6/recent/ticker-posts

SMZ Kupitia Wizara ya Afya Zanzibar Inaendela Kufanya Juhudi za Kuimarisha Huduma za Uzazi wa Mpango Nchini

Na.Mwandishi Wizara ya Afya Zanzbar.

SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya Afya inaendela kufanya   juhudi za kuimarisha huduma za uzazi wa mpango nchini, huku ikisisitiza kuwa huduma hizo ni nyenzo muhimu katika kupunguza vifo vya akina mama na watoto vinavyotokana na uzazi, pamoja na kuchochea maendeleo ya familia na taifa kwa ujumla.

Kauli hiyo imetolewa katika mkutano wa wadau wa sekta ya Afya ulioandaliwa na Wizara ya Afya kupitia Kitengo Shirikishi cha Afya ya Mama na Mtoto kwa kushirikiana na Asasi ya Kiraia ya TIMEPID, ambapo washiriki walijadili hali ya huduma za uzazi wa mpango Zanzibar, changamoto zilizopo na mikakati ya kuimarisha upatikanaji wa huduma hizo katika ngazi zote za utoaji huduma za afya.

Akizungumza katika mkutano huo, Mkurugenzi wa Mipango, Sera na Utafiti wa Wizara ya Afya Zanzibar Abdullatif Khatib Haji amesema huduma za uzazi wa mpango zimeendelea kuwa sehemu muhimu ya mfumo wa afya kutokana na mchango wake mkubwa katika kupunguza vifo vinavyotokana na uzazi.

Amesema matumizi sahihi ya huduma za uzazi wa mpango husaidia familia kupanga idadi ya watoto wanaowahitaji, kuweka nafasi salama kati ya mtoto mmoja na mwingine pamoja na kulinda afya ya mama na mtoto.

Aidha, amesema licha ya mafanikio yaliyopatikana, bado zipo changamoto zinazokwamisha upatikanaji wa huduma hizo kwa baadhi ya wananchi, ikiwemo uelewa mdogo wa jamii, mitazamo hasi kuhusu baadhi ya njia za uzazi wa mpango pamoja na changamoto za upatikanaji wa huduma katika maeneo mengine.

Kutokana na hali hiyo, amesema Wizara ya Afya imeendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo, wakiwemo UNFPA na mashirika mengine ya kimataifa, ili kuhakikisha huduma za uzazi wa mpango zinapatikana katika hospitali zote za wilaya, hospitali za mikoa na vituo vya afya nchini.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Asasi ya Kiraia ya TIMEPID, Cuthbert Maendaenda, amesema taasisi hiyo imeamua kushirikiana na Serikali katika kuhamasisha uwekezaji wa ndani kwenye huduma za uzazi wa mpango ili kuhakikisha huduma hizo zinakuwa endelevu hata pale ambapo misaada kutoka kwa wafadhili wa nje inapopungua.

Amesema TIMEPID imeandaa mkutano maalumu wa kuwajengea uwezo wajumbe wa Baraza la Wawakilishi kutoka Kamati ya Ustawi wa Jamii pamoja na Kamati ya Fedha ili kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa kutenga rasilimali za ndani kwa ajili ya huduma za uzazi wa mpango.

Amefahamisha kuwa  uwekezaji katika huduma za uzazi wa mpango ni uwekezaji wenye matokeo makubwa kwa jamii, kwani husaidia kuboresha afya ya mama na mtoto, kupunguza gharama za huduma za afya na kuwezesha familia kupanga maisha yao kwa ufanisi zaidi.

Naye Mratibu wa Huduma za Uzazi wa Mpango wa Unguja kutoka Kitengo Shirikishi cha Afya ya Mama na Mtoto, Radhia Mzee Mataka, amesema  hali halisi ya utoaji wa huduma hizo hapa  Zanzibar na kueleza hatua mbalimbali zinazoendelea kuchukuliwa ili kuongeza matumizi ya huduma za uzazi wa mpango miongoni mwa wananchi.

Amesema pamoja na mafanikio yaliyopo, bado kuna haja ya kuendelea kutoa elimu kwa jamii ili kuondoa dhana potofu zinazowafanya baadhi ya wananchi kuogopa au kutotumia njia za uzazi wa mpango.

Amefafanua kuwa elimu kwa jamii, itaendelea kutolewa kupitia vituo vya afya, mikutano ya kijamii na kampeni mbalimbali za uhamasishaji ili kuhakikisha wananchi wengi zaidi wanapata taarifa sahihi kuhusu huduma za uzazi wa mpango.

Wadau hao wameeleza kuwa kuimarishwa kwa huduma za uzazi wa mpango kutachangia kupunguza vifo vya akina mama na watoto, kuimarishwa ustawi wa familia na kuharakisha maendeleo ya kijamii na kiuchumi Zanzibar, huku wakisisitiza umuhimu wa kuongeza uwekezaji wa ndani ili kuhakikisha huduma hizo zinaendelea kuwa endelevu kwa vizazi vya sasa na vijavyo.

Mwisho.

Post a Comment

0 Comments