6/recent/ticker-posts

WAZIRI OMAR ASHUKURU IMF KWA USHIRIKIANO WA MUDA MREFU NA TANZANIA

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (Katikati), akiongoza kikao chake na Mwakilishi mpya wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) nchini Tanzania, Bi. Jana Bricco (wa kwanza kulia), aliyefika kujitambulisha tangu ashike nyadhifa hiyo pamoja na kufanya mazungumzo katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaam, ambapo walijadili masuala mbalimbali yanayohusu ushirikiano kati ya Tanzania na IMF, ambao umedumu kwa miongo kadhaa tangu miaka ya 1960.

Na. Benny Mwaipaja, Dar es Salaam.

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar, 

amelishukuru Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) kwa 

mchango wake kwa Tanzania tangu kuanza kwa ushirikiano 

kati yake na Shirika hilo, akieleza kuwa ushirikiano huo 

umeendelea kuwa muhimu katika kuimarisha uchumi na 

utekelezaji wa ajenda za maendeleo nchini.


Ametoa Shukran hizo wakati alipokutana na kufanya 

mazungumzo na Mwakilishi mpya wa IMF nchini Tanzania, 

Bi.Jana Bricco, ambaye ameanza rasmi majukumu yake 

nchini, ambapo walijadili masuala mbalimbali yanayohusu 

ushirikiano kati ya Tanzania na IMF, ambao umedumu kwa 

zaidi ya miongo sita tangu uanzishwe miaka ya 1960.

 

Mhe. Balozi Omar amesema Serikali itaendelea kuimarisha 

ushirikiano na IMF katika kufanikisha ajenda ya maendeleo 

ya Tanzania, ikiwemo utekelezaji wa Dira ya Taifa ya 

Maendeleo 2050 pamoja na mwelekeo wa kimkakati wa 

Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano unaofuata ambayo 

ni maeneo yenye manufaa kwa pande zote na yanayochangia 

utekelezaji wa ajenda ya maendeleo ya Tanzania.

 

“Tumekuwa na ushirikiano na IMF kwa muda mrefu, tangu 

miaka ya 1960 hadi leo, na tumeendelea kushirikiana katika 

maeneo mbalimbali yanayolenga kuimarisha uchumi wa nchi 

na kufanikisha ajenda yetu ya maendeleo,” alisema Mhe. 

Balozi Omar.

 

Aliongeza kuwa Tanzania inathamini ushirikiano huo, 

hususan katika kufuatilia mwenendo wa ukuaji wa uchumi, 

sera za fedha na sera za kiuchumi (monetary policy na fiscal 

policy), pamoja na matokeo ya utekelezaji wa sera hizo.

 

Mhe. Balozi Omar alisema wataendelea kutazamia kwa 

pamoja maendeleo ya sekta binafsi na mwenendo wa bei za 

bidhaa na huduma, ikiwemo mfumuko wa bei (inflation), 

maeneo ambayo yameendelea kuwa sehemu muhimu ya 

majadiliano kati ya Tanzania na IMF.

 

Aidha, Mhe. Balozi Omar ametoa wito kwa Mwakilishi huyo 

mpya wa IMF kutembelea maeneo mbalimbali nchini ili 

kupata fursa ya kujionea kwa vitendo maendeleo 

yanayotekelezwa na Serikali, hususan miradi mikubwa ya 

kimkakati, kama vile Bwawa la kuzalisha Umeme la Mwalimu 

Julius Nyerere.

 

“Mbali na miradi ya kimkakati, nakukaribisha kutembelea 

maeneo ya utalii na uzalishaji, hususan katika sekta ya kilimo 

na maeneo mengine yenye mchango mkubwa katika shughuli 

za kiuchumi nchini, na zitakusaidia kupata uelewa mpana 

zaidi kuhusu fursa, maendeleo na changamoto zilizopo nchini, 

hivyo kuwezesha majadiliano na ushirikiano wenye tija zaidi 

kati ya Tanzania na IMF.” alisema Mhe. Balozi Omar

 

