Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla akimkabidhi Keptein wa timu ya Mashabiki wa Yanga Mukrim Jamal Ramadhan mara baada ya kuibuka mabingwa wa mchezo wa fainali wa mpira wa miguu iliyozikutanisha timu za mashabiki wa Yanga na wa Simba, mchezo uliyofanyika katika uwanja wa mpira Kitogani Mka wa Kusini Unguja.Timu ya Mashabiki wa Yanga wameshinda mchezo huo kwa bao 2-0.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe.Hemed Suleiman Abdulla amesema Tamasha la Kizimkazi (Kizimkazi Festival) linaendelea kuwaunganisha na kuwaweka pamoja wananchi kutoka maeneo mbalimbali ya Tanzania kutokana na shughuli za maendeleo zinazofanyika kupitia Tamasha hilo.
Ameyasema hayo katika mchezo wa Fainali uliowakitanisha mashabiki wa Timu ya Yanga na mashabiki wa timu ya Simba wa mkoa wa kusini uliochezwa katika uwanja wa Mpira wa miguu Kitogani Mkoa wa Kusini Unguja.
Katika fainali hio, Mhe. Hemed amewataka wanamichezo kucheza mpira kwa nidhamu na kufuata kanuni na sheria za soka huku wakitambua kuwa kupitia michezo fursa mbalimbali zinapatikana ikiwemo ajira.
Mhe. Hemed amewaasa wanamichezo hao kujiepusha na makundi maovu ikiwemo matumizi ya madawa ya kulevya na kutoshiriki katika matukio mabaya yanayoweza kutaharisha amani ya nchi.
Mhe. Hemed amewapongeza viongozi wakuu wa nchi Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan na Rais wa Zanzibar Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi kwa kuiongoza nchi kwa mafanikio makubwa, Amani na usalama huku miradi mikubwa ya maendeleo ikiendelea kutekelezwa nchini.
Mhe hemed amesema amelipokea Ombi la Mbunge wa Paje Mhe. Jaffar Ismail Sanya la kuangaliwa tena bei za viingilio katika viwanja vya Wilaya na kusema kuwa Serikali itaangalia namna ya kulifanyia kazi ili vijana waweze kufaidika na viwanja hivyo.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Kusini Ndugu Othman Ali Maulid amewapongeza viongozi wakuu wa nchi kwa kuimarisha Amani na Mshikamano na akuifanya Tanzanian kuendelea kuwa salama.
Maulid amewashajihisha wananchi wa Zanzibar na Tanzania kwa ujumla kujitokeza kwa wingi kushiriki katika kilele cha Tamasha la Kizimkazi ili kuendelea kuunga mkono juhudi zinazochukuliwa na viongozi za kuwaletea maendeleo wananchi wa Pande mbili za Muungano.
Mbunge wa Jimbo la Paje Mhe. Jaffar Ismail Sanya amesema lengo la kujengwa kwa viwanja vya michezo vya Wilaya na Mikoa ni kuimarisha michezo na kukuza vipaji vya vijana hivyo ameiomba Serikali kuangalia uwezekano wa kupunguzwa viingilio katika viwanja hivyo na fursa za kuweza kuvitumia viwanja hivyo.
Mhe. Sanya amezipongeza timu zilizoshiriki katika Fainali ya Tamasha la Kizimkazi kwa kucheza kwa nidhamu na kufuata kanuni na sheria zinazoongoza mpira wa miguu.


Imetolewa na kitengo cha habari ( OMPR )
tarehe… 12 / 08 / 2026







0 Comments