Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla akikabidhi vifaa mbali mbali kwa wajasiriamali vilivyotolewa na Wizara ya Vijana, Ajira na Uwezeshaji Zanzibar, katika hafla ya Maadhimisho ya Siku ya Vijana Kimataifa yaliyofanyika katika Ukumbi wa Hoteli ya Golden Tulip Uwanja wa Ndege Zanzibar. 

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imechukua hatua mbalimbali katika kuzipatia ufumbuzi changamoto zinazowakabili vijana kwa kuanzisha Wizara maalum ya Vijana, Ajira na Uwekezaji ili kubuni, kupanga na kusimamia utekelezaji wa programu za maendeleo ya vijana.

Hayo yamesemwa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla kwa niaba ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dkt Hussein Ali Mwinyi katika Maadhimisho ya siku ya vijana Kimataifa yaliyofanyika katika Ukumbi wa Hoteli ya Golden Tulip Uwanja wa Ndege Zanzibar.

Amesema Serikali kupitia Wizara ya Vijana, Ajira na Uwezeshaji ipo katika hatua za mwisho za maandalizi ya mpango mkakati wa Kitaifa wa uzalishaji wa ajira Zanzibar ambao unajumuisha sekta za Umma na binafsi ili kutoa mchango wao katika uzalishaji wa ajira ndani na nje ya nchi.

Mhe. Hemed amesema Serikali kupitia Wakala wa Uwezeshaji wananchi kiuchumi imetoa zaidi ya shilingi Bilioni 12.7 kama mkopo wenye masharti nafuu zitakazo wanufaisha wananchi 4,730  wakiwemo vijana .

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amesema Serikali imeweka mkazo katika kuimarisha sekta ya elimu, mafunzo ya amali na ubunifu kwa vijana ambapo Bajeti ya Sekta ya elimu imeongezeka kutoka Bilioni 864 kwa mwaka 2025/2026 hadi kufikia zaidi ya Trilioni 1.1 kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

Sambamba na hayo Mhe. Hemed amesema Serikali imeimarisha upatikanaji wa mafunzo ya Ufundi na Elimu ya Amali kwa vijana kwa kujenga vyuo saba (7) vya mafuzo ya Ufundi na Elimu ya Amali ambapo vyuo vyengine vitano (5) kama hivyo vinatarajiwa kujengwa katika mwaka wa fedha 2026/27 pamoja na kujengwa karakana 25 katika Skuli za Sekondari Unguja na Pemba.

Aidha, Mhe. Hemed amesema kwa upande wa Elimu ya juu, jumla ya vijana 18,593 wamepatiwa mikopo ya elimu ya juu ambapo dhamira ya Serikali ni kuendelea kuimarisha elimu ya juu kwa kuongeza bajeti na fursa za upatikanaji wa mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu Zanzibar kwa kuanzia na ngazi ya stashahada (DIPLOMA).

Makamu wa Pili wa Rais ameeleza kuwa vijana wanaendelea kushiriki na kushirikishwa katika mambo mbalimbali pamoja na kuwajengea uwezo vijana kupitia baraza la vijana Zanzibar, Asasi za Kiraia, Serikali za wanafunzi, vyama vya michezo na taasisi nyenginezo za Kitaifa, Kikanda na Kimataifa zinazofanya kazi na vijana.

Nae Katibu Mkuu Wizara ya Vijana, Ajira na Uwezeshaji Zanzibar Bi.Salama Mbarouk Khatib amesema malengo ya kuwekwa maadhimisho ya Siku ya Vijana Kimataifa ni kutoa uelewa kwa jamii juu nafasi ya vijana katika kushiriki na kushirikishwa katika mipango mbali mbali ya maendeleo ya Taifa.

Bi. Salama amesema Wizara ya Vijana, Ajira na Uwezeshaji itaendelea kuwawezesha vijana katika nyanja mbalimbali ikiwemo kuwapatia elimu na ujuzi wa  kuweza kutambua wajibu wao kwa Taifa lao na jamii kwa ujumla .

Mapema Mwenyekiti Baraza la Vijana Taifa Dkt.Mohammed Abdurahaman Juma amemshukuru Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dkt Hussein Ali Mwinyi kwa kuwapa kipaombele vijana kwa kuwawekea Wizara maalumu inayoshughulikia masuala ya vijana ikiwemo Ajira na Uwezeshaji ili kutoa fursa mbali mbali kwa vijana kufikia mafanikio ya ndoto zao.

Dkt. Mohammed amewataka vijana wenzake kuchangamkia fursa mbalimbali zinazotolewa na Serikali na Taasisi binafsi lakini pia kushiriki katika harakati mbali mbali za maendeleo kwa kufuata maadili na miongozo ya dini zao.

Amewataka vijana kuwa mabalozi wazuri katika kuhamasisha utunzaji wa Amani na kuachana na kujiingiza katika makundi maovu yatakayowapelekea kupoteza malengo yao ya baadae.

Akizungumza kwa niaba ya Washirika wa maendeleo, Mkuu wa Ushirikiano wa Kimataifa kutoka Ubalozi wa Uswiss nchini Tanzania Bw.Holger Tausch amesema Vijana ni uwekezaji mkubwa ambao Taifa linaweza kuekeza kwa kuwapatia elimu, ujuzi na kuwawezesha katika kufikia malengo waliyojipangia kwa maendeleo ya Mataifa yao.

Holger amefahamisha kuwa katika kutambua mchango wa vijana Switzerland itaendelea kufanya kazi na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuwasaidia vijana kwa kutengeneza nafasi mbalimbali za kuwawezesha vijana na wanawake kuweza kujiajiri wenyewe na kutengezeza ajira kwa vijana wenzao.



Imetolewa na kitengo cha habari ( OMPR )

tarehe … 12 / 08 /  2026