Na. Mwandishi Wizara ya Afya Zanzibar.
WIZARA ya Afya Zanzibar imefanya kikao cha kufanya mapitio ya Kitita cha Huduma za Afya (Essential Health Care Package), kinacholenga kubainisha huduma za afya ambazo Serikali itahakikisha zinapatikana kwa wananchi.
Akizungumza mara baada ya kufungua kikao hicho kilichofanyika katika Ukumbi wa Tume ya Uchaguzi, Maisara, na kuwashirikisha wataalamu kutoka hospitali mbalimbali, Mkurugenzi wa Mipango, Sera na Utafiti wa Wizara ya Afya Zanzibar, Omar Mwalim Omar, amesema mahitaji ya huduma za afya ni mengi, huku rasilimali zilizopo zikiwa chache, hivyo kuna umuhimu wa kuweka vipaumbele katika huduma zitakazojumuishwa kwenye kitita hicho.
Amesema uamuzi wa kuamua huduma zipi ziingizwe kwenye kitita hicho si jambo linaloweza kuamuliwa na mtu mmoja, bali linahitaji ushirikishwaji wa wataalamu mbalimbali ambao watapitia orodha ya huduma zilizopendekezwa na kutoa maoni yao kwa kuzingatia ushahidi pamoja na uzoefu wanaoupata katika mazingira yao ya kazi.
Amefahamisha kuwa kikao hicho kimewakutanisha wataalamu kutoka ngazi mbalimbali, wakiwemo madaktari na madaktari bingwa, kwa lengo la kupitia kwa kina orodha ya huduma zilizopendekezwa na kutoa mapendekezo ya huduma zinazopaswa kupewa kipaumbele na kuingizwa katika kitita hicho.
Amesema baada ya wataalamu hao kukamilisha mapitio na kutoa mapendekezo yao, kitita hicho kitakuwa msingi wa hatua nyingine, ikiwemo kwa mifuko ya bima ya afya kutumia kitita hicho katika kubainisha huduma zitakazoweza kuingizwa katika mifumo yao ya bima.
Aidha, amesema mchakato huo hautaishia kwa wataalamu pekee, kwani baada ya hatua hiyo Wizara itakutana na wakuu wa programu mbalimbali za afya pamoja na wananchi na makundi yanayowakilisha wagonjwa, ambao nao watapata fursa ya kutoa maoni yao kuhusu huduma zinazopaswa kupewa kipaumbele.
Amesema lengo ni kupata Kitita cha Huduma za Afya kitakachokuwa kimefanyiwa mapitio na kuridhiwa kwa ushirikishwaji wa wataalamu, wananchi na makundi mbalimbali, ili kuhakikisha huduma zitakazowekwa kwenye kitita hicho zinaendana na mahitaji halisi ya wananchi na rasilimali zilizopo.
Kwa upande wake, Mratibu wa Mapitio ya Kitita cha Huduma za Afya, Sauda Ismail, amesema hatua ya kwanza katika mchakato huo ni kupitia huduma zote zilizopo kwenye kitita cha sasa, kwa lengo la kuhakikisha zinaendana na mahitaji ya wananchi na hali halisi ya utoaji wa huduma za afya nchini.
Amesema katika hatua hiyo, wataalamu watapitia huduma hizo na kubaini iwapo kuna huduma muhimu ambazo hazijaingizwa kwenye kitita, na endapo zitabainika kuwa hazipo, wataalamu watashauri huduma hizo zinapaswa kuingizwa katika ngazi gani ya huduma za afya, ikiwemo hospitali za Wilaya, hospitali za Mkoa, Vituo vya afya kulingana na aina na mahitaji ya huduma husika.
Amesema baada ya wataalamu kufanya mapitio hayo, maoni yatakusanywa kutoka kwa jamii kupitia wawakilishi wao, kwa kuwa wananchi ndio walengwa na wanufaika wa huduma hizo za afya.
Amesema baada ya kukamilika kwa hatua zote za ushirikishwaji, mapendekezo yatapitiwa tena na wataalamu wa ngazi za juu, ambao watatoa tathmini ya mwisho kabla ya kupatikana Kitita cha Huduma za Afya kitakachotumika kama mwongozo wa huduma zinazopaswa kutolewa kwa wananchi katika ngazi mbalimbali za mfumo wa afya.
MWISHO.
0 Comments