6/recent/ticker-posts

MAKAMU WA PILI WA RAIS ZANZIBAR--KUMUWAKILISHA WAZIRI MKUU WA JAMUHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA--MBIO ZA HISANI CRDB BANK INTERNATIONAL MARATHON--JIJINI DAR ES SALAAM

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe.Hemed Suleiman Abdulla akiwa na viongozi na wanamichezo mbalimbali katika Matembezi ya Hisani ya CRDB BANK INTERNATIONAL MARATHON yaliyofanyika katika Viwanja vya Posta Kijitonyama Jijini Dar es Salaam.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe.  Hemed Suleiman Abdulla amesema Taifa linahitaji nyenzo muhimu katika kufikia mafaniko ya malengo ya Dira ya 2050 kama vile rasilimali watu wenye afya njema, vijana wenye fursa pamoja na sekta binafsi zinazowajibika.

Ameyasema hayo kwa niaba ya Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (MB) Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Tamasha la mbio za hisani  za CRDB BANK INTERNATIONAL MARATHON zilizofanyika katika viwanja  vya Posta Kijitonyama Jijini Dar es Salaam.

Amesema lengo la Tamasha hilo ni kusaidia upatikanaji wa huduma za matibabu katika hospitali mbali mbali nchini ambapo zaidi ya watoto 1000 wamepatiwa matibabu ya moyo katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete na zaidi ya wananwake 450 wenye ujauzito hatarishi wamepatiwa matibabu katika Hospitali ya CCBRT na jambo lililoweza kuokoa maisha ya watu hao ambao wangeweza kupata madhara makubwa.

Makamu wa pili wa Rais wa Zanzibar amesema CRDB International Marathon inakwenda kuongeza nguvu katika sehemu ya vipaombele vya Sekta ya Afya kwa mwaka 2025/2026 ambapo Serikali inalenga kuimarisha huduma za kinga, afya ya uzazi, huduma ya mama na mtoto ili kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi.

Mhe. Hemed ameeleza kuwa sekta ya michezo inachangia katika uchumi, kuzalisha ajira, kukiza Utalii na uwekezaji na ni nyenzo muhimu ya kuitangaza Tanzania Kimataifa kupitia mashindano mbali mbali ambayo huacha athari chanya za kiuchumi na kijamii.

Aidha, Mhe. Hemed amewasihi wananchi kuendelea kuunga mkono jitihada za wadau mbalimbali wanaolenga kugusa maisha ya wenye uhitaji na kuboresha ustawi wa jamii kwa ujumla.

Sambamba na hayo Makamu wa pili wa Rais wa Zanzibar amewapongeza CRDB BANK FOUNDATION kwa kuekeza katika maeneo ya vipaombele vya Serikali na kudhihirisha wazi dhana ya ushirika wa Serikali na sekta binafsi katika kutatua changamoto za wananchi pamoja na kuwataka vijana na wanamichezo kuilinda amani iliyopo nchini na kusema kuwa bila ya amani na utulivu hakuna maendeleo yanayoweza kufikiwa nchini.

Mhe. Hemedi amemaliza hotuba yake kwa kuwataka vijana na wanamichezo kuilinda amani iliyopo nchini na kusema kuwa nila ya amani na utulivu hakuna maendeleo yanayoweza kufikiwa nchini .

Nae Mwenyekiti wa  Bodi ya CRDB Banki Foundation CPA. Oswald Urassa amesema Benki ya CRDB imejikita kuhakikisha inaendelea kutoa miongozo ya kisera kwa Menejimenti ili kuhakikisha Taasisi hio inawafikia walengwa kupitia  program mbali mbali zilizobuniwa na Benki hio ambazo tayari zimeshawanufaisha maelfu ya Watanzania.

CPA Oswald amesema mkakati wa Benki ya CRDB ni kuwa kinara katika utowaji wa huduma za kifedha kwa Ukanda wa Afrika Mashariki na Kati ambapo dhamira kubwa zaidi ni kuona Benki hio inaimarisha zaidi mahusiano na nchi jirani ili kutanua mbawa katika utoaji wa huduma zilizo bora , kukuza uchumi na kuimarisha huduma za jamii.

Mapema Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB Dkt. Abdulmajid Nsekela amesema malengo ya Matembezi hayo yanalenga kubadilisha maisha ya Watanzania wengi ambao wanasumbuliwa na magonjwa mbalimbali yakiwemo magonjwa ya moyo, saratani na huduma za mama wajawazito na watoto walio katika hali hatarishi.

Dkt. Nsekela amebainisha kuwa CRDB BANK imejipanga kutoa huduma kubwa zaidi kwa jamii hasa vija, wanawake na watoto wakitambua kuwa uchumi imara unaanza na watu wenye afya bora itakayotimiza malengo na ndoto zao wanazozipambania.

Dkt. Nsekela amesema kuwa kupitia CRDB Benki International Marathon wameweza kuwafikia watoto zaidi ya mia nne (400) ambao wamesaidiwa kupata huduma za matibabu ya upasuaji wa moyo na kuwasaidia kinamama wenye ujauzito hatarishi waweze kujifungua salama hivyo wataendelea na mpango wao wakuifikia zaidi jamii katika kuwaonesha fursa, kuwapa taaluma na kuwawezesha kuyafikia matarajio yao.

Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Dar-es- Salaam ndugu Albert Chalamila,   Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni Ndg. Saad Mtambuki amewataka vijana kujitoa na kuchangamkia fursa mbalimbali zinazotolewa na Benki ya CRDB ambao wanaweka juhudi kubwa katika kuekeza rasilimali fedha kwa vijana, wanawake na jamii kwa jumla ili kunyanyua mitaji, ubunifu na biashara za vijana na wajisiriamali.

Mtambuki amewakumbusha vijana wa Tanzania kuwa ili kutimiza ndoto za maisha yao watambue wana  jukumu kubwa la kuwa mabalozi wa kuhamasishana kuitunza Amani, kuwa wazalendo kwa nchi yao na kuilinda kwa nguvu zao zote ili iendelee kuwa Salama. 

Imetolewa na kitengo cha Habari ( OMPR )

Leo tarehe  16 / 08 / 2026

Post a Comment

0 Comments