Washiriki kutoka Taasisi mbali mbali za Serikali wakijadili mwelekeo wa msimu wa mvua za vuli 2026, katika Ukumbi wa ASSP, Maruhubi, Wilaya ya Mjini.
Na.Khadija Mgeni
Jamii imetakiwa kuchukua tahadhari za mapema kutokana na mvua kubwa zinazotarajiwa kunyesha kuanzia mwanzoni mwa mwezi Oktoba hadi Disemba 2026, ambazo zinaweza kuambatana na vipindi vya mvua kubwa vinavyohusishwa na hali ya El Niño.
Akitoa kauli hiyo Naibu Mkurugenzi wa Kamisheni ya Kukabiliana na Maafa Zanzibar, Muhidin Ali Muhidini, katika kikao cha kujadili mwelekeo wa msimu wa mvua za vuli 2026, kilichofanyika katika Ukumbi wa ASSP, Maruhubi, Wilaya ya Mjini.
Alisema ni vyema jamii kulichukulia kwa umakini suala la mvua hizo kwa kuchukua tahadhari mapema ili kuepuka athari zinazoweza kusababisha kupoteza maisha ya watu na mali zao.
Aidha, aliitaka jamii inayoishi katika maeneo hatarishi, ikiwemo mabondeni, njia za maji, Mto barafuku, Ziwamaboga, Jangamizini na maeneo mengine hatarishi, kuhama katika maeneo hayo ili kujiepusha na athari zinazoweza kusababishwa na mvua kubwa.
Nae Mkurugenzi wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) Ofisi ya Zanzibar, Masoud Makame Faki, alisema mvua hizo zinatarajiwa kuanza mwanzoni mwa mwezi Oktoba, ambapo maeneo mbalimbali ya Unguja na Pemba yanatarajiwa kupata mvua hizo na huenda Baadhi ya maeneo yakaathirika kutokana na mvua kubwa zinazotarajiwa.
Alisema wananchi wanatakiwa kujiandaa mapema kwa kuhakikisha usafi wa mazingira unaimarishwa ili kuepuka milipuko ya magonjwa yanayoweza kujitokeza kutokana na maji mengi na uchafu wa mazingira.
Aidha, alisema mvua hizo zinaweza kuambatana na radi na upepo mkali, hali ambayo inaweza kusababisha athari katika maeneo ya mabondeni, kuanguka kwa miti mikubwa pamoja na kuathiri sekta mbalimbali, ikiwemo uvuvi .
Alifahamisha kuwa maji mengi ya mvua yanapoingia baharini yanaweza kuathiri mwani,shughuli za uvuvi huku baadhi ya maeneo ya mijini, yakiwemo majengo ya Mji Mkongwe, yataadhirika kutokana na mvua hizo.
Ametoa wito kwa wananchi kuchukua tahadhari na kufuata taarifa na maelekezo yanayotolewa na mamlaka husika kuhusu mwenendo wa hali ya hewa.
Kwa upande wake, Mtaalam Bingwa wa Hali ya Hewa Zanzibar, Hassan Khatib Ame, amesema ongezeko la joto duniani linaendelea kuathiri mfumo wa hali ya hewa, hali ambayo inaweza kusababisha mabadiliko katika mwenendo na kiasi cha mvua katika maeneo mbalimbali.
Amesema ongezeko la joto la bahari na hali ya joto kuwa juu ya wastani linaweza kuchangia mabadiliko ya mifumo ya hali ya hewa, huku kukiwa na mwelekeo wa kuwepo kwa mvua kubwa katika msimu wa mvua za Vuli kutokana na athari za El Niño. Kwa mujibu wa utabiri wa hivi karibuni, maeneo ya Afrika Mashariki yanatarajiwa kuwa na uwezekano wa kupata mvua za juu ya wastani katika kipindi cha Oktoba hadi Desemba 2026.
Nae Yussuf iSaid Yussuf kutoka Kamisheni ya Kukabiliana na Maafa alisema Masuala ya maafa ni Masuala mtambuka kila mmoja linamuhusu hivyo kila maeneo yanatarajiwa yanakwenda kuathirika kutokana na taarifa zinazopokelewa kamisheni hiyo.
Alisema wilaya zote za Unguja zinaweza kuathirika kutokana na taarifa zinazopokelewa Kamisheni ya Kukabiliana na Maafa Katika maeneo mahsusi ya ndani ya shehia ikiwemo Wilaya ya Mjini, shehia 32, Magharibi ' A' shehia 27 ,Magharibi ' B 'shehia 16, Wilaya ya Kusini shehia, 9, Wilaya ya kati shehia 6, Kaskazini A Shehia 21 na ,Kaskazini B,shehia 10,


0 Comments