6/recent/ticker-posts

Wananchi wameshauriwa kujitokeza kwa wingi kupata huduma za elimu ya afya na lishe

 Na.Mwandishi wa Wizara ya Afya Zanzibar.

Wananchi wameshauriwa kujitokeza kwa wingi kupata huduma za elimu ya afya na lishe katika vituo vya afya na kambi  mbalimbali zinazopelekwa katika shehia zao ili kupunguza vifo vya Watoto wenye mtapia mlo.

Ushauri huo umetolewa na afisa lishe wa Wilaya ya Magharibi B Asha Khamis Saleh katika siku ya afya na lishe ya shehia katika uwanja wa Magirisi wilaya ya Magharib B Unguja.

Amesema takwimu zinaonesha kuwa kwa miezi 3 iliyopita wilaya ya magharibi B kupitia hospitali ya wilaya jitimai imeongoza kwa vifo vya Watoto wenye utapia mlo kutokana na wananchi kutowapeleka Watoto vituo vya afya kupata huduma za afya na lishe bora.

Amesema kufanyika kwa siku ya elimu ya afya na lishe ya shehia inapelekea wanawafikia wananchi wengi Zaidi ambao hawafiki vituo vya afya kuwapeleka watoto kupata huduma hiyo hasa kwa Watoto waliomaliza chanjo kuanzia mwaka mmoja na nusu na kuendelea.

Akielezea huduma zinazotolewa katika siku hiyo Afisa lishe Maimuna Idrisa Mohamed ni Pamoja na utoaji wa chanjo kwa Watoto, elimu ya lishe, huduma za kidaktari, huduma ya macho, huduma ya vyeti vya kuzaliwa kwa Watoto, elimu ya kilimo na ufugaji, elimu ya namna ya kupika na  kutumia vyakula vya lishe, upimaji shindikizo la damu na upimaji wa saratani ya mlango wa kizazi.

Kwa upande wake sheha wa shehia ya Taveta Juma Zubeir Sultan kwa niaba ya shehia za Uzi, Kijitoupele na Pangawe ameishukuru wizara ya afya kwa kuwasogezea huduma mbalimbali za afya katika shehia yao kutokana na huduma hizo kuwanufaisha wananchi wengi kwa wakati mmoja.

Nao wananchi waliofika kupatiwa huduma hizo Khadija Daudi Suleiman na Mzee Yunus Haji kwa niaba ya wananchi wenzao wameelezea walivyofarajika na huduma hizo kusogezewa karibu yao na kuomba siku hiyo iwe endelevu kwa ajili ya kurahisisha upatikanaji wa huduma kama hizo.

Siku ya elimu ya afya na lishe kwa kawaida hutakiwa kufanyika kila baada ya miezi 3 katika kila shehia ambapo kwa leo imekusanya shehia nne ya Taveta, Kijitoupele, Uzi na Pangawe. 

Post a Comment

0 Comments