Accra, Ghana — Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk Jakaya Mrisho Kikwete, amezitaka serikali za Afrika kuacha kutegemea zaidi matamko na ahadi zisizoambatana na utekelezaji, na badala yake kuweka fedha za ndani, uwajibikaji na matumizi ya ubunifu kwa kiwango kikubwa kuwa msingi wa ajenda ya afya ya bara hilo.
Dk Kikwete alitoa wito huo katika Mjadala wa Ngazi ya Juu wa Sera uliofanyika Julai 20, 2026 katika Hoteli ya Kempinski, Accra, pembezoni mwa Mkutano Maalumu wa Umoja wa Afrika kuhusu Afya.
Mjadala huo uliwakutanisha mawaziri, watunga sera, jumuiya za kiuchumi za kikanda, taasisi za bara, washirika wa maendeleo, viongozi wa sekta binafsi pamoja na wataalamu wa afya duniani.
Uliandaliwa kwa pamoja na African Renaissance Trust na Wakfu wa Jakaya Mrisho Kikwete, kwa ushirikiano na Tume ya Umoja wa Afrika na wadau wengine, chini ya kaulimbiu: “Kuendeleza Ajenda ya Afya ya Afrika kupitia Ufadhili wa Ndani, Uwajibikaji na Ubunifu wa Kimkakati.”
Dk Kikwete alisema utegemezi wa muda mrefu wa Afrika kwa misaada ya nje katika kugharamia huduma za afya hauwezi tena kuendelea kuwa msingi mkuu wa mifumo ya afya ya bara hilo.
Alisema kupungua kwa misaada ya maendeleo, kuongezeka kwa madeni ya serikali na mahitaji makubwa ya huduma bora za afya vinailazimisha Afrika kubadilisha namna inavyofadhili na kusimamia sekta hiyo.
“Ujumbe kutoka Eswatini hadi Accra ni mmoja: Afrika lazima izidi kugharamia, kuzalisha na kulinda mustakabali wake wa afya,” alisema.
Mkutano huo umefanyika miaka 25 baada ya Azimio la Abuja la mwaka 2001, ambalo lilizitaka nchi wanachama wa Umoja wa Afrika kutenga angalau asilimia 15 ya bajeti zao za kitaifa kwa ajili ya afya.
Hata hivyo, nchi nyingi bado zinakabiliwa na mapungufu makubwa ya fedha, wakati bara hilo likiendelea kubeba mzigo mkubwa wa Virusi vya Ukimwi, kifua kikuu, malaria, vifo vinavyoweza kuzuilika vya wajawazito na magonjwa yasiyoambukiza.
Dk Kikwete alitoa msisitizo maalumu kuhusu usalama wa mama na mtoto, akisema takribani wanawake 260,000 hufariki kila mwaka duniani kutokana na matatizo yanayohusiana na ujauzito na kujifungua, huku karibu asilimia 70 ya vifo hivyo vikitokea Afrika.
Alisema hali hiyo haiwezi kuelezwa kuwa ni kushindwa kwa sayansi, kwa sababu dunia tayari ina maarifa, dawa, vifaa na teknolojia zinazoweza kuzuia idadi kubwa ya vifo hivyo.
Kwa maoni yake, tatizo kubwa ni kushindwa kuyafikisha maarifa na teknolojia hizo kwa watu wanaozihitaji.
“Mama anaporudi nyumbani salama, ni kwa sababu fedha, ushahidi wa kisayansi na utoaji wa huduma vimefanikiwa kukutana,” alisema.
“Changamoto iliyo mbele ya mkutano huu si kuvumbua tena, bali ni kupeleka ubunifu uliopo kwa wananchi — kuutoa kwenye kumbi za mikutano na miradi ya majaribio na kuuweka mikononi mwa wauguzi, wakunga na wahudumu wa afya ya jamii wanaookoa maisha kila siku.”
