6/recent/ticker-posts

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe.Hemed Suleiman Amuwakilisha Rais wa Zanzibar Kongamano la Mzee Karume - Kampasi ya Karume Bububu Zanzibar

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla akifungua kongamano la Nane (8) la kumbukumbu ya Rais wa Kwanza wa Zanzibar Hayati sheikh Abeid Amani Karume kwa niaba ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dkt Hussein Ali Mwinyi lililofanyika katika chuo cha Mwalimu Nyerere kampasi ya Karume Zanzibar.

Serikali ya Awamu ya Nane inayoongozwa  na Rais Dkt. Hussein Ali Mwinyi itaendeleza  dhamira ya dhati ya Hayati Mzee Karume ya ukombozi wa wananchi uliopelekea kuishi kwa kuheshimiana, usawa na kujenga ustawi mwema wa wananchi na Taifa kwa ujumla.

Yameelezwa hayo na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe.  Hemed Suleiman  Abdulla  kwa niaba ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dkt Hussein Ali Mwinyi katika ufunguzi wa Kongamano la Nane (8) la kumbukumbu ya Rais wa Kwanza wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Hayat Sheikh Abeid Amani Karume lililofanyika katika Chuo cha Mwalimu Nyerere Kampasi ya Karume Zanzibar.

Amesema azma ya Mzee Karume kufanya Mapinduzi matukufu ya zanzibar ni kuondoa kiza cha dhulma kilichokuwa kimetanda Zanzibar na kuleta mwanga wa uhuru na heshima kwa wananchi.

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kuzingatia dhamira ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar ya mwaka 1964, Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2025/2030, Dira ya Maendeleo ya Zanzibar 2050, Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, mipango na miongozo mbalimbali, inaendelea kuleta maendeleo kwa wananchi kwa kuimarisha utoaji wa huduma bora na kuwekeza katika miradi ya kimkakati kama vile, Barabara, Bandari na Viwanja vya Ndege ili kuimarisha ukuaji wa uchumi ambao  umefikia asilimia 7.1.

Aidha amefahamisha kuwa, Serikali imeendeleza dhamira ya Hayati Mzee Karume ya kuinua uchumi wa wananchi kupitia kilimo kwa kuwapatia hati za umiliki za shamba za Mikarafuu za Serikali kwa wakulima wa Unguja na Pemba, ili kuongeza tija ya uzalishaji wa zao la karafuu na kumnufaisha mwanachi na Taifa kwa ujumla.  

Sambamba na hayo Makamu wa Pili wa rais amesema kuwa  Serikali itaendelea kuimarisha utoaji wa huduma kwa wananchi ikiwemo, Elimu, Afya, Maji safi na salama, na vilevile kuendeleza miradi inayokuza Uchumi wetu, kuhamasisha uwekezaji na kuendeleza Sera ya Uchumi wa Buluu ili kuongeza fursa za ajira kwa vijana wetu.

Mhe. Hemed amewakumbusha wananchi wote kuendelea kudumisha amani na umoja ambao ndio msingi wa maendeleo na kujiepusha na vishawishi vitakavyopelekea kuchafua amani iliyopo nchini.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Chuo cha Mwalimu Nyerere Mhe. STEPHEN MASATO WASIRA amesema lengo la kuanzishwa Kongamano hilo ni kuvirithisha vizazi vya sasa Fikra na  Falsafa za viongozi waasisi wa Taifa la Tanzania.

Mhe. Wasira ameeleza Hayati Mzee Karume alihakikisha anakomesha upendeleo wa uchumi, sheria, haki na usawa kwa watu wote na Kusisitiza umoja na mshikamano kwa Wazanzibari wote.

Amefahamisha kuwa Hayati Mzee karume alikemea vikali ubaguzi wa aina yoyote na kuwataka wananchi kuishi kwa kuheshimiana na kusaidiana kwa maslahi mapana ya  Taifa.

Nae Mkuu wa Chuo cha Mwalimu Nyerere Profesa HARUNI MAPESA amesema katika kuhakikisha chuo hicho kinatoa elimu bora yenyenkukidhi viwango vya Kitaifa na Kimataifa Chuo kinaendelea na miradi mikubwa ya ujenzi wa Majengo ya Ofisi, madarasa, hostel na ununuzi wa vifaa vya kisasa vya kujifunzia na kufundishia  katika kampasi zote za chuo hicho.

Profesa Mapesa amefahamisha kuwa chuo kwa kushirikiana na wadau mbalimbali kimepitia na kuboresha mitaala na kuanzisha mitaala mipya ili iweze kukidhi mahitaji ya sasa ya jamii na Taifa kwa Ujumla sambamba na kuanzisha shahada mbili za umahiri katika fani ya Uongozi na maadili, shahada ya jinsia na maendeleo pamoja na shahada ya maendeleo ya jamii.

Amesema chuo cha Mwalimu Nyerere kutaendelea kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia ili kiweze kutanua mbawa zaidi za mafanikio ndani na nje ya Tanzania.


 Imetolewa na Kitengo cha Habari ( OMPR )

Leeo tarehe ….08 / 04 / 2026

Post a Comment

0 Comments