Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar zitaendelea kuunga mkono juhudi za kuikuza na kuieneza lugha ya kiswahili ili iendelee kutumika Duniani kote.
Yameelezwa hayo na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla katika ufunguzi wa kongamano la Tano ( 5 ) la Idhaa za Kiswahili Duniani linalofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa (AICC) Jijini Arusha.
Akizungumza na viongozi wa serikali, wadau wa habari na wataalamu wa lugha ya kiswahili waliohudhuria katika Kongamano hilo, Mhe. Hemed amesema katika kufikia malengo ya kuifanya lugha ya Kiswahili kutumika duniani kote, Serikali zote mbili zitahakikisha zinaimarisha mafunzo ya ubunifu wa kidijitali, uwezeshaji wa mitaji, kuimarisha miundombinu ya Tehama na kukuza ushirikiano wake na sekta binafsi.
Amesema Idhaa za Kiswahili zimekuwa ni mhimili muhimu wa maendeleo ya lugha ya kiswahili kwa kutoa taarifa sahihi, kuimarisha elimu, demokrasia na maadili ya jamii.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amefahamisha kuwa mabadiliko makubwa ya kiuchumi na kijamii yanayotokea yanaendelea kuifanya lugha ya kiswahili kuwa nyenzo muhimu ya mawasiliano, maarifa na maendeleo nchini.
Amefahamisha kuwa Vyombo vya habari pamoja na majukwaa ya kidijitali kama vile mitandao ya kijami vina nafasi ya kipekee katika kuifikisha lugha ya kiswahili kwa hadhira pana zaidi duniani kupitia ubunifu wa kidijitali kama vile maudhui ya mitandao ya kijamii, video za elimu na program za simu .
Sambamba na hayo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amewaagiza viongozi na watendaji wa Idhaa za Kiswahili kuendeleza utaratibu wa kukaa pamoja na wataalamu wa Kiswahili na kubadilishana uzoefu wa namna bora zaidi ya kukikuza kiswahili pamoja na kukabiliana na changamoto za utangazaji kwa kiswahili.
Aidha, amewataka wanahabari kunjenga uramaduni wa kutumia kamusi katika kazi zao ili kufahamu matumizi sahihi ya msamiati na istilahi za lugha ya kiswahili pamoja na kuandaa vipindi vinavyohamasisha amani na mshikamano, kukuza maadili na kujiepusha na kauli zinazoweza kuvuruga amani na kuvunja uhusiano na Mataifa Mengine.
Kwa upande wao Mawaziri wenye dhamana ya Wizara za Habari kwa Tanzania Bara Mhe. Paul Christian Makonda na kwa Zanzibar Mhe. Riziki Pembe Juma wamesema wizara zitaendelea kutatua changamoto zilizopo ili lugha ya kiswahili izidi kupata hadhi na heshima na kuwa lugha muhimu ya mawasiliano duniani kote.
Wamesema Serikali kupitipia wizara husika zitaendelea kushirikiana na vyombo vya habari ili kuilinda lugha ya kiswahili iendelea kutumika kwa ufasaha na kuekeza katika Teknolojia na matumizi ya kidijitali ili kiswahili kuzidi kuthaminika, kuheshimika na kutambulika zaidi Ulimwenguni.
Wameeleza kuwa Tanzania ni nchi pekee iliyofanikiwa kufungua vituo vya kufundishia lugha ya kiswahili nje ya nchi jambo ambalo linaendelea kuipa heshima Tanzania na kuthibitisha kuwa chimbuko la lugha ya kiswahili ni Tanzania.
Wakizungumzia mashindano ya Afkon 2027 wamesema Tanzania imejipanga kwa mashindano hayo yatakayozidi kuipa hadhi lugha ya kiswahili kwa kuitangaza Kimataifa lakini pia yatatoa fursa ya kukuza uchumi wa nchi kupitia shughuli mbali mbali za kiuchumi zitakazofanyika wakati michuano hio ikiendelea.
Nae Mwenyekiti wa Bodi ya Baraza la Kiswahili Tanzania (BAKITA) Profesa Martin Mhandoamesema BAKITA itaendelea kutoa kila aina ya ushirikiano ili kuhakikisha lugha ya kiswahili inaendelea kutumika kwa ufasaaha hasa katika vyombo vya habari na kuiwezesha lugha hio kuendana na Mabadiliko ya Kidunia.
Profesa Mhando amefahamisha kuwa Idhaa za Kiswahili Dunianiz zimekuwa na mchango mkubwa katika zikiifikia hadhira na kukitangaza kiswahili Kimataifa hivyo zinapaswa kuhakikisha wanakitumia kiswahili kwa ufasaha wakati wa kufikisha ujumbe kwa hadhira iliyokusudiwa.
Ameeleza kuwa kukua na kuenea kwa kasi kwa lugha kiswahili kunatokana na mchango mkubwa unaotolewa na Serikali kwa kuhakikisha kiswahili kinafundishwa vyuoni na mashuleni jambo linalochangia lugha ya kiswahili kuzidi kutambulika ulimwenguni kote.
Wakitoa salamu kwa niaba ya Radio za Kitaifa na Kimataifa watangazaji Salum Othmana kutoka Shirika la Utangazaji Zanzibar( ZBC ) na Bibi Yenje Lee kutoka Idhaa ya Kiswahili ya Kimataifa ya Radio China wamesema vyombo vya habari vitahakikisha wanaiwezesha lugha ya kiswahili kuendelea kuwa hai na kutumika kwa ufasaha zaidi kupitia vyombo mbali mbali vya habari ndani na nje ya nchi.
Wamesema vyombo vya habari vimepiga hatua kubwa kimaendeleo kupitia lugha ya kiswahili kwa kuandaa na kutafsiri vipindi mbali mbali kwa lugha ya kiswahili jambo ambalo limewapatia sifa na heshima kubwa pamoja na kuendelea kufuatiliwa na wadau wengi duniani.
Imetolewa na Kitengo cha Habari ( OMPR )
Leo tarehe 24 / 03 / 2026
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
0 Comments