Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla akimkabidhi mfano wa hundi ya shilingi milioni Tano (5,000,000)Bi. Msimu Kassim Abdalla mshindi wa Mashindano ya TUSUA INNOVATION yaliyoandaliwa na Global Youth Empowerment Institute, Mfano huo wa hundi amekabidhiwa katika ufunguzi wa kongamano la vijana Ukanda wa Afrika Mashariki kwa mwaka 2026 lililofanyika katika Ukumbi wa Dkt. Ali Mohammed Shein - SUZA TUNGUU Mkoa wa Kusini Unguja.
Serekali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar zinaendelea na mkakati wa kuwekeza katika sekta ya elimu, maendeleo ya ujuzi, TEHAMA, ujasiriamali na mazingira yanayowawezesha vijana kugeuza mawazo yao katika biashara,ubunifu na ajira.
Hayo yamesemwa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla kwa niaba ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi katika hafla ya ufunguzi wa Kongamano la vijana Ukanda wa Afrika Mashariki mwaka 2026, lililofanyika katika Ukumbi wa Dkt. Ali Mohammed Shein - SUZA Tunguu Mkoa wa Kusini Unguja.
Amesema maendeleo ya vijana ni uwekezaji wa kimkakati kwa mustakbali wa Taifa ambapo dhamira ya Serikali ni kuendelea kuimarisha sera, program na mifumo ya kuwawezesha vijana kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya Taifa.
Makamun wa Pili wa Rais amesema Serikali kwa kushirikiana na Benki ya Maendeleo ya Afrika imefanikisha utekelezaji wa miradi iliyogharimu zaidi ya Dola za Kimarekani milioni 54 kwa ajili ya maendeleo ya ujuzi na ajira za vijana katika sekta ya uchumi wa Buluu ambayo inatarajiwa kuwafikia vijana zaidi ya elf 43,000.
Mhe. Hemed amefahamisha kwamba Serikali zinawandaa vijana kuweza kumudu mahitaji ya uchumi wa sasa na baadae kwa kuwajengea msingi utakaowasaidia kushindana katika uchumi wa Kikanda na Kimataifa .
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amesema kupitia ajenda ya uchumi wa Bulu, uwekezaji mkubwa umefanyika katika maendeleo ya ujuzi, ubunifu na biashara zinazotegemea rasilimali bahari hatua iliyowafungulia vijana maelfu ya fursa mpya za ajira, uwekezaji na ujasiriamali.
Sambamba na hayo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar ameeleza kufurahishwa kwake na azma ya vijana ya kuendelea kuijenga East Africa Youth Conference kuwa jukwaa la vijana wa Afrika Mashariki na kuwahakikishia kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kuthamini jitihada zote zinazochangia kusukuma mbele maendeleo ya vijana, ushirikiano wa Kikanda na kubadilishana uzoefu baina ya vijana wa ukanda wa Afrika Mashariki na mataifa mengine.
Aidha, Mhe. Hemed ametoa wito kwa vija kuitumia vyema fursa ya Kongamano hilo kwa kujifunza, kujijengea uwezo na kuwekeza katika maarifa, Teknolojia na kuwa sehemu ya mabadiliko katika kujiajiri na kuzalisha fursa za ajira kwa wengine.
Nae Waziri wa Vijana, Ajira na Uwezeshaji Mhe.Shaban Ali Othman amesema Wizara yake itaendelea kuunga mkono juhudi mbalimbali za kimaendeleo zinazofanywa na Vijana kwa kuwapatia elimu, ujuzi na kuwawezesha katika kufikia malengo yao.
Mhe. Shaban amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeweka msisitizo katika kuzinyanyua Taasisi na Jumuia mbalimbali zinazoshughulika na maendeleo ya vijana ili kuona kwamba ndoto na malengo ya vijana yanatimia kwa uwelidi mkubwa.
Ameyashukuru Mashirika na Taasisi mbalimbali zinazoendelea kufanya kazi na vijana wakiwa na lengo la kuona vijana wananyanyuka katika nyanja mbalimbali ikiwemo biashara, Ubunifu, matumizi ya Tehama na kutanua wigo mpana wa ajira na kujiajiri.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Global Youth Empowerment Bibi Amina Sanga amesema moja ya malengo makuu ta Taasisi hio ni kutengeneza viongozi vijana ambao watapatiwa mafunzo, nyenzo na Teknolojia ili waweze kuekeza katika maeneo ya kimkakati ya maendeleo na kutimiza malengo yao.
Mkurugenzi Sanga amesema Taasisi ya Global Youth Empowerment inazipongeza Serikali zote mbili kwa uwekezaji mkubwa unaofanyika kwa vijana kwa dhamira ya kuona vijana wanapatiwa fursa za maendeleo lakini pia kuandaliwa kuwa viongozi bora wazalendo wa baadae.
Amewasisitiza vijana kuzitumia na kuziendea fursa mbalimbali zinazotolewa na Serikali, Mashirika, Taasisi na jumuia za Vijana ili kukuza vipaji vyao na kufikia matarajiao yao ya malengo waliojiwekea.
Meneja wa CRDB BANK Kanda ya Pwani Bwana Iddy Badru ambao ni miongoni mwa wafadhili wakuu wa Kongamano la Jukwa la vijana wa Afrika Mashariki, amesema Jukwaa hilo limewaunganisha vijana zaidi ya elf 3 ambalo litatoa muelekeo kwa vijana katika kuzifikia fursa za uwekezaji, ajira, teknolojia na ushauri wa Biashara ili kuweza kutimiza malengo yao na Nchi zao.
Amesema CRD BANK imekuwa ikitoa mafunzo mbalimbali kwa vijana na wanawake juu ya matumizi ya fedha, ushauri wa biadhara na mikopo ambavyo vimewasaidia kubadilisha mawazo yao, biashara zao pamoja na kukuwa na kuimarika uchumi na kipato cha mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla.
Ndugu Iddy amefahamisha kuwa kupitia programu mbali mbali zilizobuniwa na CRDB BANK, vijana na wanawake wamenufaika na mafunzo, elimu, na mikopo ambapo zaidi ya Shilingu Bilioni 15 zimetumika katika kuwasaidi vijana kutimiza malengo yao.
Wakichangia maada mbalimbali zilizojadiliwa katika Kongamano hilo, Bibi Ruth Mueni Kutoka Kenya amesema vijana katika kutimiza malengo yao ni lazima kujitambua, kutengeneza mahusiano mazuri na watu pamoja na kuwa tayari kujifunza na kuyafanyia kazi kwa vitendo yale wanayojifunza.
Ruth amewaomba viongozi wakuu wa nchi wanachama wa Global Youth Empowerment Institute kuondolewa vikwazo ambavyo vinawadumaza vijana kufikia malengo yao, kuwawezesha vijana kupata mitaji na masoko ya uhakika sambamba na viongozi kuwa na utayari wa kuwashika vijana katika fursa mbalimbali zinazotekea ndani na nje ya nchi zao.
Imetolewa na Kitengo cha Habari ( OMPR )
Leo tarehe 15 / 08 / 2026

0 Comments