6/recent/ticker-posts

Viongozi muna wajibu wa kuwafikia wananchi na watumishi wa ngazi za chini kusikiliza na kutatua changamoto zao

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla akizungumza na wafanyabiashara wa Soko la Chuini Wilaya ya Magharibi "A" Unguja wakati wa ziara yake ya kukagua maendeleo ya biashara katika soko hilo pamoja na kusikiliza changamoto mbali mbali zinazowakabili wafanyabiashara Sokoni hapo.

Imetolewa na Kitengo cha Habari (OMPR )

" Viongozi muna wajibu wa kuwafikia wananchi na watumishi wa ngazi za chini kusikiliza na kutatua changamoto zao badala ya kubakia maofisini muda wote wa kazi.

Maelekzo hayo hutolewa mara kwa mara Mhe. Hemed Suleiman Abdulla wakati akizungumza na viongozi wa Serikali ama katika ziara zake kwa lengo la kuwakumbusha wajibu wao wa msingi wa kuwatumikia wananchi.

Licha ya kutoa Maelekezo haya, Mhe, Hemedi huwaonesha mifano na kutoa msisitizo mkubwa kwa kufanya ziara mbali mbali katika miradi ya maendeleo pamoja na kuzitembelea Wizara mbali mbali ili kujua changamoto zinazozikabili ili aweze kushirikiana nao katika kuzitafutia utatuzi.

Mapema Julai 04, 2026 Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar akiambatana na viongozi mbali mbali wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi alikagua maendelo ya ujenzi wa bararabara zinazojengwa ndani ya Mkoa wa Mjini Magharibi ikiwemo barabara ya Viwanja vya Magereza hadi kwa Mchina yenye urefu wa KM 0.6, barabara ya Mwanakwerekwe Makaburini – Magomeni hadi Kariakoo yenye urefu wa KM 3.7 , FLYOVER Amani, barabara ta Amani-Mikunguni hadi kwa Biziredi yenye urefu wa Km 2.5, barabara ya Mnazimmoja-Malindi hadi Kinazini yenye urefu wa Km 2,4 pamoja na barabara ya ZRA hadi Fumba ambazo zote zinazojengwa kwa kiwango cha lami na hadi kufikia Disemba 2026 barabara hizo zitakuwa zimekamilika.

Mhe. Hemed alipongeza juhudi kubwa zinazofanywa na wizara ya Ujenzi na Uchukuzi kwa kusimamia vyema utekelezaji wa miradi ya maendeleo inayotekelezwa pamoja na kusema kuwa utakapokamilika ujenzi wa miundombinu ya barabara zitarahisisha upatikanaji wa huduma mbali mbali za kiuchumi na kijamii.

Amesema miundombinu bora ya barabara inafungua fursa mbalimbali za kiuchumi ikiwemo kuimarika kwa biashara, kuongezeka kwa pato la Taifa, kuongezeka thamani maeneo yote yaliyokaribu na miradi ya maendeleo.

Katika ziara zake Mhe. Hemed amewatoa hofu wananchi kuwa kila aliepisha ujenzi wa miundombinu atalipwa fidia kulingana na tathmini na viwango vya mali zao.

Mhe, Hemed aliwafahamisha wananchi kuwa adhma ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Daktari Hussein Ali Mwinyi ni kuona Wazanzibari wanaondokana na changamoto ya usafiri na usafirishaji ili kuondoa foleni na kurahisisha upatikanaji wa huduma mbalimbali hasa kwa vile Zanzibar ni visiwa vya Utalii.

Mhe. Hemed akauelekeza uongozi wa Wizara ya Ujanzi na Uchukuzi kuhakikisha wananchi wote waliopitiwa na ujenzi hasa wale waliokwisha kulipwa fidia zao wanaondoka katika maeneo hayo pamoja na kuandaa utaratibu mzuri wakuhakikisha hawarudi tena mara ujenzi wa miundombinu ya bararabara utakapokamilika ili kuweka haiba na muonekano mzuri wa miundombinu hio.

