6/recent/ticker-posts

SMZ Imeweka Mpango Madhubuti wa Program ya OKOA MVUVI Zanzibar Yenye Lengo la Kuhakikisha Usalama wa Mvuvi

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe.  Hemed Suleiman Abdulla akimkabidhi bwana Ramadhan Rajab Mtoro leseni inayomtambulisha kufanya shughuli za uvuvi katika uzinduzi wa Programu ya OKOA MVUVI Zanzibar uliofanyika katika Kiwanja cha Magarawa, Uroa Pongwe Mkoa wa Kusini Unguja. 

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeweka mpango madhubuti wa program ya OKOA MVUVI Zanzibar yenye lengo la kuhakikisha usalama wa mvuvi unakuwa ni msingi wa maendeleo ya sekta ya uvuvi.

Hayo yameelezwa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla katika hafla ya uzinduzi wa Programu ya OKOA MVUVI Zanzibar uliofanyika katika Kiwanja cha Magarawa Uroa Pongwe Mkoa wa Kusini Unguja.

Amesema kupitia program hio wavuvi wataweza kupata elimu na ujuzi wa usalama baharini, vifaa muhimu vya uokozi na kuimarishwa kwa mifumo ya uokoaji ili kukabiliana na majanga ya baharini.

Mhe. Hemed amesema sekta ya uvuvi ni miongoni mwa nguzo muhimu ya uchumi wa Buluu inayotoa ajira, kipato,chakula na chanzo muhimu cha biashara hivyo programu ya Okoa Mvuvi itakuza ustawi, usalama na maendeleo ya mvuvi katika maeneo yote ya Zanzibar.

Makamu wa pili wa Rais wa Zanzibar amesema  kwa muda mrefu sasa kumekuwa na ajali na majanga mbalimbali ya baharini yaliyosababisha majeraha, hasara za mali na kupoteza maisha ya watu kutokana na kutotumia vifaa vya usalama,mabadiliko ya hali ya hewa, ukosefu wa mawasiliano ya uhakika baharini pamoja na kutumia vyombo visivyokuwa katika hali ya  usalama.

Sambamba na hayo Makamu wa pili wa Rais wa Zanzibar amesema Serikali itaendelea kuimarisha mazingira bora ya wavuvi kwa kuendelea na ujenzi wa madiko ya kisasa Unguja na Pemba, kuongeza wigo wa masoko ya samaki na kuwapatia mikopo wananchi ili kujiendeleleza kiuchumi ambapo kwa mwaka wa fedha  2026 / 2027 kiasi cha shilingi Bilioni 47.3 zimetengwa kwa ajili ya kuwawezesha wananchi kiuchumi.

Hata hivyo amewasihi wananchi kuendelea kuchangamkia fursa za kiuchumi katika sekta ya uvuvi na kuwasisitiza kuvitunza na kuvitumia kwa utaratibu uliosahihi vifaa watakavyopatiwa ili lengo la program ya Okoa Mvuvi iweze kufikiwa.

Naibu Waziri wa Wizara ya Uchumi wa Buluu na Uvuvi Mhe. Mboja Ramadhan Mshenga amesema program hio inakwenda kumkomboa mvuvi kutokana na majanga na hatari mbali mbali alizokuwa akikabiliana nazo kabla ya kuzinduliwa kwa Program ya Okoa Mvuvi Zanzibar jambo lililokwamisha maendeleo ya wavuvi nchini.

Mhe. Mboja amewasisitiza wavuvi na watumiaji wa bahari kuwa tayari kujifunza katika kuelekea uvuvi wa kisasa uvuvi endelevu wenye kunyanyua kipato cha mvuvi wa Zanzibar.

Amewataka wavuvi kuvitunza vifaa watakavyopatiwa na kuvitumia kwa uangalifu mkubwa sambamba na kulipa kwa wakati mikopo waliyopatiwa ili wavuvi wengine waweze kufaidika na mikopo hio.

Akisoma taarifa ya Kitaalamu juu ya programu ya Okoa Mvuvi, Katibu Mkuu Wizara ya Uchumi wa Buluu na Uvuvi Kepteni Hamad Bakari Hamad amesema program hio ni mfumo mpana wa kutambua na kumrasimisha mvuvi, kumpatia elimu na mafunzo pamoja na kuboresha vyombo na zana za usalama na mawasiliano baharini.

Kepteni Hamad amefahamisha kuwa katika kuimarisha usalama wa mvuvi akiwa wa baharini Wizara kwa kushirikiana na Taasisi mbalimbali zimejipanga kukabiliana na majanga, kuratibu shughuli za utafutaji na uokozi ili kubaini mazingira ya hatari na kutoa huduma ya uokozi kwa haraka.

Amesema katika Wilaya ya Kusini vikundi 15 vya uvuvi vitapatiwa boti za kisasa zikiwa na zana muhimu za uvuvi na vifaa vya msingi vya usalama na kutoa boti za doria na uokozi.

Ametoa wito kwa wavuvi kuvitunza vifaa watakayopatiwa,  kutumia vifaa vya usalama kila wanapokwenda baharini pamoja na kushirikiana na mamlaka husika ili kutambua mabadiliko ya hali ya hewa.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla  akizungumza na Wananchi katika hafla ya Uzinduzi wa Programu ya OKOA MVUVI Zanzibar iliyofanyika  katika Kiwanja cha Magarawa Uroa Pongwe Mkoa wa Kusini Unguja.

Imetolewa na Kitengo cha Habari ( OMPR )

Leo tarehe …10 / 08 / 2026

Post a Comment

0 Comments