Naibu Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, Mhe. Ali Abdulgulam Hussein, amesema Serikali itaendelea kuwekeza katika maendeleo ya michezo kwa kuimarisha miundombinu, kuwajengea uwezo waamuzi na kuweka mazingira bora yatakayowezesha kukuza vipaji vya vijana nchini.
Ameyasema hayo wakati akifungua mafunzo ya zoezi la utimamu wa mwili kwa waamuzi wa mpira wa miguu wa Unguja yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mao Zedong, Wilaya ya Mjini.
Amesema Serikali imejipanga kuhakikisha sekta ya michezo, inaendelea kuimarika kupitia ujenzi na ukarabati wa viwanja vya kisasa vinavyokidhi viwango vya kimataifa, hatua ambayo inalenga kuinua kiwango cha soka Zanzibar na kuwawezesha wanamichezo kupata mazingira bora ya kuendeleza vipaji vyao.
Aidha amesema Shirikisho la Mpira wa Miguu Zanzibar (ZFF) limekuwa likishirikiana na Wizara ya Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo katika kuwawezesha wachezaji na waamuzi kucheza ligi Katika maeneo mbali mbali ya viwanja vya michezo .
Mhe.Gulam amesema kupitia mafunzo hayo yatawasaidia waamuzi kuwa na utayari wa kimwili na kiakili ili kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi, huku akiwataka kuendelea kujifunza na kuongeza ujuzi kupitia vyanzo mbalimbali, ikiwemo mitandao ya kijamii.
" Uamuzi wa soka ni ajira inayoweza kubadilisha maisha ya vijana na kuwafungulia fursa mbalimbali ndani na nje ya nchi."amesema Mhe. Gulam.
Aidha, amewasisitiza waamuzi kuzingatia nidhamu, misingi na maadili ya kazi yao ili kufikia lengo la Serikali la kuimarisha sekta ya michezo nchini.
Hata hivyo amemtaka Mwenyekiti wa Bodi ya Ligi kuhakikisha anazingatia maslahi ya waamuzi hao ikiwemo kuboresha mazingira yao ya kazi pamoja na kuwawezesha kupata bima ya afya, ili kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi
Hata hivyo, ameeleza kuwa ligi mbalimbali ni sehemu muhimu ya kuitangaza Zanzibar, hivyo amewataka waamuzi na wadau wa soka kutumia mashindano hayo kuitangaza Zanzibar na maandalizi ya AFCON, jambo litakalosaidia kuongeza hamasa na fursa za kiuchumi.
Pia, ameupongeza uongozi wa ZFF pamoja na Chama cha Waamuzi kwa madaraja mbalimbali kwa kazi wanayoendelea kuifanya, licha ya changamoto wanazokabiliana nazo katika utekelezaji wa majukumu yao.
Kwa upande wake, Katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la Michezo Zanzibar, Said Marine, amesema mpira wa miguu ni uwekezaji mkubwa unaoweza kuwainua vijana kiuchumi na kuwafungulia fursa mbalimbali.
Amewataka waamuzi kuendeleza vipaji vyao, kuunga mkono juhudi za Serikali na kuhakikisha wanatekeleza majukumu yao kwa weledi na uadilifu.
Akitoa tathmini ya mafunzo hayo, Mkufunzi wa Utimamu wa Mwili kwa Waamuzi ambaye pia ni Katibu wa Kamati ya Waamuzi ya Zanzibar Issa Haji Vuai, amesema Serikali kupitia ZFF imeweka utaratibu maalum wa kila mwaka wa kuwaandaa waamuzi wa madaraja mbalimbali kwa kuwafanyia vipimo vya utimamu wa mwili.
Amesema jumla ya waamuzi 73 walishiriki katika mtihani huo, ambapo waamuzi 61 wamefanikiwa kumaliza mtihani, huku waamuzi 12 wakishindwa kufikia viwango vilivyowekwa na kutakiwa kusubiri kwa muda wa wiki tatu kabla ya kurudia upimaji huo .
Zoezi la upimaji wa utimamu wa mwili kwa waamuzi wa Ligi Kuu ya Zanzibar kwa mwaka 2026 linatarajiwa kukamilika baada ya siku nne.



%20(1).jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
0 Comments