 ya madaktari kutoka China inayotarajiwa kuwasili mwezi Novemba.

Kwa upande wake, Balozi wa China kwa upande wa zanzibar, Li Qianghua, amesema Serikali ya China itaendelea kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya Afya katika kuimarisha huduma za afya kwa wananchi wa Zanzibar.

Amesema ushirikiano huo utaendelea kuimarishwa katika maeneo mbalimbali, ikiwemo utoaji wa huduma za afya katika hospitali na jamii, upatikanaji wa vifaa tiba pamoja na kuwajengea uwezo wataalamu wa afya wazawa ili waweze kutoa huduma bora na zenye ufanisi kwa wananchi.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Zanzibar, Dkt. Mngereza Mzee Miraji, amesema ushirikiano kati ya Zanzibar na China umeleta mafanikio makubwa katika sekta ya afya, hususan katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa kichocho kwa upande wa Pemba.

 Amesema hali ya ugonjwa wa kichocho Pemba imeendelea kuimarika, ambapo kiwango cha maambukizi kilikuwa asilimia 1.6, na sasa kufikia chini asilimia mia moja hatua inayoiweka Zanzibar katika nafasi nzuri ya kufikia hatua ya kutokomeza ugonjwa huo kwa mujibu wa miongozo ya Shirika la Afya Duniani (WHO).

Amesema hatua hiyo ni mafanikio makubwa kwa Zanzibar kwa kuwa si mataifa yote yameweza kufikia hatua hiyo, na kwamba mafanikio hayo yametokana na juhudi za Serikali kupitia Wizara ya Afya, ikiwemo uwekezaji mkubwa unaofanyika katika sekta ya afya na ushirikiano na wadau mbalimbali, wakiwemo Serikali ya China.

Kiongozi wa Madaktari wa Timu ya 35 kutoka China, amesema ushirikiano kati ya Zanzibar na China ni wa muda mrefu na umeendelea kuwa na manufaa makubwa katika kuimarisha huduma za afya kwa wananchi wa Unguja na Pemba.

Amesema katika kipindi chao cha kufanya kazi Zanzibar, wamekuwa wakishirikiana kwa karibu na wataalamu wa afya wazawa katika kutoa huduma, kubadilishana uzoefu na kuwajengea uwezo, huku akieleza kuwa wataendelea kuthamini ushirikiano huo na kuimarisha mahusiano kati ya wataalamu wa afya wa China na Zanzibar.

Post a Comment

0 Comments