6/recent/ticker-posts

Wanaushirika kuzingatia mafunzo wanayopatiwa ili kupata ujuzi wa msingi wa kuendesha biashara


Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Ushirika Zanzibar, Zainab Abdulqadir Hassan, amewataka wanaushirika kuzingatia mafunzo wanayopatiwa ili kupata ujuzi wa msingi wa kuendesha biashara kwa lengo la kujiimarisha kiuchumi.

Ameyasema hayo wakati akifungua mafunzo ya kuwajengea uwezo wanaushirika kutoka Wilaya ya Mjini na Magharibi ‘A’, yaliyofanyika katika ukumbi wa Wizara ya Vijana, Ajira na Uwezeshaji, Mpendae.

Amesema mafunzo hayo yatawezesha vyama vya ushirika kujiendesha kibiashara kwa ufanisi, kukuza shughuli zao na kuongeza faida kupitia usimamizi bora na uzalishaji unaozingatia mahitaji ya soko.

Aidha, amesema vyama vya ushirika vinapaswa kuendeshwa kimkakati ili kuzalisha bidhaa zenye ubora na uwezo wa kushindana katika soko la kisasa.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Utafiti na Mafunzo kutoka Tume ya Maendeleo ya Ushirika Dodoma, Grace Masambaji,
amewataka washiriki hao kutumia  mafunzo hayo ili kufikia lengo la kuwa na vyama vya ushirika vya kisasa vinavyoendeshwa kidijitali na kwa misingi ya kibiashara.

Naye Mwezeshaji wa mafunzo hayo, Justin Mogendi, amesema mafunzo hayo yatawasaidia wanaushirika kukabiliana na changamoto za masoko pamoja na kuongeza ushindani wa bidhaa zao.

Ameeleza kuwa mafunzo hayo ya kimkakati yanalenga kuinua maisha na maslahi ya wanachama hao kwa kuwapatia ujuzi wa kuzalisha bidhaa zinazokidhi mahitaji ya soko la kisasa na kuongeza ubunifu kulingana na mahitaji ya wateja.

Mafunzo hayo yameandaliwa kupitia ushirikiano kati ya Tume ya Maendeleo ya Ushirika Dodoma na Idara ya Maendeleo ya Ushirika Zanzibar kwa lengo la kuvijengea uwezo vyama vya ushirika kujiendesha kwa ufanisi.

Post a Comment

0 Comments