Na.Mwandishi Wizara ya Afya Zanzibar.
WIZARA ya Afya Zanzibar imefanya kikao cha pamoja na Ubalozi wa Marekani nchini Tanzania kwa lengo la kujadili kwa kina namna ya kutekeleza makubaliano ya ushirikiano katika sekta ya afya, kufuatia makubaliano yaliyofikiwa kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Marekani yenye thamani ya takribani Dola za Marekani bilioni 3.1.
Kikao hicho kimefanyika kwa pamoja na Mkurugenzi Mkuu wa Wizara ya Afya Zanzibar, wakurugenzi na wataalamu wa sekta ya afya pamoja na timu kutoka Ubalozi wa Marekani, kwa ajili ya kuweka mikakati ya kuhakikisha uwekezaji huo unaendana na vipaumbele vya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na kuleta matokeo mazuri katika utoaji wa huduma za afya kwa wananchi.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Zanzibar, Dkt, Mngereza Mzee Miraji, amesema kikao hicho ni sehemu ya hatua za kuanza kuweka mpango madhubuti wa utekelezaji wa makubaliano hayo, ambapo Zanzibar inalenga kuhakikisha fursa hiyo inaunganishwa na uwekezaji unaofanywa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Amefahamisha kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imekuwa ikiongeza kwa kasi uwekezaji katika sekta ya afya, ikilinganishwa na miaka ya nyuma huku akisema kuwa katika kipindi cha miaka mitano iliyopita Serikali imewekeza karibu Shilingi bilioni 130, na miaka mitano ijayo imepanga kuwekeza takribani Shilingi trilioni 1.016 katika sekta hiyo.
Aidha amesema kuwa kwa msingi huo, ni muhimu uwekezaji unaotokana na ushirikiano huo wa kimataifa uende sambamba na mipango ya Serikali, ili rasilimali zinazopatikana zitumike kwa ufanisi na kuongeza juhudi zinazofanywa na Zanzibar.
Ameeleza kuwa moja ya maeneo makubwa yaliyojadiliwa katika kikao hicho ni nguvu kazi katika sekta ya afya, eneo la Maabara, mifumo ambapo Serikali inahitaji kuwa na wataalamu wa kutosha, wenye ujuzi na maarifa yanayoendana na mabadiliko ya teknolojia na mahitaji ya sasa ya huduma za afya na kupitia ushirikiano huo.
Kwa upande wa mwakilishi kutoka Ubalozi wa Marekani nchini Tanzania , Jessica Greene, ambae ni Mkuu wa Ofisi ya mashirikiano nchini Tanzania akiongozana na timu ya wataalamu wa afya , amesema ushirikiano huo unalenga kutumia uzoefu na utaalamu uliopo kwa upande wa Marekani kusaidia kuimarisha mifumo ya afya Zanzibar, huku mipango hiyo ikiandaliwa kwa kuzingatia mahitaji na vipaumbele vilivyowekwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya Afya.
Amesema ushirikiano wa karibu kati ya Wizara ya Afya Zanzibar na Ubalozi wa Marekani utasaidia kuhakikisha maeneo yaliyokubaliwa yanafanyiwa kazi kwa utaratibu na kwa kuzingatia malengo yaliyowekwa katika makubaliano.
Ushirikiano huo unaelezwa kuwa ni hatua muhimu katika kuunganisha uwekezaji wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na fursa zinazotokana na ushirikiano wa kimataifa, huku sekta ya afya ikitarajiwa kuwa miongoni mwa sekta zitakazonufaika zaidi na uwekezaji huo.
Mwisho
0 Comments