Na.Mwandishi wa Wizara ya Afya Zanzibar.
WIZARA ya Afya Zanzibar imefanya kikao maalumu na Uongozi wa Chuo Kikuu cha Zanzibar (SUZA) kujadili utekelezaji wa agizo la Serikali la kukihamisha Chuo cha Afya Mbweni kutoka SUZA na kuwa chini ya Wizara ya Afya Zanzibar, ambapo baada ya kukamilika kwa mchakato huo chuo hicho kitaendelea kutoa mafunzo ya ngazi ya Cheti na Diploma za afya.
Hatua hiyo pia inalenga kuipa SUZA nafasi ya kuimarisha zaidi utoaji wa elimu ya ngazi ya Shahada (Degree), ikiwemo taaluma ya Udaktari, wakati Wizara ya Afya ikisimamia mafunzo ya ngazi ya Cheti na Diploma kupitia Chuo cha Afya Mbweni.
Akizungumza baada ya kikao hicho, Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Zanzibar, Dkt Mngereza Mzee Miraji, amesema wamekubaliana mambo mawili ya msingi, ikiwemo kuundwa kwa kamati ndogo ya kitaalamu itakayopitia sheria na kanuni zinazohusiana na mchakato huo na kuwasilisha mapendekezo ya hatua za utekelezaji ndani ya muda mfupi.
Amesema jambo la pili ni kuhakikisha mapitio hayo yanaenda sambamba na maandalizi ya wataalamu kutoka Wizara ya Afya watakaohusika na uendeshaji wa chuo hicho, ili baada ya kukabidhiwa Wizara waanze kazi mapema kwa kushirikiana na wataalamu kutoka SUZA.
Amefamisha kuwa mabadiliko hayo yatafanyika kwa utaratibu bila kuathiri shughuli za Chuo cha Afya Mbweni, huku baadhi ya hatua za awali tayari zikianza kutekelezwa na kuongeza kuwa ndani ya wiki mbili kutakuwa na mpango kazi wa utekelezaji utakaoainisha hatua za kukamilisha mchakato huo.
Kwa upande wake, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (SUZA), Profesa Said Ali Hamad, amesema wamejadili kwa pamoja mchakato wa kukirejesha Chuo cha Afya Mbweni na kubainisha mambo matatu muhimu yanayopaswa kufanyiwa kazi. Amesema jambo la kwanza ni suala la Sheria, kwa kuwa Chuo cha Afya Mbweni kilianzishwa kwa mujibu wa sheria baada ya chuo hicho kuunganishwa na SUZA na hatua ya kurejesha chuo hicho Wizara ya Afya ni lazima kurejesha sheria itakayokipa chuo hicho uhalali wa kuendelea na shughuli zake.
Amefahamisha kuwa jambo la pili ni suala la usajili na uendeshaji wa chuo, ambapo baada ya kurejeshwa, Chuo cha Afya Mbweni kinapaswa kusajiliwa na NACTVET ili kiweze kutambuliwa rasmi na kupewa ithibati ya kutoa programu za elimu ya afya katika ngazi zinazokusudiwa ambapo hatua hiyo itazingatia masuala ya wanafunzi waliopo pamoja na wanaotarajiwa kujiunga na chuo hicho, ili mchakato huo usiathiri maendeleo yao ya masomo.
Aidha jambo la tatu amesema ni suala la rasilimali na ushirikiano kati ya SUZA na Wizara ya Afya, ambapo pande hizo zitaendelea kushirikiana na kuhakikisha zinapatikana rasilimali zinazohitajika kwa ajili ya uendeshaji na ufundishaji katika chuo hicho.
Mwisho
0 Comments