6/recent/ticker-posts

Mhe. Hemed Suleiman Abdulla amesema atahakikisha anatimiza ahadi zake zote alizoziahidi wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025

Mwakilishi wa Jimbo la Kiwani ambae pia ni Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla amesema atahakikisha anatimiza ahadi zake zote alizoziahidi wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025 ikiwemo kuimarisha mazingira ya madrasa zilizomo katika Jimbo la Kiwani.

Ameyasema hayo katika ziara yake ya kukagua miradi ya maendeleo inayojengwa katika Wadi ya Mwambe Jimbo la Kiwani Mkoa wa kusini Pemba.

Akifungua  madarasatu NURUL-HIDAYA na madarasat NURU IMANIYA zilizomo katika Wadi ya Mwambe amesema  lengo la kujengwa na kufanyiwa ukarabati kwa madrasa hizo ni kuboresha mazingira ya kusomea na kufundishia kitabu kitukufu cha Qur'an na kuhakisha wananfunzi wanasoma katika mazingira bora na salama yatakayo wawezesha kukihifadhi kwa uweledi kitabu kitukufu cha Qur-an.

Mhe. Hemed amefahamisha kuwa mtoto anapopatiwa elimu ya Qur-an mapema humjenga  kimaadili na kuwa na hofu ya Mwenyezi Mungu jambo litakalosaidia kupata viongozi wenye uzalendo na utayari wa kuitumikia nchi yao.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amewakumbusha wazazi na walezi kuimarisha  ushirikiano na kuweka kando tofauti zao walizonazo ili kuweza kulitekeleza vyema jukumu kubwa la kuwalea watoto katika malezi bora yenye kumpendeza Mwenyezi Mungu.

Mhe. Hemed amewataka wananchi kila mmoja kwa nafasi yake kuhakikisha wanatoa ushirikiano kwa wakandarasi wanaojenga miundombinu mbali mbali Jimboni humo pamoja na kuwaasa vijana kutojiingiza katika vitendo viovu ikiwemo utumiaji wa madawa ya kulevya na wizi, na badala yake washirikiane katika harakati za kuileta Kiwani Maendeleo.

Sambamba na hayo mwakilishi huyo  amewatoa hofu wananchi wa Wadi ya Mwambe kwa kuwaeleza kuwa Viongozi wa Jimbo wanaendelea na mchakato wa  kuhakikisha huduma ya maji safi na salama inapatikana kwa uhakika katika vijiji vyote vilivyomo ndani ya Wadi hio na Jimbo la Kiwani kwa ujumla.

Akiwasilisha taarifa ya kitaalamu juu ya ujenzi wa madrasa hizo Mjumbe wa Kamati ya siasa ya Jimbo la Kiwani Dkt. Massoud Suleima Abdulla amesema fedha zilizotumika katika ujenzi wa madrasa hizo ni zaidi ya shilingi za Kitanzania Milioni 70 zilizojumuisha ujenzi wa vyumba viwili vya kusomea kwa kila madrasa, matundu ya vyoo manne na ofisi ya mwalimu Mkuu pamoja na kuweka vitendea kazi vyote muhimu kwa ajili ya kusomea na kufundishia.

Dkt. Massoud ameeleza kuwa kukamilika kwa madrasa hizo zinatoa fursa kwa wanafuzi kusoma katika mazingira bora na salama ambapo kila madrasa ina uwezo wa kuwahudumia zaidi ya wanafunzi  200 kwa wakati mmoja.

Kwa upande wao Mwalimu  wa Madrasat hizo wamemshukuru Mwakilishi wa Jimbola Kiwani pamoja na uongozi nzima wa jimbo hilo kwa kuwajengea madrasa hizo ambazo zimeondoa changamoto zilizokuwepo ndani ya maeneo yao.

Walimu hao wamewaomba wazazi na walezi kufanya juhudi katika kuwasimamia  watoto wao ili kuweza  kuisoma vyema Qur-an itakayowajenga kimaadiili na kiroho.

Nae Afisa Mdhamini Wizara ya Maji, Nishati na Maadini Mhandisi SULEIMAN HAMAD OMAR amesema Wizara itahakikisha ndani ya kipindi kifupi kijacho huduma ya maji safi na salama inapatikana bila ya usumbufu ndani ya Wadi ya Mwambe hususan katika Kisiwa cha Shamiani Muambe ili wananchi waondokanae na kadhia ya kufuata huduma hio masafa ya mbali.

Mhandisi Hamad amewaomba wananchi wa Mwambe na Vitongoji vyake kutoa mashirikiano wakati wa ufikishaji wa miundombinu ya maji ili kuwawezesha wataalamu wa ZAWA kufanya kazi zao kwa ufanisi Mkubwa.

Akikagua ujenzi wa Mnara wa kuwekea Matenki ya maji pamoja na kukabidhi matenki manne yenye uwezo wa kuhifadhi maji lita elf 5 kwa kila moja yanayotarijiwa  kuhudumia vijiji vinne vilivyomo katika shehia ya Jombwe, Mhe. Hemed amesema ujenzi huo umegharimu zaidi ya shilingi Milioni 60 wenye lengo la  kuhakikisha changamoto ya maji inamalizika na wananchi wanapata maji safi na salama  kwa masaa 24.

Amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeridhia kujengwa Skuli ya Ghorofa ya G+4 katika kijiji cha Umbaju ambayo itapunguza changamoto ya uhaba wa madarasa lakini pia kuongeezeka kwa kiwango cha ufaulu Jimboni humo.

Makamu wa Pili wa Rais ameeleza kuwa ujenzi wa miundombinu ya barabara inaendelea kila kona katika Jimbo la Kiwani huku Serikali ikiwa imeshawalipa fidia wananchi wote waliopisha ujenzi wa miundombinu hio.

Katika ziara yake hio Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amefungua na kukabidhi madrasa mbili za Qur-an, kukagua ujenzi wa Tawi la CCM Shamiani Mwambe, kukagua ujenzi wa Mnara wa Kuwekea Matenki ya Maji Jombwe, kukagua ujenzi wa barabara ya Mawasiliano-Chanjaani hadi Jombwe yenye urefu wa Kilomita 1.7 pamoja na kuzungumza na wanafunzi wa kidato cha nne wanaosoma katika Skuli ya Sekondari Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Imetolewa na kitengo cha habari ( OMPR )

tarehe  01 / 08 / 2026


Post a Comment

0 Comments