Na.Mwandishi Wizara ya Afya Zanzibar.
KAIMU Waziri wa Afya Zanzibar, Dkt, Saada Mkuya Salum, ametembelea Kambi Maalum ya Uchunguzi wa Magonjwa ya Moyo kwa Watoto inayoendelea katika Hospitali ya Lumumba, Unguja, na kueleza kuwa huduma zinazotolewa kupitia kambi hiyo ni hatua muhimu katika kuimarisha afya ya watoto na kupunguza athari zinazotokana na magonjwa ya moyo kwa kuwabaini wagonjwa mapema na kuwawezesha kupata matibabu stahiki.
Kambi hiyo imeandaliwa na Wizara ya Afya Zanzibar kwa kushirikiana na NAHR AL HAYAT kutoka Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), na UAE RED CRESENT ambapo timu ya madaktari bingwa wa magonjwa ya moyo imewasili Zanzibar kutoa huduma za uchunguzi wa kibingwa kwa watoto wenye umri wa kuanzia kuzaliwa hadi miaka 15 kutoka Unguja na Pemba.
Akizungumza mara baada ya kutembelea kambi hiyo, Dkt. Saada amesema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kushirikiana na taasisi na wadau mbalimbali wa maendeleo ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma za afya za kibingwa zenye ubora na zinazofikika kwa urahisi.
Amefahamksha kuwa ujio wa madaktari bingwa itaongezauwezo wa kuwafikia watoto wengi wenye changamoto za moyo ambao walikuwa hawajapatiwa uchunguzi wa kina, huku akiwahimiza wazazi na walezi kutumia kikamilifu fursa hiyo muhimu kwa kuwafikisha watoto wao katika vituo vilivyopangwa.
Aidha, ameeleza kuwa watoto watakaobainika kuwa na matatizo ya moyo yanayohitaji matibabu ya kibingwa zaidi watawezeshwa kupata matibabu nchini India kupitia mpango wa NAHR AL HAYAT UAE na UAE RED CRECENT, kwa kushirikiana na Wizara ya Afya Zanzibar, jambo litakalokuwa na manufaa makubwa kwa wananchi wa zanzibar.
Kwa upande wa, Dkt Juma Ali Makame Mkuu wa Kitengo cha Ushirikiano Kimataifa amesema huduma zinazotolewa zinahusisha uchunguzi wa kina wa magonjwa ya moyo kwa watoto kwa kutumia vifaa vya kisasa, pamoja na kutoa ushauri wa kitabibu kwa wazazi kuhusu namna ya kuwatunza watoto wenye matatizo hayo.
Baadhi ya wazazi na walezi waliopata huduma wameishukuru Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya Afya kwa kuwaletea huduma hizo karibu na wananchi, wakieleza kuwa zimewapa matumaini mapya ya watoto wao kupata matibabu yanayostahili.
Kambi hiyo imeanza kutoa huduma katika Hospitali ya Lumumba tarehe 3 Agosti na itaendelea Kizimkazi tarehe 4 Agosti, na baadae Hospitali ya Chake Chake, Pemba, tarehe 5 na 6 Agosti, ambapo watoto kutoka maeneo mbalimbali wataendelea kupatiwa huduma za uchunguzi wa kibingwa.
Wizara ya Afya Zanzibar imeendelea kuwahimiza wazazi na walezi kuwafikisha watoto wenye dalili za magonjwa ya moyo katika vituo vilivyopangwa, ikisisitiza kuwa uchunguzi wa mapema ni hatua muhimu ya kuokoa maisha na kuhakikisha watoto wanapata matibabu kwa wakati.
Mwisho.
0 Comments