Akizungumzia uzoefu wa Tanzania, Dk Kikwete alisema Wakfu wa Jakaya Mrisho Kikwete umeshirikiana na Wizara ya Afya pamoja na taasisi za kitaifa za utafiti kuchambua hali ya afya ya mama na mtoto na kuanzisha Mkutano wa Kitaifa wa Kisayansi unaofanyika kila baada ya miaka miwili.
Alisema katika kipindi hicho, vifo vya wajawazito nchini Tanzania vimepungua kutoka zaidi ya vifo 550 kwa kila watoto 100,000 wanaozaliwa hai hadi vifo 104.
Kwa hatua hiyo, Tanzania ina nafasi ya kufikia lengo la Maendeleo Endelevu la kupunguza vifo hivyo hadi 70 kwa kila watoto 100,000 wanaozaliwa hai ifikapo mwaka 2030.
Dk Kikwete alisema suala muhimu si kiasi cha fedha kinachotengwa kwa afya pekee, bali ni kama fedha hizo zinawafikia watu wanaozihitaji na kutoa matokeo yanayoonekana.
“Swali si tunatumia kiasi gani katika afya. Swali ni kama uwekezaji wetu unawafikia wananchi wanaouhitaji zaidi,” alisema.
Alibainisha kuwa wananchi hawapimi mafanikio ya matumizi ya afya kwa asilimia ya Pato la Taifa, bali kwa kuangalia kama dawa zinapatikana hospitalini, wahudumu wa afya wapo kazini, vifaa vya uchunguzi vinapatikana na kama mama na watoto wanaendelea kuishi.
Sehemu muhimu ya mjadala huo ilikuwa uzinduzi wa mfumo wa African Renaissance Health Financing Insights Dashboard, unaolenga kuzisaidia serikali kufuatilia ahadi za kifedha, matumizi ya bajeti, mapungufu ya fedha na matokeo yanayopatikana.
Mfumo huo pia unatarajiwa kuimarisha ushirikiano kati ya wizara za fedha na wizara za afya katika kupanga na kusimamia uwekezaji wa afya.
“Uwajibikaji lazima sasa uwe nguzo kuu ya ufadhili wa afya, kwa sababu tukiepuka ubadhirifu, tunaweza kufanya mengi zaidi kwa fedha chache,” alisema Dk Kikwete.
Aidha, alitaka Afrika kupunguza utegemezi wa dawa na chanjo kutoka nje, akieleza kuwa bara hilo linaagiza kutoka nje kati ya asilimia 80 na 100 ya dawa zake na zaidi ya asilimia 99 ya chanjo.
Alihimiza nchi wanachama kuunga mkono Wakala wa Dawa wa Afrika, kuwekeza katika uzalishaji wa dawa ndani ya bara na kutumia fursa za biashara ya kikanda kuimarisha usalama wa afya.
Dk Kikwete aliwasilisha vipaumbele vitano: kuifanya afya kuwa uwekezaji wa kimkakati; kuongeza mapato ya ndani kupitia bima, kodi bunifu na matumizi yenye ufanisi; kulinda huduma muhimu wakati misaada inapopungua; kuimarisha uwajibikaji; na kuongeza ushirikiano wa kikanda.
Kamishna wa Umoja wa Afrika anayeshughulikia Afya, Masuala ya Kibinadamu na Maendeleo ya Jamii, Balozi Amma Twum-Amoah, alisema mafanikio lazima yapimwe kwa mabadiliko yanayoonekana katika maisha ya wananchi.
“Vipaumbele vyetu lazima vionekane katika utekelezaji, na maendeleo yetu yapimwe kwa maboresho yanayopatikana katika maisha ya kila siku ya watu wetu,” alisema.
Dk Kikwete alihitimisha kwa kusema kuwa Afrika haina upungufu wa ahadi, mikakati au ubunifu. Kinachokosekana ni utekelezaji kwa kiwango kikubwa.
“Tuondoke Accra tukiwa na dhamira ya kubadili ahadi kuwa bajeti, bajeti kuwa programu, programu kuwa matokeo yanayopimika, na matokeo kuwa maisha marefu, yenye afya na uzalishaji zaidi kwa wananchi tunaowahudumia.”


0 Comments