6/recent/ticker-posts

RAIS DKT. MWINYI AFUNGUA JUKWAA LA UWEKEZAJI ZANZIBAR 2026, ATOA WITO WA KUNUFAIKA NA FURSA ZA UWEKEZAJI

 

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema Zanzibar imeingia katika hatua mpya ya mageuzi ya kiuchumi yanayolenga kuimarisha ushindani katika soko la kimataifa kwa kupanua fursa za uwekezaji, kuimarisha msingi mpana wa uchumi na kujenga mazingira rafiki yatakayowezesha ukuaji endelevu na ustawi wa wananchi.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 04 Juni 2026, alipofungua rasmi Jukwaa la Uwekezaji Zanzibar 2026 lililofanyika katika Hoteli ya Golden Tulip Airport, Mkoa wa Mjini Magharibi, likiwakutanisha wawekezaji kutoka mataifa mbalimbali duniani.

Aidha, Rais Dkt. Mwinyi amesisitiza kuwa Serikali inaendelea kuboresha mazingira ya biashara kupitia uwekezaji mkubwa katika miundombinu, mageuzi ya taasisi na matumizi ya mifumo ya kidijitali ili kuvutia wawekezaji zaidi na kuongeza ushindani wa Zanzibar katika soko la kimataifa.

Halikadhalika, Rais Dkt. Mwinyi amesema zaidi ya miradi 800 ya uwekezaji yenye thamani ya zaidi ya Dola za Marekani bilioni 9 inaendelea kutekelezwa Zanzibar, huku uchumi ukikua kwa asilimia 7.3 na mfumuko wa bei ukidhibitiwa katika asilimia 4.1.

Katika hafla hiyo, Rais Dkt. Mwinyi pia alishuhudia utiaji saini wa mikataba ya ushirikiano kati ya Mamlaka ya Uwekezaji na Ukuzaji wa Maeneo Huru Zanzibar (ZIPA), Taasisi ya Wawekezaji ya Marekani na Benki ya AfriExim, hatua inayolenga kuimarisha ushirikiano wa kimataifa na kuongeza uwekezaji Zanzibar.

Jukwaa la Uwekezaji Zanzibar 2026 limewakutanisha washiriki takribani 600 kutoka mataifa mbalimbali duniani, wakiwemo wawekezaji, taasisi za kifedha, washirika wa maendeleo, wafanyabiashara pamoja na Watanzania wanaoishi nje ya nchi (Diaspora).














Post a Comment

0 Comments