Na.Mukrim Mohamed
Viongozi wa Jimbo la Chaani wameanza hatua za kuweka mfumo mpya wa kuimarisha kilimo cha mpunga kwa kuvisimamia vikundi vya wakulima kitaalamu, hatua inayolenga kukifanya kilimo hicho kuwa endelevu na kuwa chanzo cha ajira kwa vijana.
Akizungumza katika kikao na wakulima wa mpunga wa Jimbo hilo, Mbunge wa Chaani ambaye pia ni Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhe. Ayoub Mohamed Mahmoud, alisema hatua iliyopo sasa ni kuhakikisha vikundi vya wakulima vilivyoundwa vinasajiliwa na kupewa usimamizi wa kitaalamu ili kuweka msingi imara wa maendeleo ya sekta hiyo.
Alisema ili kusaidia sekta ya kilimo kwa ufanisi, ni lazima isimamiwe kwa mtazamo wa kitaalamu zaidi na kuwekwa mikakati thabiti itakayohakikisha inaendelea kuwa na tija kwa muda mrefu.
"Tupo kwenye hatua ya utekelezaji, tumeshaunda vikundi na sasa tupo kwenye hatua ya kuvisajili. Kama tunataka kuwasaidia wakulima kiukweli lazima tusimamie jambo hili kitaalamu na si kufanya siasa. Tunataka sekta hii ya kilimo iwe endelevu," alisema Mhe. Ayoub.
Alisema uendelevu wa kilimo unamaanisha kujenga mazingira yatakayowezesha sekta hiyo kuzalisha ajira ndani yake, ambapo vijana wataweza kuona kilimo kama fursa ya ajira na kipato badala ya shughuli inayofanywa na wazee pekee.
"Tutengeneze ajira ndani ya hiki hiki kilimo mnacholima, watoto wetu watengenezewe ajira humu humu. Ajira hizo zitatengenezwa vipi? Ndiyo maana tumewaletea wataalamu," aliongeza.
Kwa upande wake, Mwakilishi wa Jimbo la Chaani, Mhe. Juma Usonge Hamad, alisema tayari kuna programu mbalimbali zinazolenga kuimarisha sekta ya kilimo ndani ya jimbo hilo kwa kuwasaidia wakulima kuongeza uzalishaji na kupata manufaa zaidi kutokana na shughuli zao.
Alisema kupitia programu hizo, wakulima wataweza kuzalisha kwa ufanisi, kuwa na uhakika wa chakula kwa ajili ya familia zao pamoja na kutumia kilimo kama fursa ya kufanya biashara na kuongeza kipato.
Akitoa mtazamo wa kitaalamu, Profesa Felista Michel Mombo kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine, amesema changamoto kubwa iliyopo kwa sasa si ukosefu wa rasilimali au mipango, bali ni namna ya kuratibu na kuunganisha juhudi zilizopo ili ziweze kumsaidia mkulima kufikia kilimo chenye tija.
Profesa Felista alisema kinachohitajika kwa sasa si kuanzisha jambo jipya, bali ni kuhakikisha mambo yaliyopo yanafanyiwa kazi kwa mpangilio mzuri, ikiwemo kubaini changamoto halisi zinazowakabili wakulima ili kupatikane suluhisho linaloendana na mahitaji yao.
Alisema kupitia uratibu mzuri wa huduma za kitaalamu, upatikanaji wa mahitaji muhimu ya kilimo na ushirikiano kati ya wadau mbalimbali, wakulima wataweza kuongeza uzalishaji na kunufaika zaidi na shughuli zao.
Nao baadhi ya wakulima waliohudhuria kikao hicho walisema hatua ya viongozi kukutana nao na kusikiliza changamoto zao imeongeza matumaini ya kupatikana kwa ufumbuzi wa muda mrefu utakaowawezesha kuongeza uzalishaji na kuboresha maisha yao.
Waliwataka viongozi hao kuendelea kufuatilia na kutatua changamoto zinazowakabili, ikiwemo upatikanaji wa pembejeo na mahitaji mengine muhimu ya kilimo, ili kuwawezesha kuongeza uzalishaji wa mpunga na kufanya kilimo hicho kuwa na tija zaidi.
Kikao hicho ni sehemu ya juhudi za viongozi wa Jimbo la Chaani za kuimarisha sekta ya kilimo kwa kusikiliza maoni ya wakulima moja kwa moja na kuweka mikakati ya kutatua changamoto zinazokwamisha maendeleo ya wakulima, pamoja na kujenga mazingira yatakayowavutia vijana wengi kushiriki katika kilimo.
0 Comments