Na.Mwandishi Wizara ya Afya Zanzibar.
Wizara ya Afya Zanzibar, imepokea msaada wa vishikwambi 22 kutoka Shirika la JHPIEGO ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha huduma za uchunguzi, matibabu na uhifadhi wa taarifa za wagonjwa wa saratani, hususan saratani ya matiti na mlango wa kizazi.
Vishikwambi hivyo vinatarajiwa kutumika kwa wafanyakazi wa afya katika kukusanya na kuingiza taarifa za wagonjwa wanaofikiwa na huduma za saratani kuanzia katika ngazi ya jamii na vituo vya afya vya msingi hadi hospitali za wilaya na za mkoa.
Akizungumza mara baada ya kupokea msaada huo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Zanzibar Dkt Mngereza Mzee Miraji amesema vifaa hivyo vitakuwa na mchango mkubwa katika kuhakikisha taarifa za wagonjwa wa saratani zinakusanywa na kuhifadhiwa kwa usahihi, hatua ambayo itaiwezesha Serikali kuwa na takwimu sahihi na zinazoweza kutumika katika kupanga na kuimarisha huduma za afya.
Amesema vishikwambi hivyo vitaunganishwa na mfumo wa Zan AMR, ambao utasaidia kuhakikisha taarifa za wagonjwa zinawasilishwa na kuhifadhiwa katika mfumo mmoja, kuanzia wanapofikiwa katika ngazi ya huduma za afya ya msingi hadi wanapofika katika hospitali zinazotoa huduma za juu zaidi.
Dkt Mngereza amefahamisha kuwa matumizi ya mfumo huo ni hatua muhimu katika kuimarisha uhakika wa taarifa, kwa kuwa takwimu sahihi za wagonjwa ni msingi wa kufanya maamuzi katika sekta ya afya, ikiwemo kupanga mahitaji ya dawa, vifaa tiba, wataalamu na huduma nyingine zinazohitajika katika kukabiliana na saratani.
Amesema Serikali ya Awamu ya Nane, katika kipindi cha mwaka mmoja, imeongeza juhudi katika kukabiliana na changamoto ya saratani Zanzibar kwa kuweka mkazo katika maeneo mbalimbali, ikiwemo ujenzi wa Hospitali Maalumu ya Saratani Binguni.
Ameeleza kuwa ujenzi wa hospitali hiyo unaendelea na unatarajiwa kukamilika ndani ya miezi 18, ambapo baada ya kukamilika itakuwa na vifaa maalumu vya uchunguzi wa aina mbalimbali za saratani pamoja na huduma za matibabu.
Hatua hiyo, amesema, inalenga kupunguza changamoto ambazo wananchi wamekuwa wakikabiliana nazo katika kupata huduma za uchunguzi na matibabu ya saratani, pamoja na kuweka mazingira bora ya utoaji wa huduma hizo ndani ya Zanzibar.
Mbali na ujenzi wa hospitali hiyo, Serikali imeendelea kushirikiana na wadau mbalimbali katika kupambana na saratani, ikiwemo JHPIEGO, ambayo imekuwa ikitekeleza programu za uchunguzi wa saratani ya matiti na mlango wa kizazi katika maeneo mbalimbali ya Zanzibar.
Aidha, amesema vifaa na mashine maalumu za uchunguzi zimeendelea kugawanywa katika vituo vya afya ili kuongeza uwezo wa watumishi kuwafikia wananchi na kufanya uchunguzi wa saratani kwa wakati.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mradi wa BEAT Breast Cancer kutoka JHPIEGO, Dkt Mary Rose Giattas, amesema Shirika hilo limeamua kukabidhi vishikwambi hivyo ili kusaidia utekelezaji wa programu ya saratani ya matiti na mlango wa kizazi Zanzibar, hususan katika ukusanyaji wa taarifa sahihi za wagonjwa na wateja wanaofikiwa na huduma hizo.
Amesema vifaa hivyo vitatumika katika hatua mbalimbali za utoaji wa huduma, kuanzia katika jamii hadi kwenye hospitali zinazotoa huduma za uchunguzi na matibabu ya saratani.
Aidha amesema upatikanaji wa taarifa sahihi ni muhimu katika kufuatilia wagonjwa, kujua idadi ya watu wanaofikiwa na huduma, kutambua mahitaji yaliyopo pamoja na kusaidia wataalamu na Serikali kufanya maamuzi sahihi kuhusu namna ya kuimarisha huduma za saratani.
Ameeleza kuwa JHPIEGO inatarajia kuwa baada ya kuwawezesha watumishi wa afya watakaotumia vishikwambi hivyo kupitia mafunzo, wataweza kutumia mfumo huo kwa ufanisi na kuingiza taarifa kwa wakati na kwa usahihi.
Amesema hatua hiyo itasaidia kuimarisha mfumo wa ukusanyaji wa taarifa za wagonjwa na kuhakikisha taarifa zinazopatikana katika ngazi mbalimbali za huduma za afya zinafika kwenye mfumo na kutumika katika kuimarisha huduma.
Hatua hiyo pia inaonesha umuhimu wa ushirikiano kati ya Serikali na washirika wa maendeleo katika kuimarisha mapambano dhidi ya saratani, kwa lengo la kuhakikisha wananchi wanapata huduma za uchunguzi na matibabu kwa wakati, huku teknolojia ikitumika kama nyenzo muhimu katika kuboresha utoaji wa huduma hizo.
Saratani ya matiti na saratani ya mlango wa kizazi ni miongoni mwa changamoto zinazohitaji uchunguzi wa mapema na ufuatiliaji wa karibu sambamba na kuimarisha huduma katika ngazi ya jamii na vituo vya afya, pamoja na kuwa na mfumo mzuri wa taarifa, kunaweza kusaidia kuwabaini wagonjwa mapema na kuhakikisha wanafanyiwa ufuatiliaji na kupata huduma zinazohitajika
Mwisho.
0 Comments