Na.Mwandishi Wizara ya Afya Zanzibar.
Wizara ya Afya Zanzibar kupitia Taasisi ya Utafiti wa Afya Zanzibar (ZAHRI), imesaini makubaliano ya ushirikiano na Chuo Kikuu cha Tiba cha Ninging cha nchini China, yatakayolenga kuimarisha tafiti za afya, kuendeleza ubadilishanaji wa wataalamu na teknolojia, pamoja na kufanya tafiti zitakazosaidia kuimarisha huduma za afya kwa wananchi.
Akizungumza mara baada ya hafla ya utiaji saini wa makubaliano hayo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Zanzibar, Dkt, Mngereza Mzee Miraji, amesema ushirikiano huo unaonesha dhamira ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya kuendelea kuimarisha sekta ya afya kupitia tafiti za kisayansi zinazotoa majibu ya changamoto zinazoikabili jamii.
Alisema makubaliano hayo yamejikita katika maeneo makuu matatu muhimu yatakayosaidia kuleta mageuzi makubwa katika sekta ya afya Zanzibar ambapo eneo la kwanza ni kuimarisha ushirikiano kati ya Wizara ya Afya, Taasisi ya Utafiti wa Afya Zanzibar (ZAHRI) na Chuo Kikuu cha Tiba cha Ninging katika kufanya tafiti mbalimbali zitakazosaidia Serikali kupata ushahidi wa kisayansi wa kufanya maamuzi sahihi kuhusu mipango na sera za afya.
Amefahamisha kuwa eneo la pili linahusu kufanya tafiti maalumu kuhusu magonjwa na changamoto mpya zinazoibuka katika sekta ya afya, ikiwemo ili kubaini namna bora ya kuyadhibiti na kupunguza athari zake kwa jamii.
Aidha, amesema eneo la tatu litajikita katika kufanya tafiti zitakazosaidia kupunguza vifo vya mama na mtoto, akieleza kuwa Serikali imeendelea kuweka nguvu kubwa katika kuimarisha huduma za afya ya uzazi, mtoto na lishe kwa kuwa ni msingi wa kujenga jamii yenye afya bora.
Aliongeza kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na taasisi mbalimbali za ndani na nje ya nchi ili kuhakikisha Zanzibar inanufaika na maendeleo ya sayansi, teknolojia na ubunifu katika sekta ya afya.
Katibu Mkuu huyo alisema kupitia ushirikiano huo, wataalamu wa afya na watafiti wa Zanzibar watanufaika kwa kupata mafunzo ya kitaalamu, kubadilishana uzoefu na kufanya tafiti za pamoja zitakazoongeza uwezo wao wa kitaaluma na kuimarisha huduma wanazozitoa kwa wananchi.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Afya Zanzibar (ZAHRI), Mayasa Salum Ali, alisema kutiwa saini kwa makubaliano hayo ni mafanikio makubwa kwa taasisi hiyo na ni mwanzo wa ushirikiano mpana zaidi katika nyanja za tafiti za afya.
Amesema ZAHRI itaendelea kushirikiana kwa karibu na Chuo Kikuu cha Tiba cha Ninging katika kufanya tafiti mbalimbali zinazolenga kuimarisha afya ya wananchi, hususan katika maeneo yenye changamoto kubwa zinazohitaji kufanyiwa utafiti.
Amesema ushirikiano huo pia utatoa fursa kwa watafiti wa Zanzibar kushiriki katika tafiti za kimataifa, kupata mafunzo ya kisasa na kutumia teknolojia mpya za utafiti, jambo litakalosaidia kuongeza ubora wa tafiti zinazofanyika nchini.
Aliongeza kuwa taasisi yake itaendelea kushirikiana na wadau wengine wa maendeleo ili kuhakikisha tafiti zinazofanyika zinatoa matokeo yanayoweza kutumika moja kwa moja katika kuimarisha huduma za afya na kuongeza ustawi wa wananchi.
Naye mwakilishi kutoka Chuo Kikuu cha Tiba cha Ninging cha nchini China Profesa Su Chuan amesema watashirikiana na sekta ya Afya kuona mafanikio kati yao yanaenda kuleta mafanikio makubwa katika masuala utafiti na mambo mengine.
Amefahamisha kuwa , ushirikiano huo utasaidia kujenga kizazi cha watafiti wenye uwezo mkubwa wa kukabiliana na changamoto za afya zinazojitokeza katika jamii, huku akieleza kuwa uzoefu wa pande zote mbili utakuwa chachu ya kupata matokeo bora zaidi.
Makubaliano hayo yanatarajiwa kuimarisha uwezo wa Zanzibar katika kufanya tafiti za afya zenye viwango vya kimataifa, kuimarisha huduma za afya kupitia tafiti hizo pamoja na kuongeza ushirikiano wa kitaaluma kati ya Zanzibar na China.
Mwisho
0 Comments