6/recent/ticker-posts

Tahadhari za mapema ni muhimu kwa wakazi wa maeneo ya mabondeni kutokana na jiografia yake



Afisa Operesheni na Misaada ya Kibinadamu kutoka Kamisheni ya Kukabiliana na Maafa Zanzibar, Mohammad Mwinyi Hassan, amesema tahadhari za mapema ni muhimu kwa wakazi wa maeneo ya mabondeni kutokana na jiografia yake kuwa rahisi kukumbwa na mafuriko na madibwi ya maji 

Akizungumza wakati wa mafunzo kwa kamati za maafa za Shehia ya Kinuni na Muembe Majogoo yaliyofanyika katika Skuli ya Kinuni, Wilaya ya Magharibi ‘B’ Unguja, amesema jamii inapaswa kuchukua hatua za kujikinga ili kupunguza athari za majanga.
Amesisitiza umuhimu wa kutumia maji salama kwa kuyachemsha au kuyatibu, ili kuepuka maambukizi ya bakteria yanayotokana na kuchanganyika kwa maji safi na maji taka hasa pale mabomba yanapopasuka.

Aidha, amewataka wakazi wa maeneo ya majimaji kuwa makini na kuchukua tahadhari za mapema ili kujikinga na magonjwa ya tumbo  yanayoweza kusababishwa na mazingira hayo.

Ameongeza kuwa pamoja na juhudi za utoaji elimu, bado kuna baadhi ya wananchi hupuuzia tahadhari hizo, hali inayoweza kuhatarisha afya zao.

Nae Afisa Afya wa Wilaya, Jabir Sleiman Haji, amewataka wajumbe hao kuwa mabalozi wa kuielimisha jamii kuhusu afya ya mazingira, ili kuachana na tabia hatarishi zinazosababisha maafa, ikiwemo kutupa taka ovyo kwenye mitaro na kuachia maji taka hasa wakati wa mvua kubwa.

Kwa upande wake, Diwani wa Wadi ya Kinuni, Salama Rajabu Masinga, amesema kuwa jukumu la usafi ni la kila mtu. na tayari huduma za usafi zimeanzishwa ili kuhakikisha mji unakuwa safi, hivyo amesisitiza ushirikiano wa pamoja na kila mwananchi kutimiza wajibu wake.    

Aidha, amebainisha kuwa mahakama maalum zimeanzishwa kushughulikia makosa hayo na adhabu za papo kwa papo zitatolewa.

Nao masheha wamesema bado jamii nyingi haina uelewa wa kutosha kuhusu elimu ya afya ya mazingira, hivyo wameiomba Serikali kuweka sheria kali zaidi ili kuhakikisha changamoto za usafi wa mazingira zinapatiwa ufumbuzi wa kudumu.

Na Khadija Khamis 

WHSUM

Post a Comment

0 Comments