Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kushirikiana na Sekta Binafsi katika kujenga mazingira rafiki yanayowezesha uwekezaji na biashara kukua na kuzalisha ajira nyingi zaidi hususan kwa vijana na wanawake.
Ameyasema Hayo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla kwa niaba ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt Hussein Ali Mwinyi katika ufunguzi wa Tamasha la Tatu (3) la FAHARI YA ZANZIBAR lililofanyika katika Viwanja vya Mnazi Mmoja Mkoa wa Mjini Magharibi.
Amesema Serikali ya mapinduzi ya Zanzibar itazidi kuimarisha mifumo ya utoaji wa huduma ili Zanzibar iwe mahali salama penye ushindani kwa wawekezaji na kuhakikisha kuwa wananchi wanashiriki na kunufaika na fursa zinazotokana na uwekezaji.
Mhe. Hemed amesema ili kufikia azma hio ni wajibu wa Wizara ya Vijana na Uwezeshaji wakishirikiana na Wakala wa Uwezeshaji wananchi kiuchumi kuendelea kubuni na kutekeleza program bunifu na kuimarisha mifumo ya utoaji wa huduma kidijitali ili huduma zinazotolewa zilete matokeo chanya katika kuongeza uzalishaji, ajira na kipato kwa wananchi.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amewasisitiza viongozi kuongeza ushirikiano na kuboresha huduma zinazotolewa na Wizara na Taasisi za Serikali ili kupunguza vikwazo visivyo vya lazima, kurahisisha upatikanaji wa huduma za Serikali na kuharakisha utekelezaji wa Sera na mipango inayochochea ukuaji wa wa sekta binafsi.
Sambamba na hayo Mhe. Hemed amewakumbusha wajasiriliamali suala zima la ubunifu, uwajibikaji na uadilifu kwa kuitumia vizuri mikopo wanayopatiwa kwa malengo yaliyopangwa na kurejesha kwa wakati ili wananchi wengine wapate fursa hio.
Aidha, Makamu wa pili wa rais wa Zanzibar amewahimiza vijana kutumia elimu, maarifa na Teknolojia kuanzisha biashara bunifu na kutumia fursa zinazotolewa na Serikali badala ya kusubiri ajira kutoka Serikalini huku wakitambua kuwa wao ndio nguvu kazi na mtaji mkubwa wa Taifa.
Nae Waziri wa Vijana, Ajira na Uwezeshaji Mhe. Shaban Ali Othman ameesema Wizara kupitia Wakala wa Uwezeshaji wananchi kiuchumi Zanzibar (ZEEA ) watahakikisha wanaendelea kufanya kazi kwa karibu na wafanyabiashara na wajasiriamali katika kuwapatia elimu ya fedha na mikopo ili waweze kunyanyua mitaji yao na kukuza biashara zao.
Mhe. Shaaban ameahidi kuzifanyia kazi changamoto zinazowakabili wafanyabiashara na wajasiriamali ikiwemo uhaba wa upatikanaji wa mikopo na vifaa kwa ajili ya wajasiriamali kwa kuhakikisha ZEEA inawafikia wajasiriamali wengi Unguja na Pemba.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa uwezeshaji wananchi kiuchumi Zanzibar Ndg.Juma Burhan Mohammed amesema Tamasha la Fahari ya Zanzibar limekuwa jukwaa muhimu kwa wafanyabiashara na wajasiriamali kufungua fursa za masoko na kuonesha ithibati ya kujenga uchumi jumuishi.
Burhani amefahamisha kuwa hadi kufikia mwezi Agosti 2026, ZEEA imetowa mafunzo ya uwezeshaji wananchi kiuchumi kwa wajasiriamali na wafanyabiashara wapatao Elf 23 Unguja na Pemba kwa lengo lakuhakikisha wanafanya biashara zao kwa uweledi mkubwa.
Burhani amesema ZEEA inakabiliwa na changamoto ya kiwango kidogo cha utowaji wa mikopo kulingana na uhitaji mkubwa uliopo, uhaba wa ajira sambamba na kuwepo mapungufu katika Sheria No. 2 ya mwaka 2022 Sheria ya Wakala wa Uwezeshaji wananchi kiuchumi Zanzibar, hivyo ameiomba Serikali kuyapatia ufumbuzi changamoto hizo ili kuweza kufikia malengo waliojiwekea.
Akitoa salamu za Stanbic Banki Tanzania ndugu Fredrick Max ambao ndio wadhamini Mkuu wa Tamasha hilo la Tatu ( 3 ) la Fahari ya Zanzibar amesema Benki hio itaendelela kufanya Kazi na ZEEA kwa kuwawezesha wafanyabiashara na wajasiriamali kuweza kukuza mitaji yao na kutimiza malengo waliyojiwekea.
Max amesema wajasiriamali wanapowezeshwa kwa kupatiwa mitaji, kujengewa uwezo na kupatiwa vitendea kazi husaidia huongezeka thamani bishara zao na kuweza kupata masoko ndani na nje ya nchi.
Mapema makamu wa pili wa rais wa Zanzibar ametembelea na kukagua mabanda mbali mbali ya taasisi za serikali na sekta binafsi na kujionea shuguli mbali mbali zinazofanya na wajasiriamali na sekta nyengine za serikali.
Imetolewa na Kitengo cha Habari ( OMPR )
Leo tarehe …05 / 09 / 2026
..............................
Makamu wa pili wa rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla akitembelea na kukagua mabanda mbali mbali ya taasisi za serikali na sekta binafsi wakati wa ufunguzi wa Tamasha la Tatu (3) la FAHARI YA ZANZIBAR lililofanyika katika Viwanja vya Mnazi Mmoja Mkoa wa Mjini Magharibi.
0 Comments