6/recent/ticker-posts

Makamu wa pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed  Suleiman Abdulla ameongoza Kikao kazi juu ya Kupambana na kujikinga na Mvua za El-NIN0 zinazotarajiwa kunyesha Oktoba hadi Disemba 2026 kilichofanyika katika Ukumbi wa Uchaguzi House Maisara Mkoa wa Mjini Magharibi.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla ameongoza kikao kazi juu ya Kupambana na kujikinga na Mvua za El-NIN0 zinazotarajiwa kunyesha Oktoba hadi Disemba 2026.

Kikao hicho kilichofanyika leo Septemba 03, 2026 katika Ukumbi wa Tume ya Uchaguzi Maisara, Mhe. Hemed ambae pia ni Mwenyekiti wa kamati ya Maafa Zanzibar amepokea taarifa mbali mbali kutoka kwa wataalamu wa hali ya hewa pamoja na uongozi wa kamisheni ya kupambana na Maafa Zanzibar.

Amesema kuwa wakati Taifa likijipanga kupambana na kujikinga na Maafa yanayoweza kutokea kufuatia mvua hizo za EL NINO ni wajibu wa kila mwananchi kuhakikisha anachukua tahadhari   juu ya mvua hizo.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amewaelekeza wajumbe wa kamati hio kuhakikisha kunakuwepo na ushirikishwaji wa Taasisi za Serikali na Taasisi binafsi kufahamu ukubwa wa tatizo hilo ili kuhakikisha mvua hizo hazileti athari kwa  wananchi na mali zao.

Mhe. Hemed amesema wakati umefika kila Wizara, Taasisi na mtu mmoja mmoja kutoa  elimu kwa watendaji wao na jamii iliyowazunguka juu ya mvua za EL NINO ambayo itawasaidia kuongeza umakini katika kupambana na kukabiliana na Majanga yanayoweza kutokea.

Sambamba na hayo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar ameitaka Wizara ya habari, sanaa, utamaduni,na michezo kuhakikisha wanavielekeza vyombo vya habari vya serikali na binafsi kutoa taaaluma kwa wananchi juu ya athari za mvua zinazotarajiwa kunyesha.

Aidha Mhe. Hemed amewataka viongozi wa dini, walimu wa madrasa na taasisi nyengine kuyatumia majukwa kutoa elimu na tahadhari kwa wananchi hususan wanaoishi sehemu hatarishi juu ya kutafuta sehemu salama za kuishi na kufanyia shughuli zao kabla ya mvua hizo kuanza ambazo zitadumu wa mud wa miezi mitatu.

Wakitoa taarifa za kitaalamu juu ya mvua hizo Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya hewa Kanda ya Zanzibar Ndg.Masoud Makame Faki na Mkurugenzi wa Kamisheni ya Maafa Zanzibar ndugu Makame Khatib Makame wamesema mvua hizo zinasababishwa na kupanda kwa Joto la bahari ambalo linatarajiwa kupanda hadi kufikia nyuzi joto 3.6 C na kutegemewa kupata mvua kubwa za EL-NINO.

Wamesema kuwa taasisi zao zimejipanga katika kutoa elimu kwa wananchi wote ili kuweza kuwasaidia kujikinga na maadhara ambayo yanaweza kujitokeza kupitia mvua hizo na kutoa ushauri kwa wananchi kuhakisha wanafuatilia taarifa zinazotolewa na Mamlaka ya hali ya Hewa na Serikali kwa ujumla ili kujua mwenendo wa hali ya hewa nchini.

Nao washiriki wa kikao hicho wameahidi kutoa elimu kwa wananchi wote wa Zanzibar hususan wale wanaoishi katika maeneo hatarishi kuhama na kutafuta sehemu nyengine za kuishi kwa kipindi chote cha mvua kubwa zinatarajiwa kunyesha.

Wakati huo huo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amepokea taarifa juu ya mwenendo wa matayarisho ya Mashindano ya Afcon  kutoka kwa kamati saidizi zinazoelezea hatua za utekelezaji wa mataarisho hayo.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amesema ameridhiswa na taarifa hio na  kuwasisitiza wajumbe wa kamati hizo kuhakikisha wanaongeza nguvu za ziada katika kuwasimamia wakandarasi wa miradi inayoendelea kujengwa ili iweze kukamilika kwa wakati sambamba na kuyatekeleza maelekezo ya mashindano ya AFCON ili kuweza kufikia malengo yaliyokusudiwa.

Imetolewa na kitengo cha Habari ( OMPR )

tarehe  03 / 09 / 2026.

Post a Comment

0 Comments