Na.Mwandishi Wizara ya Afya Zanzibar.
MKURUGENZI Mkuu wa Wizara ya Afya Zanzibar, Dkt Mariyam Seif Hemed, amesema uandaji wa Mfumo wa Urejeshaji na Usafirishaji wa Sampuli za Maabara ni hatua muhimu katika kuimarisha mfumo wa ukusanyaji, uhifadhi na usafirishaji wa sampuli kutoka vituo vya afya vya Unguja na Pemba.
Hayo ameyaeleza wakati akizungumza katika warsha ya uandaji wa Taratibu za Uendeshaji wa Kawaida (SOPs) za Mfumo wa Urejeshaji na Usafirishaji wa Sampuli za Maabara, ambapo amesema maabara zina nafasi muhimu katika utoaji wa huduma za afya, kwa kuwa majibu sahihi ya vipimo huwawezesha wataalamu wa afya kufanya maamuzi sahihi kuhusu matibabu ya wagonjwa na udhibiti wa magonjwa.
Amesema dunia inakabiliwa na kuibuka kwa magonjwa mapya pamoja na kurejea kwa baadhi ya magonjwa yaliyowahi kudhibitiwa, ni muhimu Zanzibar kuwa na mfumo madhubuti wa uchunguzi na ufuatiliaji wa magonjwa.
Amefahamisha kuwa uwezo wa kugundua ugonjwa mapema na kuthibitisha uwepo wake kwa wakati unasaidia kuchukua hatua za haraka za matibabu na kuzuia kuenea kwa magonjwa katika jamii.
Dkt, Mariyam ameipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya Afya kwa hatua mbalimbali zinazochukuliwa katika kuimarisha huduma za maabara na kuongeza uwezo wa uchunguzi wa magonjwa.
Amesema Zanzibar imeendelea kuwa na mtandao wa vituo vinavyotoa huduma za maabara katika Unguja na Pemba, huku mifumo ya usafirishaji wa sampuli ikitumika katika programu mbalimbali za afya, ikiwemo TB, HIV, malaria na chanjo.
Amesema mwaka 2025, Wizara ya Afya ilikamilisha Mwongozo wa Uendeshaji wa Mfumo Jumuishi wa Urejeshaji na Usafirishaji wa Sampuli za Maabara Zanzibar, ambao umeweka msingi wa namna sampuli zinavyopaswa kukusanywa, kufungashwa, kuhifadhiwa na kusafirishwa.
Amewataka washiriki wa warsha hiyo kutumia uzoefu na utaalamu wao kuhakikisha mwongozo unaoandaliwa unakuwa rahisi kueleweka, unaendana na mazingira ya Zanzibar na unaweza kutekelezwa katika vituo vya afya vya Unguja na Pemba.
Kwa upande wake, Mratibu Mwandamizi Pandemic Fund kutoka Shirika la Jhpiego, Asha Ussi, amesema kutokana na mwingiliano mkubwa wa watu duniani, magonjwa yanaweza kuvuka mipaka kwa urahisi, hivyo nchi zinapaswa kuwa tayari katika kuyagundua mapema na kuchukua hatua za kukabiliana nayo kabla hayajasambaa na kuleta madhara kwa jamii.
Amesema ni muhimu kuwa na mifumo madhubuti pamoja na utaratibu unaoeleweka wa kuchukua sampuli, kuzisafirisha na kuzifanyia uchunguzi kwa wakati, ili kuwezesha hatua stahiki kuchukuliwa mapema na kusaidia kudhibiti magonjwa nchini.
Naye Mkuu wa Divisheni ya Huduma za Uchunguzi wa Wizara ya Afya, Abdalla Said Mohd, amesema wamejipanga kuhakikisha sampuli zinazopatikana katika vituo vya afya zinasafirishwa na kuchunguzwa kwa wakati.
Amesema Wizara inaendelea kushirikiana na mashirika mbalimbali, yakiwemo CIHEB na Shirika la Posta Tanzania, katika kuhakikisha sampuli zinafikishwa katika maeneo husika kwa wakati na kufanyiwa uchunguzi ili majibu yake yapatikane kwa haraka.
Amesema warsha hiyo ni muhimu kwa kuwa itasaidia kuimarisha huduma za uchunguzi na afya nchini, huku ikiwakutanisha wadau kutoka maeneo mbalimbali, wakiwemo wataalamu wa Wizara ya Afya, ZHSF, sekta ya mifugo, wawakilishi kutoka Pemba pamoja na wataalamu wengine.
Ameeleza kuwa ushirikiano wa wadau hao utasaidia kuweka mfumo madhubuti na unaotekelezeka wa urejeshaji na usafirishaji wa sampuli za maabara, jambo litakalosaidia kuongeza ufanisi wa uchunguzi na kuimarisha uwezo wa Zanzibar katika kugundua na kudhibiti magonjwa kwa wakati.
Mwisho.
0 Comments