Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imedhamiria kuziondoa changamoto zote wanazokutana nazo wakulima wa mwani Kisiwani Pemba kwa kujenga Kiwanda kikubwa cha kuchakatia na kusarifia zao la mwani Kisiwani humo.
Ameyasema hayo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla wakati akikagua maendeleo ya ujenzi wa Kiwanda hicho kilichopo Chamanangwe Wilaya ya Wete, Mkoa wa kaskazini Pemba.
Amesema kwa muda mrefu wakulima wa zao la mwani wamekosa soko la uhakika la kuuzia zao hilo na kupelekea wananchi walio wengi hasa akinamama kuachana na biashara hio hivyo kujengwa kwa kiwanda hicho kitakwenda kutatua changamoto hio na kuwawezesha wakulinkulima wa zao hilo kupata soko la uhakika.
Mhe. Hemed ameuagiza Uongozi wa Wizara ya Uchumi wa Buluu na Uvuvi kuhakikisha wanachukua hatua za dharura katika kuhakikisha vifaa vyote vilivyokwama kutokana na changamoto ya usafiri vinafika Kisiwani Pemba ili ujenzi wa Kiwanda cha Mwani uweze kuendelea na kukamilika kwa wakati na kutoa huduma kwa wananchi.
Amesema Wizara ya Uchumi wa Buluu inapaswa kuwa karibu na wakulima wa zao la mwani kusilikiliza changamoto zao na kuangalia namna bora ya kuwasaidia ikiwemo kuwawezesha kwa vitendea kazi na kuwapatia elimu ili waweze kulima kisasa kilimo chenye faida kwao na Taifa kwa ujumla.
Hata hivyo amewakumbusha wananchi wa Mkoa wa Kaskazini Pemba juu ya kuitunza na kuilinda miundombinu mbali mbali inayojengwa katika Mkoa wao sambamba na kuona umuhimu wa kuilinda amani iliyopo nchini kwani ndio msingi mkubwa wa maendeleo.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu Kampuni ya Mwani Zanzibar ZAFCO ndugu Nassor Rashid Mohd amesema kiwanda hicho kipo katika hatua ya ufungaji wa mitambo ya kuzalisha chakula cha mifugo pamoja na uchakataji na kusarifu mwani mbichi ambao utaongeza thamani ya zao hilo kwa wakulima.
Amesema kitakapokamilika kiwanda hicho kinatarajiwa kutoa huduma mbali mbali ikiwemo kuchakata mwani mbichi zaidi ya kilo elf 40 kwa siku, kuzalisha lita elf 22 za mbolea ya virutubisho vya mimea kwa siku na kusarifu unga wa mwani ambao utatumika katika kutengenezea bidhaa mbali mbali za dawa na chakula jambo litakaloongeza soko la zao la mwani.
Nassor amesema Kiwanda cha kuchakatia na kusarifia mwani cha Chamanangwe kinajengwa na Mkandarasi kampuni ya MGR Investment ambapo shilingi za Kitanzania Bilioni 15.9 zimeshatumuka katika ujenzi huo unaotarajiwa kukamilika na kuanza kazi mwishoni mwa mwezi wa Disemba 2026.
Akikagua ujenzi wa matangi ya kuhifadhia maji yanayojengwa Mtambwe Daya, na Mtambwe mpaka njia, Makamu wa Pili wa Rais amesema azma ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ni kuhakikisha wananchi wa Zanzibar wanapata huduma ya maji safi na salama kwa masaa 24 bila ya usumbufu wowote.
Mhe. Hemed amewaagiza viongozi wa Wizara ya Maji, Nishati na Maadini kusimamia kwa karibu miradi hio ili kubaini changamoto zinazojitokeza na kuzichukulia hatua jambo litakalosaidia miradi hio kukamilika kwa wakati uliopangwa na kwa viwango vya hali ya juu.
Wakati huo huo Mhe. Hemed alikagua maendeleo ya ujenzi wa barabara ya Bwagamoyo- Matuunihadi Kele Mwambwe Kaskazini yenye urefu wa Kilomita 6.5 ambapo amewaangiza wakandarasi wanaojenga barabaraha hio kukamilisha ujenzi wa mitaro ya kupitishia maji ya mvua na kuwekwa alama za barabarani ili kurarahisisha matumizi ya barabara hio kwa madereva na watembea kwa miguu.
Amewasihi wananchi wa Mtambwe kuitunza miundombinu inayojengwa katika maeneo yao ili iweze kutumika kwa muda mrefu sambamba na kushirikiana pamoja katika harakati za kimaendeleo.
Hata hivyo Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar ametembelea na kukagua Viwanja vya mpira vinavyojengwa katika kijiji cha Kinyikani na kusema kuwa ujenzi wa viwanja hivyo ni fursa kubwa katika kuibua vipaji vya michezo lakini pia kukifungua Kisiwa cha Pemba kiuchumi kupitia utalii wa Michezo.
Amesema Serikali imejenga viwanja hivyo kwa lengo la kupunguza uhapa wa viwanja vya michezo nchini hivyo ni lazima lengo hilo litimie kwa kukabidhiwa wananchi viwanja hivyo waweze kuvitumia katika kukuza vipaji vyao vya michezo mbali mbali.
Katika ziara yake hio Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alikagua ujenzi wa Skuli ya Msingi Kiuyu, Kiwanda cha Kuchakata na Kusarifu Mwani Chamanangwe, ujenzi wa Kiwanja cha Mpira cha Mkoa wa Kaskazini Pemba kinachojengwa Kinyikani, ujenzi wa Barabara ya Bwagamoyo -Matuuzi hadi Kele Mtambwe.Miradi ya Matangi ya Kuhifadhia Maji Safi na Salama yanayojengwa Mtambwe Kusini na Kaskazini pamoja na barabara ya Kinazini Mtambwe.
Imetolewa na kitengo cha habari ( OMPR )
Leo tarehe…04 / 08 / 2026
0 Comments