Katika kuhakikisha wananchi wa Zanzibar wanaondokana na changamoto ya huduma za usafiri hasa safari wa baharini, Serikali ya Awamu ya Nane inaendela na ujenzi wa bandari mbali mbali Unguja na Pemba ili kuondoa msongamano wa meli zinazosubiri ukuta kwa ajili ya kushusha na kupakia mizigo kwa lengo la kuimarisha biashara na upatikanaji wa bidhaa kwa wananchi kwa urahisi na uhakika.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alikagua ujenzi wa Bandari ya abiria na mizigo ya Maruhubi (Mpigaduri), ujenzi wa Kituo cha kushushia na kupimia mafuta Mangapwani na kukagua bandari Jumuishi ya Mangwapani ambayo inatarajiwa kuwa bandari kubwa zaidi katika ukanda wa Afrika Mashariki itakayokuwa na uwezo wa kuhudumia makontena laki mbili na hamsini kwa mwaka ambapo matarajio ya baadae ya Shirika la Bandari Zanzibar (ZPC) ni kuifanyia utanuzi zaidi bandari hio ili iweze kuhudumia makontena milioni moja kwa mwaka.

Alitamatisha ziara yake katika Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi kwa kufika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abedi Amaani Karume (AAKIA) kukagua ujenzi wa Jengo la Biashara na jengo la abiria la terminal two na kusema kuwa utakapokamilika ujenzi huo uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Zanzibar utakuwa ni miongoni mwa viwanja bora duniani kwa utoaji wahuduma bora kwa wageni wanaoingia na kutoka Zanzibar.

Hapa alitoa neno kwa wakandarasi wa majengo hayo kuhakikisha wanajenga kwa kufuata viwango vinavyotakiwa na kukamilisha miradi hio kwa wakati ili uwanja huo uweko tayari kupokea wageni wengi wanaotarajiwa kuingia nchini kwa shughuli za utalii lakini na katika kipindi cha Mishindano ya AFCON yanayotarajiwa kufanyika mwakani 2027.

Uwanja wa ndege ni lango kuu la ukuwaji wa uchumi wa nchi kwa kuingiza idadi kubwa ya watalii wanaosaidia kuongezeka kwa pato la Taifa na ajira kwa wananchi. Kutokana na umuhimu huo Mhe. Hemed amewataka wafanyakazi wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Zanzibar kuendelea kufanya kazi kwa weledi na nidhamu ya hali ya juu wakati wanapowahudumia wageni wanaoingia na kutoka nchini ili kuendelea kuitangaza na kulinda heshima ya Zanzibar.

Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi Mhe. Dkt, Khalid Salum Mohammed nae akamshukuru Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwa kuamua kufanya ziara ya kukagua miradi inayotekelezwa na wizara yake na kusema maelekezo yake yamekuwa yakileta msukumo wa kufanya ufuatliaji zaidi na kuhakikisha miradi hio inakamilika ka wakati uliopangwa.

Dkt. Khalid akamuhakikishaia Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kuwa ujenzi wa Barabara zote zinazojengwa ndani ya Mkoa wa Mjini Magharibi, Uwanja wa ndege na Bandari ya Mpigaduri utamalizika kabla ya mashindano ya AFKON ambayo yatatoa fursa mbali mbali za kiuchumi kwa wakaazi wa Zanzibar.

Ikafika zamu ya Wizara ya Kilimo, Maliasili, Umwagiliaji na Mifugo, Wizara yenye dhamana ya kuwasimia wakulima na wafugaji katika kuhakisha wanalima na kufuga kisasa zaidi kwa maslahi yao na Taifa kwa ujumla.

Asubuhi na mapema Julai 06, 2026 Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla alifika katika Kijiji cha Mtule kilichopo Wilaya ya Kusini, Mkoa wa Kusini Unguja kukagua uwekezaji wa kilimo cha mboga mboga na matunda na ufugaji wa kuku wa kienyeji uliowekezwa na bwana Rashid Khamis mzawa na mkaazi wa kijiji hicho.

Baada ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kufanya ukaguzi shambani hapo, alimpatia fursa mmiliki wa mradi huo kuzungumza mawili matatu na hapa Bwana khamis akamueleza Mhe. Hemed  kuwa zaidi ya shilingiza KIitanzania  milioni 150 ameziwekeza katika kilimo kilichojikita cha mapapai, mabilingani, pilipili boga, matikiti, tungule na ufugaji wa kuku wa kienyeji uliozalisha ajira kumi na mbali(2) na  kwa sasa wanajipanga kuanzisha kilimo cha spices.

Bwana Khamis akawashauri vijana kujikita katika kilimo na ufugaji na kusema kuwa kwa Zanzibar kilimo ni mtaji wenye faida kubwa endapo utaupa muda wa kutosha.

Baada ya kukagua shamba hilo lenye ukubwa wa zaidi ya hekta sita Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliwataka kwa watendaji wa Wizara ya Kilimo pamoja na wakulima na wafugaji, kulima na kufuga kwa kuangalia mahitaji ya soko la ndani, mahoteli ya kitalii na wagani wengine wanaingia Zanzibar.

