6/recent/ticker-posts

Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ampokea Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) Mhe. Félix Antoine Tshisekedi Tshilombo, Ikulu Ndogo Tunguu Zanziba

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) Mhe. Félix Antoine Tshisekedi Tshilombo baada ya kuwasili Ikulu Ndogo ya Zanzibar, tarehe 18 Agosti, 2026.
 Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) Mhe. Félix Antoine Tshisekedi Tshilombo akisaini Kitabu cha Wageni baada ya kuwasili Ikulu Ndogo ya Zanzibar, tarehe 18 Agosti, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) Mhe. Félix Antoine Tshisekedi Tshilombo baada ya kuwasili Ikulu Ndogo ya Zanzibar, tarehe 18 Agosti, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) Mhe. Félix Antoine Tshisekedi Tshilombo katika Ikulu Ndogo ya Zanzibar, tarehe 18 Agosti, 2026.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Waandishi wa Habari kufuatia Ziara ya Kikazi ya Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) Mhe. Félix Antoine Tshisekedi Tshilombo katika Ikulu Ndogo ya Zanzibar, tarehe 18 Agosti, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) Mhe. Félix Antoine Tshisekedi Tshilombo akizungumza na Waandishi wa Habari katika Ikulu Ndogo ya Zanzibar, tarehe 18 Agosti, 2026. 

TANZANIA, DRC KUONGEZA KASI YA MIRADI YA UCHUKUZI NA BIASHARA
Tanzania na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) zimekubaliana kuongeza kasi ya utekelezaji wa miradi ya uchukuzi inayounganisha nchi hizo ili kupunguza muda na
gharama za usafirishaji wa mizigo, pamoja na kupanua biashara na uwekezaji kwa manufaa ya pande zote mbili.

Makubaliano hayo yamefikiwa leo, tarehe 18 Agosti 2026, Ikulu Ndogo, Zanzibar, wakati wa mazungumzo kati ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, na Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Mheshimiwa Félix Tshisekedi, aliyefika nchini kwa mwaliko wa Rais Dkt. Samia.

Katika mazungumzo hayo, Rais Dkt. Samia amesisitiza umuhimu wa kuimarisha mtandao wa reli, barabara, huduma za bandari na usafiri wa majini unaounganisha Bandari ya Dar
es Salaam na maeneo ya uzalishaji nchini DRC kupitia Ziwa Tanganyika.

“Lengo letu ni kuhakikisha tunarahisisha usafirishaji wa mizigo kati ya Tanzania na DRC kwa kuimarisha miundombinu na huduma za uchukuzi, ili kupunguza muda na gharama na hivyo kuongeza biashara na uwekezaji kati ya nchi zetu,” amesema Rais Dkt. Samia.

DRC ni miongoni mwa watumiaji wakubwa wa bandari za Tanzania, ikiwa na takribani tani milioni 7.2 za mizigo iliyopitishwa mwaka 2023.

Rais Dkt. Samia amepongeza hatua ya DRC kujenga barabara yenye urefu wa kilomita 450 kutoka Manono hadi Bandari ya Kalemie, sambamba na uboreshaji wa bandari hiyo, akisema miradi hiyo itachangia kuimarisha biashara na uwekezaji kupitia Ushoroba wa Kati. 

Amesema Tanzania inaendelea kuboresha bandari zake katika Ziwa Tanganyika, kuongeza idadi ya meli na kuendeleza mtandao wa reli kuelekea Magharibi ili kurahisisha usafirishaji
wa mizigo kwenda DRC na nchi nyingine jirani.

Viongozi hao pia wamejadili kupanua ushirikiano katika sekta za mawasiliano, nishati na madini. Rais Dkt. Samia ametoa wito kwa nchi hizo mbili kushirikiana katika uchimbaji, uongezaji thamani, utafiti na masoko ya madini ili kuongeza manufaa yatokanayo na rasilimali hizo.

Aidha, Rais Dkt. Samia ameialika DRC kujiunga na Kituo cha Madini na Jiosayansi cha Afrika (AMGC) kilichopo Tanzania ili kushirikiana katika tafiti, kubadilishana utaalamu na kuendeleza uwekezaji wenye tija katika sekta ya madini.

Tanzania pia imeeleza utayari wa kupanua biashara ya mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi na DRC, pamoja na kutoa huduma za kibingwa na kuendesha kambi za matibabu nchini humo.

Katika masuala ya amani na usalama, Rais Dkt. Samia amesema Tanzania itaendelea kuunga mkono juhudi za DRC za kurejesha amani na utulivu Mashariki mwa nchi hiyo.

Kwa upande wake, Rais Tshisekedi amesema DRC imeanza maandalizi ya kujenga bandari kavu jijini Dar es Salaam ili kurahisisha usafirishaji wa mizigo ya nchi hiyo inayopitia
Bandari ya Dar es Salaam.

Bandari hiyo kavu inatarajiwa kutoa huduma za forodha, usimamizi wa mizigo ya baharini, uthibitishaji wa madini na udhibiti wa ubora wa bidhaa.

“Tunataka kurahisisha zaidi biashara kati ya nchi zetu. Ujenzi wa bandari kavu Dar es Salaam utasaidia kuboresha usimamizi na usafirishaji wa mizigo ya DRC inayopitia Tanzania,” amesema Rais Tshisekedi.

Vilevile, Rais Tshisekedi amesema DRC inatathmini uwezekano wa kupanua safari za Shirika la Ndege Tanzania (Air Tanzania) nchini humo, hatua inayolenga kuongeza usafiri, utalii, biashara na mwingiliano wa wananchi wa nchi hizo mbili.

Rais Tshisekedi pia amesisitiza umuhimu wa Afrika kuchakata madini na rasilimali zake ndani ya bara ili kuongeza thamani, kujenga minyororo ya uzalishaji na kutengeneza ajira kwa vijana.

“Afrika inapaswa kuongeza thamani ya rasilimali zake ndani ya bara. Hii itatuwezesha kujenga minyororo ya uzalishaji, kuongeza manufaa ya rasilimali zetu na kutengeneza ajira zaidi kwa vijana wetu,” amesema Rais Tshisekedi.

Ziara hiyo imeweka msukumo mpya katika matumizi ya Ushoroba wa Kati na Ziwa Tanganyika kama mihimili muhimu ya biashara, uwekezaji na uhusiano wa kiuchumi kati ya Tanzania na DRC.

Tanzania na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo zina uhusiano wa muda mrefu wa kidiplomasia, kiuchumi na kijamii.

Nchi zote mbili ni wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), jambo linalotoa fursa ya kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi na kikanda.

Kijiografia, Tanzania ina nafasi ya kimkakati ya kuiunganisha DRC na Bahari ya Hindi na masoko ya kimataifa, huku DRC ikiwa soko muhimu kwa bidhaa, huduma na uwekezaji kutoka Tanzania.

DRC ina watu zaidi ya milioni 100 na utajiri mkubwa wa rasilimali, hali inayoifanya kuwa moja ya masoko muhimu katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.

Post a Comment

0 Comments