Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (Katikati), akiongoza kikao chake na Mwakilishi mpya wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) nchini Tanzania, Bi. Jana Bricco (wa kwanza kulia), aliyefika kujitambulisha tangu ashike nyadhifa hiyo pamoja na kufanya mazungumzo katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaam, ambapo walijadili masuala mbalimbali yanayohusu ushirikiano kati ya Tanzania na IMF, ambao umedumu kwa miongo kadhaa tangu miaka ya 1960.
Na. Benny Mwaipaja, Dar es Salaam.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar,
amelishukuru Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) kwa
mchango wake kwa Tanzania tangu kuanza kwa ushirikiano
kati yake na Shirika hilo, akieleza kuwa ushirikiano huo
umeendelea kuwa muhimu katika kuimarisha uchumi na
utekelezaji wa ajenda za maendeleo nchini.
Ametoa Shukran hizo wakati alipokutana na kufanya
mazungumzo na Mwakilishi mpya wa IMF nchini Tanzania,
Bi.Jana Bricco, ambaye ameanza rasmi majukumu yake
nchini, ambapo walijadili masuala mbalimbali yanayohusu
ushirikiano kati ya Tanzania na IMF, ambao umedumu kwa
zaidi ya miongo sita tangu uanzishwe miaka ya 1960.
Mhe. Balozi Omar amesema Serikali itaendelea kuimarisha
ushirikiano na IMF katika kufanikisha ajenda ya maendeleo
ya Tanzania, ikiwemo utekelezaji wa Dira ya Taifa ya
Maendeleo 2050 pamoja na mwelekeo wa kimkakati wa
Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano unaofuata ambayo
ni maeneo yenye manufaa kwa pande zote na yanayochangia
utekelezaji wa ajenda ya maendeleo ya Tanzania.
“Tumekuwa na ushirikiano na IMF kwa muda mrefu, tangu
miaka ya 1960 hadi leo, na tumeendelea kushirikiana katika
maeneo mbalimbali yanayolenga kuimarisha uchumi wa nchi
na kufanikisha ajenda yetu ya maendeleo,” alisema Mhe.
Balozi Omar.
Aliongeza kuwa Tanzania inathamini ushirikiano huo,
hususan katika kufuatilia mwenendo wa ukuaji wa uchumi,
sera za fedha na sera za kiuchumi (monetary policy na fiscal
policy), pamoja na matokeo ya utekelezaji wa sera hizo.
Mhe. Balozi Omar alisema wataendelea kutazamia kwa
pamoja maendeleo ya sekta binafsi na mwenendo wa bei za
bidhaa na huduma, ikiwemo mfumuko wa bei (inflation),
maeneo ambayo yameendelea kuwa sehemu muhimu ya
majadiliano kati ya Tanzania na IMF.
Aidha, Mhe. Balozi Omar ametoa wito kwa Mwakilishi huyo
mpya wa IMF kutembelea maeneo mbalimbali nchini ili
kupata fursa ya kujionea kwa vitendo maendeleo
yanayotekelezwa na Serikali, hususan miradi mikubwa ya
kimkakati, kama vile Bwawa la kuzalisha Umeme la Mwalimu
Julius Nyerere.
“Mbali na miradi ya kimkakati, nakukaribisha kutembelea
maeneo ya utalii na uzalishaji, hususan katika sekta ya kilimo
na maeneo mengine yenye mchango mkubwa katika shughuli
za kiuchumi nchini, na zitakusaidia kupata uelewa mpana
zaidi kuhusu fursa, maendeleo na changamoto zilizopo nchini,
hivyo kuwezesha majadiliano na ushirikiano wenye tija zaidi
kati ya Tanzania na IMF.” alisema Mhe. Balozi Omar
Kwa Upande wake Mwakilishi mpya wa Shirika la Fedha la
Kimataifa (IMF) nchini Tanzania, Bi. Jana Bricco,
ameipongeza Tanzania kwa kukamilisha kwa mafanikio
Mpango wa Extended Credit Facility (ECF) inayohusisha
upatikanaji wa mkopo nafuu kwa ajili ya kuimarisha uchumi
wa nchi kupitia sekta za uzalishaji na huduma za jamii na
Resilience and Sustainability Facility (RSF) ya kukabiliana na
athari za mabadiliko ya tabianchi, mafanikio ambayo
yamechangiwa na kuimarika kwa utulivu wa uchumi jumla,
uendelevu wa bajeti na kupungua kwa kiwango cha deni la
Taifa.
Bi. Bricco amesema mafanikio hayo yalibainishwa na
kuthaminiwa katika kikao cha Bodi ya IMF, na kukamilika
kwa programu hiyo kunatoa fursa ya kuanza ukurasa mpya
katika uhusiano kati ya Tanzania na IMF, utakaojikita zaidi
katika mashauriano ya sera, ufuatiliaji wa uchumi na kujenga
uwezo wa kitaalamu,
“Kukamilika kwa ECF-RSF hakumaanishi mwisho wa
ushirikiano kati ya Tanzania na IMF, bali ni fursa ya
kuubadilisha na kuuimarisha uhusiano huo kulingana na
hatua mpya ya maendeleo ya Tanzania, huku IMF ikiendelea
kuwa mshirika katika juhudi za kuimarisha ustawi wa uchumi,
uendelevu wa sera na kufanikisha matarajio ya maendeleo ya
Taifa kwa mwaka 2050” alisema Bi. Bricco.
Aliongeza kuwa IMF iko tayari kuendelea kushirikiana na
Serikali katika kipindi kijacho kwa kutoa ushauri wa sera
unaoendana na mahitaji ya nchi pamoja na msaada wa
kujenga uwezo katika maeneo yatakayopewa kipaumbele
katika utekelezajinwa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
“IMF inaona nafasi kubwa ya kuendelea kuunga mkono
utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, malengo na
maeneo yaliyolengwa katika programu zilizokamilika yana
mwingiliano mkubwa na matarajio ya Tanzania ya kujenga
uchumi imara, shindani na wenye uwezo wa kutoa fursa zaidi
kwa wananchi” alisema Bi. Bricco
Kikao hicho kilihudhuriwa pia na Kaimu Katibu Mkuu ambaye
pia ni Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Bw. Nsubili
Joshua, Kamishna Msaidizi wa Idara ya Fedha za Nje, Wizara
ya Fedha, Bw. Robert Mtengule, Kamishna Msaidizi Idara ya
Uchambuzi wa Sera, Wizara ya Fedha, Bw. Juma Mkabakuli
na maafisa wengine waandamizi wa Wizara ya Fedha na IMF.
Mwakilishi mpya wa Shirika la Fedha la Kimataifa IMF nchini Tanzania, Bi. Jana Bricco, akizungumza wakati wa kikao na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (hayupo pichani), kilichofanyika katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaam, ambapo aliipongeza Tanzania kwa kukamilisha kwa mafanikio Mpango wa Extended Credit Facility (ECF) inayohusisha upatikanaji wa mkopo nafuu kwa ajili ya kuimarisha uchumi wa nchi kupitia sekta za uzalishaji na huduma za jamii na Resilience and Sustainability Facility (RSF) ya kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi, mafanikio ambayo yamechangiwa na kuimarika kwa utulivu wa uchumi jumla, uendelevu wa bajeti na kupungua kwa kiwango cha deni la Taifa.
.jpg)
.jpg)


.jpg)
.jpg)
0 Comments