Na.Khadija mgeni
Vyama vya ushirika vimetakiwa kuzingatia mipango ya maendeleo na usimamizi bora wa biashara ili viweze kujiendesha kwa ufanisi na kufikia malengo ya maendeleo ya kiuchumi.
Kauli hiyo imetolewa na Afisa Mwandamizi wa Idara ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania Bara, Sadiki Juma Khamis, wakati akifunga mafunzo ya kuwajengea uwezo wanaushirika kutoka Mkoa wa Mjini Magharibi yaliyofanyika katika ukumbi wa Wizara ya Vijana, Ajira na Uwezeshaji, Mpendae.
Amesema mafunzo hayo ni ya kimkakati ili kuhakikisha vyama hivyo vinajiendesha kwa misingi bora ya biashara na kufanikisha malengo yaliyowekwa.
Naye Mkufunzi wa mafunzo hayo, Justin Mogendi, amesema washiriki wamepatiwa elimu itakayowasaidia kuwa na mipango Bora pamoja na kufuata dira na dhamira ya uendeshaji wa shughuli zao kwa mfumo wa kibiashara wenye tija.
Kwa upande wake, Mkuu wa Divisheni ya Maendeleo ya Ushirika, Abdulmajid Masoud Khalfan, amevitaka vyama hivyo kujifunza kutoka kwa wanaushirika waliofanikiwa ili kutumia mbinu bora zinazosaidia kuimarisha maendeleo ya vyama vyao.
Nae Mshiriki wa Mafunzo hayo Mtumwa Taibu Hussein kutoka Chama cha Watembeza Watalii Zanzibar (ZAFEGUCO), amesema mafunzo hayo yamekuwa chachu ya kuwasaidia kufikia malengo yao ya maendeleo ya kiuchumi.
Naye Gharoub Abeid Moh’d kutoka Chama cha Ushirika Kwetu Art Sokoni amesema fursa hiyo imewapa mwanga mpya wa namna bora ya kuendesha vyama vya ushirika na kuahidi kuwaelimisha wengine ili nao wanufaike.
Mafunzo hayo yamefanyika katika wilaya saba za Unguja kupitia ushirikiano kati ya Tume ya Maendeleo ya Ushirika Dodoma na Idara ya Maendeleo ya Ushirika Zanzibar, yakilenga kuviwezesha vyama vya ushirika kujiendesha kwa ufanisi zaidi.


0 Comments