Na.Khadija Mgeni.WHSUM.
Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo Zanzibar, Mheshimiwa Dkt. Riziki Pembe Juma, amewataka Wanafunzi, wasomi na wadau wa lugha ya Kiswahili kuhakikisha wanaitumia lugha hiyo kama nyenzo muhimu ya maendeleo, hasa katika sekta ya teknolojia na ajira.
Ameyasema hayo wakati akifungua Kongamano la 16 la Chama cha Wanafunzi wa Kiswahili wa Vyuo Vikuu na vya kati (CHAWAKITA) Taifa, lililofanyika katika Ukumbi wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM).
Amesema ni wakati sasa wa kubadilisha dhana ya Kiswahili kuwa zaidi ya somo la darasani na kukifanya kuwa chombo cha ubunifu, biashara na maarifa.
Dkt, Riziki amewashauri wanafunzi kujikita katika uandishi wa makala, tafiti na maudhui ya kidijitali kwa Kiswahili ili kuongeza wigo wa matumizi ya lugha hiyo katika Dunia ya sasa inayokua kwa kasi kiteknolojia.
Amefahamisha kuwa kumeonekana kuwepo kwa uoga wa kuthubutu Kujitokeza katika kuzichangamkia fursa za kiswahili Duniani, hivyo amewataka Wanafunzi hao, kuzichangamkia fursa hizo.
Pia amewaomba Walimu na Wahadhiri wa Kiswahili kuwajengea uwezo wanafunzi na kuwahamasisha Kujitoa katika kuzisogelea fursa kokote Duniani.
Hata hivyo Dkt. Riziki amewapongeza CHAWAKITA kwa kuendelea kufanya makongamano kama hayo kwa Lengo la kuhamasisha kukikuza Kiswahili kitambulike Afrika Mashariki na Duniani kote na kuwataka kuendelea huku akiwaahidi kuwa Wizara zao zote mbili zinazosimamia masuala ya Utamaduni na sanaa (SMZ) na (SMT) zitaendelea kuwasimamia na kuwapatia miongozo ili waweze kupiga hatua zaidi.
Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dodoma, Profesa Razack Bakari Lokina, ameeleza kuwa kongamano hilo linaonyesha dhamira thabiti ya Serikali zote mbili katika kutambua umuhimu wa kuwekeza katika lugha ya Kiswahili kwa maendeleo ya Taifa.
Akisoma Risala ya Chama cha Wanafunzi wa Kiswahili wa Vyuo Vikuu na vya kati, (CHAWAKITA) Taifa Mwenyekiti wa chama hicho Bi Neema Ntambala amesema Dhamira ya kuanzishwa kwa chama hicho ni kukuza na kuendeleza lugha ya Kiswahili ndani na nje ya mipaka ya Tanzania kwa kushirikiana na wadau wengine wa Lugha hiyo.
Amesema CHAWAKITA kimefanya makongamano 15 katika mikoa mbalimbali ukiwemo, Arusha, Morogoro, Iringa na Mbeya na sasa Dodoma ikiwa ni Kongamano la 16 linalofaanyika katika Chuo Kikuu Cha Dodoma, ikiwa Mada kuu ya Kongamano hilo ni “KISWAHILI NI NYENZO YA FURSA, MAWASILIANO NA MAENDELEO KATIKA ULIMWENGU”. Ikilenga kuwa, Kiswahili ni Chombo cha fursa kwa kufungua nafasi za ajira, elimu, biashara, tafiti na ushirikiano wa kima.
Baadhi ya washiriki wa kongamano hilo wameeleza kuwa maelekezo yaliyotolewa yamewapa ufahamu mpya kuhusu nafasi ya Kiswahili, hasa katika kufikia fursa mbalimbali.Kongamano hilo la siku mbili limewakutanisha wanafunzi na wataalamu wa Kiswahili kutoka Afrika Mashariki kwa lengo la kujadili mchango wa lugha hiyo katika maendeleo ya kijamii, kiuchumi, na kiteknolojia.







0 Comments