6/recent/ticker-posts

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe.Hemred Suleiman Ameridhishwa na Hatua Kubwa Iliyofikiwa ya Ujenzi wa Uwanja wa AFCON Fumba Zanzibar

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe.Hemed Suleiman Abdulla akikagua ujenzi wa Uwanja wa Kisasa wa Afcon Fumba Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja, Wilaya ya Magharibi "B " akipata maelezo kutoka kwa msimamizi wa ujenzi wa Kampuni ya ORKUN Ahmet Ugur Isler, wakati wa ziara yake kuangalia maendeleo ya ujenzi huo  

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla amesema ameridhishwa na hatua kubwa iliyofikiwa ya ujenzi wa Uwanja wa AFCON Fumba unaodhihirisha utayari wa Zanzibar kushiriki katika Mashindano ya Afcon 2027.

Ameyasema hayo alipofanya ziara ya kukagua maedeleo ya ujenzi wa mradi wa Uwanja wa Mpira wa AFCON Fumba unaojengwa katika Kijiji cha Fumba Wilaya ya Magharibi "B" Unguja.

Amewatoa hofu Watanzani kuwa Ujenzi wa Uwanja wa AFCON Fumba  utakamilika kwa wakati uliopangwa ukiwa na mahitaji yote yanayohitajika kuwemo katika Viwanja vya Kimataifa na  kutumika katika Mashidano ya Afcon yanayotarajiwa kufanyika mwezi Juni 2027.

Mhe. Hemed amemshukuru Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi kwa maono yake makubwa yaliyolenga katika ujenzi wa miradi ya kimkakati ambayo itaifungua Zanzibar kiuchumi na kupiga hatua kumbwa zaidi kimaendeleo.

Makamu wa Pili wa Rais amesema miundombinu yote muhimu kama vile umeme, maji na barabara itapatikana katika uwanja huo na kuwahakikishaia wananchi wa Zanzibari kuwa Serikali kupitia Shirika la Umeme Zanzibar (ZECO ) inajipanga ifikapo mwaka 2030 Zanzibar iweze kujitosheleza yenyewe kwa Nishati ya umeme.

Mhe. Hemed amempongeza  Mkandarasi wa ujenzi wa Uwanja wa AFCON Fumba Kampuni ya ORKUN group of Zanzibar na Mshauri elekezi Al-Khatmy Consultancy kwa  kazi kubwa na nzuri wanayoendelea kuifanya ambapo amewataka kuendelea kufanya kazi mchana na usiku ili kuhakikisha uwanja huo unakamilika kwa wakati ili uweze kutumika kwa kusidio lililopangwa .

Sambamba na hayo Mhe. Hemed amesema utakapokamilika ujenzi wa Uwanja wa AFCON, Zanzibar  itanufaika na fursa mbalimbali kiuchumi na kijamii kama vile kuongezeka kwa watalii wanaoingia nchini, kuimarika kwa biashara, kuendelela kwa ujenzi wa miundombinu  mbalimbali pamoja na Zanzibar kutangazika zaidi Kimataifa.

Aidha, Mhe. Hemed amewashauri wafanyakazi wa Kampuni ya ORKUN group of Zanzibar ikijitokeza changamoto yoyote ile kati yao na muajiri wao kupeleka malalamiko yao katika Taasisi husika ili hatua ziweze kuchukuliwa kwa mujibu wa sheria na miongozo ya ajira na kuacha kulalamika pembeni jambo ambalo haliwezi kuleta mustakabali mzuri wa utatuzi wa changamoto zao.

Kwa upande wake Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo Mhe. Dkt. Riziki Pembe Juma amesema ziara za Mkamu wa Pili wa Rais za kukagua ujenzi wa miradi mbalimbali ya maendeleo inayojengwa Unguja na Pemba inatoa msukumo kwa viongozi kuweza kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi na kusimamia ujenzi wa miradi hio ili iweze kukamilika kwa wakati na kwa viwango vilivyopangwa.

Dkt. Riziki amewataka wananchi kuzitumia kikamilifu fursa zitakazopatikana  katika Mashindano ya Afcon 2027 lakini pia kutangaza mila na utamaduni wa Zanzibar kwa wageni watakaoingia nchini.

Mhandisi kutoka Kampuni ya ORKUN group of Zanzibar ndugu, Mohammed Noor amemueleza Makamu wa Pili wa Rais kuwa ujenzi wa uwanja wa AFCON Fumba umefika asilimia 81 ambao utagharimu zaidi ya Shilingi Bilioni 390 na hadi kukamilika mwezi Disemba mwaka huu unatarajiwa kuhudumia wanamichezo elfu 36,500 kwa wakati mmoja.

Mhandisi Noor amesema kwa hatua ya kwanza ujenzi huo utajumuisha uwanja wa Kimataifa wa michezo, viwanja viwili kwa ajili ya kufanyia mazoezi, vyoo, vyumba vya mapumziko, Bwawa la kuogelea na Ofisi.

Imetolewa na Kitemgo cha Habari ( OMPR )

Leo tarehe  17 / 08 / 2026

...........................................................................

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe.Hemed Suleiman Abdulla akiambatana na viongozi mbalimbali katika ziara ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa Uwanja wa AFCON Fumba,  Wilaya ya Magharibi "B" Unguja

Post a Comment

0 Comments