6/recent/ticker-posts

Wizara ya Afya Zanzibar Kuimarisha Huduma na Programu Mbalimbali za Afya ya Jamii

Na.Mwandishi Wizara ya Afya Zanzibar.

Wizara ya Afya Zanzibar imefanya kikao kazi na wadau mbalimbali wa sekta ya afya, wanaoshirikiana kwa karibu na Serikali ya Mapinduzi ya   Zanzibar     kwa lengo la kupitia hatua zilizofikiwa na kuweka mikakati ya kuharakisha uanzishwaji wa Taasisi ya Afya ya Jamii Zanzibar.

Kikao hicho kimewakutanisha wadau kutoka (CDC) ya Marekani barani Afrika, (WHO) pamoja na JHPIEGO, ambao wamekuwa wakifanya kazi kwa karibu na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya Afya katika kuimarisha huduma na programu mbalimbali za afya ya jamii.

Hatua ya  kuanzishwa kwa Taasisi ya Afya ya Jamii Zanzibar ipo hatua muhimu ya kitaalamu, baada ya kufanyika mapitio mbalimbali ya nyaraka pamoja na zoezi la kuainisha na kuchanganua majukumu na mifumo iliyopo katika sekta ya afya ambapo kwa sasa, maandalizi yameingia katika hatua ya utekelezaji na kuandaa mazingira ya kuanzishwa rasmi kwa taasisi hiyo.

Akizungumza kuhusu hatua hiyo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Zanzibar Dkt Mngereza Mzee Miraji  amesema kuanzishwa kwa Taasisi ya Afya ya Jamii ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuimarisha mfumo wa uendeshaji na uratibu wa huduma za afya ya jamii.

Amesema taasisi hiyo itakuwa na jukumu la kuratibu majukumu mbalimbali yanayohusiana na afya ya jamii ambayo kwa sasa yanafanyika kupitia taasisi na idara tofauti ndani ya Wizara ya Afya.

Amefahamisha kuwa hatua hiyo inalenga kupunguza utitiri wa taasisi na Idara zenye majukumu yanayofanana, kurahisisha uratibu na kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa programu za afya ya jamii, jambo ambalo linatarajiwa kusaidia Serikali kupata matokeo bora zaidi katika utoaji wa huduma kwa wananchi.

Aidha amesema mchakato huo unaenda sambamba na jitihada za Serikali za kuimarisha huduma za kibingwa, ikiwemo mpango wa kuanzisha Taasisi ya Saratani Zanzibar.

Amesema kwa  upande wa Taasisi ya Saratani, amesema hatua inayofuata ni kuanza mazungumzo rasmi kuhusu uanzishwaji wake, ambayo yanatarajiwa kuanza ndani ya mwaka huu, mchakato huo unaendelea katika hatua za kisheria, huku Serikali ikiangalia kwa haraka ili kufikia utekelezaji.

Amesema ushirikiano na wadau wa sekta ya afya ni muhimu katika kufanikisha hatua hizo, kwani unaiwezesha Serikali kupata utaalamu, uzoefu na usaidizi wa kitaalamu katika kuhakikisha taasisi hizo zinaanzishwa kwa kuzingatia mahitaji ya Zanzibar na viwango vinavyokubalika katika sekta ya afya.

Uanzishwaji wa Taasisi ya Afya ya Jamii Zanzibar unatarajiwa kuwa hatua muhimu katika mageuzi ya mfumo wa afya, kwa kuimarisha uratibu wa huduma za afya ya jamii, kupunguza mwingiliano wa majukumu na kuweka mfumo wenye ufanisi zaidi katika kuwahudumia wananchi.

Mwisho 

Post a Comment

0 Comments