Kwa Upande wake Mwakilishi mpya wa Shirika la Fedha la 

Kimataifa (IMF) nchini Tanzania, Bi. Jana Bricco, 

ameipongeza Tanzania kwa kukamilisha kwa mafanikio 

Mpango wa Extended Credit Facility (ECF) inayohusisha 

upatikanaji wa mkopo nafuu kwa ajili ya kuimarisha uchumi 

wa nchi kupitia sekta za uzalishaji na huduma za jamii na 

Resilience and Sustainability Facility (RSF) ya kukabiliana na 

athari za mabadiliko ya tabianchi, mafanikio ambayo 

yamechangiwa na kuimarika kwa utulivu wa uchumi jumla, 

uendelevu wa bajeti na kupungua kwa kiwango cha deni la 

Taifa.

 

Bi. Bricco amesema mafanikio hayo yalibainishwa na 

kuthaminiwa katika kikao cha Bodi ya IMF, na kukamilika 

kwa programu hiyo kunatoa fursa ya kuanza ukurasa mpya 

katika uhusiano kati ya Tanzania na IMF, utakaojikita zaidi 

katika mashauriano ya sera, ufuatiliaji wa uchumi na kujenga 

uwezo wa kitaalamu,

 

“Kukamilika kwa ECF-RSF hakumaanishi mwisho wa 

ushirikiano kati ya Tanzania na IMF, bali ni fursa ya 

kuubadilisha na kuuimarisha uhusiano huo kulingana na 

hatua mpya ya maendeleo ya Tanzania, huku IMF ikiendelea 

kuwa mshirika katika juhudi za kuimarisha ustawi wa uchumi, 

uendelevu wa sera na kufanikisha matarajio ya maendeleo ya 

Taifa kwa mwaka 2050” alisema Bi. Bricco.

 

Aliongeza kuwa IMF iko tayari kuendelea kushirikiana na 

Serikali katika kipindi kijacho kwa kutoa ushauri wa sera 

unaoendana na mahitaji ya nchi pamoja na msaada wa 

kujenga uwezo katika maeneo yatakayopewa kipaumbele 

katika utekelezajinwa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

 

“IMF inaona nafasi kubwa ya kuendelea kuunga mkono 

utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, malengo na 

maeneo yaliyolengwa katika programu zilizokamilika yana 

mwingiliano mkubwa na matarajio ya Tanzania ya kujenga 

uchumi imara, shindani na wenye uwezo wa kutoa fursa zaidi 

kwa wananchi” alisema Bi. Bricco

 

Kikao hicho kilihudhuriwa pia na Kaimu Katibu Mkuu ambaye 

pia ni Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Bw. Nsubili 

Joshua, Kamishna Msaidizi wa Idara ya Fedha za Nje, Wizara 

ya Fedha, Bw. Robert Mtengule, Kamishna Msaidizi Idara ya 

Uchambuzi wa Sera, Wizara ya Fedha, Bw. Juma Mkabakuli 

na maafisa wengine waandamizi wa Wizara ya Fedha na IMF.

Mwakilishi mpya wa Shirika la Fedha la Kimataifa IMF nchini Tanzania, Bi. Jana Bricco, akizungumza wakati wa kikao na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (hayupo pichani), kilichofanyika katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaam, ambapo aliipongeza Tanzania kwa kukamilisha kwa mafanikio Mpango wa Extended Credit Facility (ECF) inayohusisha upatikanaji wa mkopo nafuu kwa ajili ya kuimarisha uchumi wa nchi kupitia sekta za uzalishaji na huduma za jamii na Resilience and Sustainability Facility (RSF) ya kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi, mafanikio ambayo yamechangiwa na kuimarika kwa utulivu wa uchumi jumla, uendelevu wa bajeti na kupungua kwa kiwango cha deni la Taifa.




Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (Kulia), akiagana na 

Mwakilishi mpya wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) nchini Tanzania, Bi. Jana 

Bricco, aliyefika kujitambulisha tangu ashike nyadhifa hiyo pamoja na kufanya 

mazungumzo katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaam, ambapo 

walijadili masuala mbalimbali yanayohusu ushirikiano kati ya Tanzania na IMF, 

ambao umedumu kwa miongo kadhaa tangu miaka ya 1960.

Post a Comment

0 Comments