6/recent/ticker-posts

RAIS DKT. MWINYI AHIMIZA KUIMARISHWA KWA DIPLOMASIA YA UCHUMI NA MALAYSIA

 

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, akisalimiana na Balozi wa Tanzania Nchini Malaysia, Meja Jenerali Mbaraka Naziad Mkeremy alipofika Ikulu Jijini Zanzibar kwa mazungumzo na kuaga akielekea Kituo chake cha Kazi, mazungumzo hayo yaliyofanyika katika ukumbi wa Ikulu Zanzibar.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amemtaka Balozi wa Tanzania nchini Malaysia, Meja Jenerali Mbaraka Naziad Mkeremy, kutumia nafasi yake kuimarisha diplomasia ya uchumi, hususan katika kuvutia uwekezaji, kukuza biashara na kuongeza watalii kutoka Malaysia wanaotembelea Zanzibar.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo tarehe 17 Agosti 2026, alipokutana na Balozi Mkeremy, aliyefika Ikulu Zanzibar kuaga na kupokea maelekezo kabla ya kuelekea katika kituo chake kipya cha kazi nchini Malaysia.

Amesisitiza umuhimu wa kutangaza fursa za uwekezaji zilizopo Zanzibar katika utalii, hoteli na makaazi, uvuvi, mafuta na gesi pamoja na maeneo mengine ya Uchumi wa Buluu.

Aidha, Rais Dkt. Mwinyi amemtaka Balozi Mkeremy kuimarisha ushirikiano wa Zanzibar na Malaysia katika elimu, ikiwemo kuongeza fursa za ufadhili wa masomo na ushirikiano baina ya vyuo vikuu.

Naye Balozi Mkeremy amesema amepokea maelekezo hayo na kuahidi kuyafanyia kazi katika utekelezaji wa majukumu yake nchini Malaysia.



Post a Comment

0 Comments