Na Khadija Khamis ,WHSUM
Serikali imeeleza kuwa itaendelea kutoa elimu ya tahadhari za mapema kwa jamii katika maeneo mbalimbali hatarishi, ili kukabiliana na majanga katika kipindi cha mvua kubwa zinazoendelea kunyesha hatua hii itasaidia .kushajihisha kujikinga pamoja na kukabiliana na adhari hizo
Kauli hiyo ilitolewa na Mkurugenzi wa Utawala, Mipango na Rasilimali Watu kutoka Kamisheni ya Kukabiliana na Maafa Zanzibar, Haji Ame Haji, wakati akifungua mafunzo kwa wajumbe wa masheha kutoka shehia za Kwamtumwajeni na Nyerere huko Shehia ya Mtumwajeni.
Alisema wajumbe hao wanapaswa kuwa mabalozi wazuri katika maeneo yao kwa kuhakikisha jamii inaweka mazingira safi na kutumia vyoo kwa usahihi.
Aidha, alitoa tahadhari kwa wazazi na walezi kuhakikisha wanawalinda watoto wao dhidi ya hatari zinazotokana na mashimo na mitaro inayojaa maji, ili kupunguza athari za majanga.
Naye Afisa Afya wa Wilaya ya Mjini, Nasriya Mohammed, aliwataka wazazi na walezi kuwasimamia vyema watoto wao, hususan kuepuka vyakula vinavyouzwa bila kuzingatia usafi ambavyo vinaweza kuhatarisha afya zao.
Alieleza kuwa jamii inapaswa kubadilisha tabia kwa kuweka utaratibu wa kutibu maji au kuchemsha maji ya kunywa, pamoja na kujiepusha na utupaji holela wa taka taka ikiwemo mapempas .
Alibainisha kuwa kuna baadhi ya wafanyabiashara huuza vyakula kama pweza, ngisi na samaki wa kukaanga bila kufunika, jambo linaloweza kusababisha athari kubwa kiafya.
Kwa upande wake, Sheha wa Shehia ya Kwamtumwajeni, Rajab Ally Ndauchwa, aliipongeza kamisheni ya maafa kwa hatua ya kupita kila shehia kutoa elimu ambapo aliwataka wajumbe na wananchi kwa ujumla kuchukua tahadhari katika masuala ya afya na usafi wa mazingira, na kuwa mabalozi wa kueneza elimu hiyo kwa wengine.
Aliongeza kuwa ni muhimu kwa mamlaka husika, ikiwemo manispaa, kusimamia sheria za usafi wa mazingira pamoja na kuweka maeneo maalum ya kutupa taka ili kudhibiti uchafuzi wa mazingira.
Aidha, aliwahimiza wananchi kuwa tayari kubadilika na kufuata maelekezo ya wataalamu wa afya ili kujikinga na magonjwa ya mlipuko.

0 Comments