Kijiji cha Bambi kinajulika sana kwa ukulima wa viazi vitamu na mboga mboga kama vile pilipili boga na tungule na katika kuendelea kuunga mkono jitihada za wajasiriamali wadogo wadogo, Mhe, Hemed alifika kijijini hapo kuwakagua wakulima na kuwasikiliza changamoto zao.

Na hapa akawashauri wakulima na wafugaji kuangalia fursa ambazo zitawasaidia kutimiza malengo yao na aliwataka vijana kuitumia fursa ya kilimo katika kutengeneza maisha yao na kuachana na mtazamo hasi wa kwamba ajira ni kuajiriwa Serikalini jambo ambalo si sahihi.

CHEJU ni eneo maarufu kwa ukulima wa zao la Mpunga. Licha ya kuwa na maeneo ya kutosha kwa ajili ya kilimo lakini bado Zanzibar inaagiza mchele kutoka nje ya nchi jambo ambalo limemlazimu Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kutaka kufahamu sekta ya kilimo inapitia changamoto gani hadi Zanzibar ikashindwa kujitosheleza kwa chakula cha ndani.

Alifika Cheju katika mashamba ya mpunga na hapa akapata fursa ya kukagua mashamba hayo lakini pia akajionea namna ya uvunaji wa mpunga kwa kutumia mashine ili kupunguza changamoto ya upotevu wa mpunga na kuokoa muda wa kukaa shambani.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar akawatakwa watendaji wa wizara ya Kilimo kuhakikisha sekta ya kilimo inatanua wigo mpana wa kuekeza katika kilimo cha biashara na kuachana na kilimo cha kujikimu kisichokuwa na faida kwa wakulima.

Akawasihi wakulima kuwa tayari kukaribisha wawekezaji ili kupata fursa nyingi ikiwemo kujifunza mbinu mbali mbali za kulima kilimo cha kisasa chenye tija zaidi.

Akatoa agizo kwa Wizara ya Kilimo kuangalia namna bora ya kuwasaidia na kuwawezesha wakulima na wafugaji kwa kuwapatia elimu na nyenzo mbali mbali zitakazowasaidia kukuza na kuendeleza miradi yao.

Akiwa bado katika kijiji caha Cheju, Mhe. Hemed alikagua eneo la kufugia ng’ombe wa maziwa ambapo alisema lengo la Serikali ni kuona Ufugaji Zanzibar unakuwa na kuimarika hasa kwa vile ufugaji ni fursa ambayo inaweza kuwasaidia vijana kujiajiri na kujikwamua na umasikini kwa kukuza uchumi wa mtu mmoja mmoja na Taifa kwa jumla.

Mtazamo wa Serikali ni kuwa na ufugaji mkubwa zaidi na kuhakikisha wafugaji wanasaidiwa kwa kupewa elimu ya ufugaji wa kisasa lakini pia kuwawezesha na kuwaonesha fursa ambazo wanaweza kuzitumia ndani ya Zanzibar na Tanzania kwa Ujumla.

Waziri wa Kilimo, Umwagiliaji, Maliasili na Mifugo Mhe. Suleiman Massoud Makame akaeleza kuwa jambo zuri na lakufurahisha katika maendeleo ya sekta ya kilimo ni kuwa wafadhili mbali mbali wamekuwa na mwamko wa wakuekeza na kusaidia katika sekta ya kilimo kwa kuhamasisha wakulima kulima kilimo cha kisasa kinachotumia teknolojia zaidi jambo lililochangia kuongezeka maradufu kwa uzalishaji wa mpunga kutoka vipolo kumi kwa robo eka na kufikia zaidi ya vipolo 22.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alihitimisha ziara yake kwa kukagua ujenzi wa Kituo cha kisasa cha SEED FARM kwa ajili ya kuhifadhia mbegu za mazao mbali mbali hasa mbegu za mpunga kinachojengwa katika eneo la Kibonde Mzungu, Wilaya ya magharibi “B” Unguja ambacho kitakuwa na uwezo wa kuhifadhi mbegu lukuki kwa ajili ya wakulima wa mpunga wa Zanzibar.

Hapa aliwasihi vijana kujikita zaidi katika kujiajiri kwenye na kuekeza katika maeneo mbali mbali ikiwemo kilimo na ufugaji ambao una faida kubwa endapo wakulima na wafugaji watafuga na kulima kisasa zaidi.

KILIMO NI UTI WA MGONGO, TULIME KISAYANSI

KILIMO BIASHARA CHENYE TIJA ZAIDI.

Post a Comment

0 Comments