6/recent/ticker-posts

SMZ Itaendelea Kushirikiana na Chama cha Mabenki Tanzania ( TBA ) Katika Kuijenga Sekta ya Fedha Yenye Nguvu

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla amefanya uzinduzi wa Mfumo wa kidijitali wa utoaji wa huduma za Kibenki wa Nikofit ChatBot uliozinduliwa katika Maadhimisho ya Miaka 30 ya Chama cha Mabenki Tanzania (TBA ) hafla iliyofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Kwanza Resort Kizimkazi Zanzibar Mkoa wa Kusini Unguja.

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kushirikiana na Chama cha Mabenki Tanzania ( TBA ) katika kuijenga sekta ya fedha yenye nguvu, Ubunifu na jumuishi ili kuleta maendeleo ya kibenki na kukuza uchumi wa Taifa.

 

Hayo yamesemwa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla kwa niaba ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi katika hafla ya chakula cha jioni iliyoandaliwa naTBA  katika kuadhimisha Miaka 30 ya chama cha Mabenki Tanzania hafla iliyofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Kwanza Kizimkazi,Mkoa wa Kusini Unguja.

 

Amesema kumekuwa na mabadiliko makubwa ya kimaendeleo katika sekta ya kibenki hatua iliyopelekea kutoka katika mfumo ambao huduma za kibenki zilitengemea matawi na huduma za ana kwa ana, na kuingia katika mfumo wa  kidijitali unaounganisha benki, simu za mkononi na mifumo mbalimbali ya malipo na kurahisisha upatikanaji wa huduma kwa wananchi.

 

Mhe. Hemed amefahamisha kuwa Mfumo wa  kidijitali umechangi kuleta matokeo chanya yaliyowawezesha  Watanzania wengi kupata huduma za kifedha ikiwemo mitaji ya biashara, fursa za kuweka akiba na kuwekeza, kutengeneza ajira pamoja na kukuwa kwa uchumi.


Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amesema tunapoadhimisha miaka 30 ya TBA, ni  vyema washiriki wakatambua kuwa , kwa mujibu wa Mamlaka ya kukuza Uwekezaji Zanzibar (ZIPA), imeeleza kuwa katika nchi za Ukanda wa Afrika Mashariki Zanzibar  imekuwa na ongezeko kubwa la  uwekezaji ambapo kwa kipindi cha kuanzia Novemba 2020 hadi Agosti, 2026 jumla ya miradi 640, yenye mtaji wa takriban Dola za Marekani Bilioani 7.1 imeidhinishwa.

 

Hata hivyo Mhe. Hemed amewahamasisha TBA na wawekezaji wengine kuangalia fursa mbalimbali za uwekezaji hapa Zanzibar ikiwemo kuekeza katika Sekta  Uchumi wa Buluu ambayo uwekezaji wake unaweza  kuchangia zaidi katika ukuaji wa uchumi wa Taifa.

 

Sambamba na hayo Mhe. Hemed amesema Kwa lengo la kuimarisha mazingira bora ya uwekezaji, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inaendelea kuwekeza katika miundombinu ya kimkakati ikiwemo ujenzi wa barabara mijini na vijijini, kuwekeza katika nishati ya uhakika ya umeme na maji pamoja na miundombinu ya bandari na Viwanja vya Ndege.

 

Aidha, Serikali imeimarisha Sera bora za uwekezaji, mazingira rafiki ya biashara yanayovutia uwekezaji pamoja kuanzishwa mfumo Jumuishi wa Taarifa za Ardhi (LARIS) unaotunza kumbukumbu na kuhakikisha usalama wa umiliki wa ardhi ambayo ni rasilimali muhimu katika uwekezaji.

 

Nae Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BOT) Dkt. Rahma Salim Mahfoudh amesema    mchango wa TBA unaonekana katika  maeneo mbalimbali nchini kama vile kuekeza katika Miradi ya Kimkakati ya Taifa, kutoa mikopo iliyosaidia kukuwa na kuimarika kwa uchumi na uwekezaji pamoja na kutoa elimu ya kifedha kwa wateja wao kwa lengo la kuhakikisha uwepo wa matumizi mazuri ya fedha kwa ukuaji bora wa uchumi wa Taifa.

 

Dkt. Rahma amezishauri Taasisi za kifedha nchini kuwa wabunifu katika kutanua wigo mpana kwa kutoa huduma bora ndani na nje ya nchi sambamba na kujiandaa katika matumizi ya Mifumo ya kidijitali ikiwemo matumizi ya Akili Mnemba katika kufikisha huduma karibu zaidi kwa wateja na kwa usalama zaidi.

 

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama cha Mabenki Tanzania (TBA ) Bw.Theobald Sabi amesema mafanikio makubwa yamepatikana ndani ya miaka 30 ya Chama hicho ikiwa ni pamoja na kuimarika kwa usimamizi na uwekezaji katika sekta ya fedha na kuwa sehemu ya ukuaji wa uchumi wa Tanzania.

 

Amefahamisha kuwa TBA inawakilisha Benki na Taasisi za kifedha zaidi ya 42 ambazo  zimekuwa sehemu ya madiliko katika uchumi wa Tanzania kwa kuwekeza katika miradi ya Kimkakati ya Taifa jambo ambalo limesaidia kuongezeka kwa ajira, kutanuka kwa huduma za kiuchumi na kijamii pamoja na  kukuwa pato la Taifa.

 

Bwana Sabi amebainisha kuwa TBA inaendelea kuekeza katika Mifumo madhubuti ya Kielektroniki ambayo italeta mapinduzi makubwa ya kidijitali na ujumuishi wa kifedha na kutambua hatari yoyote ikitokezea ambapo kwa sasa mifumo hio imesaidia kufikisha huduma za kibenki mikononi mwa wateja.

 

Mapema Mkuu wa Mkoa wa Kusini Unguja Ndugu Hamida Mussa Khamis amekipongeza Chama cha Mabenki Tanzania kwa kuamua kuadhimisha miaka 30 ya chama hicho Visiwani Zanzibar jambo linalodhihirisha umoja na mshikamano uliopo katika pande zote mbili za Muungao.

 

Bi. Hamida mewakaribisha wawekezaji kuja kuekeza Zanzibar hasa katika Mkoa wa Kusini Unguja Mkoa ambao unakuwa kwa kasi katika shughuli za uwekezaji na Utalii.






Imetolewa na Kitengo cha Habari ( OMPR )

Leo tarehe …05 / 09 / 2026

Post a Comment

0 Comments