Kaimu Waziri wa Biashara na Maendeleo ya Viwanda ambae pia Waziri wa Kazi na Uwekezaji Mhe. Shariff Ali Shariff amesema ameridhishwa na wafanyabiashara kufuata bei elekezi iliyowekwa na Serikali katika kuuza bidhaa zao.
Mhe. Shariff ameyasema hayo wakati alipofanya ziara ya kutembelea masoko ya Darajani, Mombasa, Mwanakwererekwe na Jumbi kuhusiana na kuangalia bei elekezi iliyotolewa na Serikali, amesema wafanyabiashara wengi wametekeleza agizo la Serikali la kuweka bei katika bidhaa zao.
“Nimerishwa sana na Wafanyabiashara wametii, wanauza bidhaa zao kwa kufuata bei iliyotolewa na serikali bidhaa ya mchele wa mapembe inauzwa kwa bei ya sh. 2000 hadi 1800 na wengine wamepunguza hadi sh. 1600 na mafuta hii faraja kubwa kila mmoja anaweza kununua ila changamoto iliopo ni wananchi kuweza kumudu ”, ameeleza Mhe. Sheriff.
Aidha amefahamisha kuwa ipo haja kwa wafanyabiashara kupatiwa elimu kuhusiana na kuendesha na kuhifadhi biashara zao kwani wafanyabiashara wengi hawana uelewa katika kuhifadhi na usafi ni muhimu kufanya hivyo ili kuboresha bidhaa na wafanyabiashara katika masoko.
Waziri huyo ametoa maelekezo kwa wafanyabiasha ya bidhaa ya kuku, nyama na samaki kuweka mazingira mazuri wakati wanapouza bidhaa zao kwa kuvaa safi zenye kuridhisha, kutumia vishio au kuvaa glavu pamoja na kuhifadhi bidhaa hizo hata hivyo amesema serikali itatoa muongozo kuhusiana na wafanyabiashara hao.
Aidha ameeleza kuwa Serikali inafuatia na kuchukua hatua wafanyabiashara wanaouza biadhaa amabazo zimepitwa na muda kwa kuziangamiza na kuziteketeza hivyo amewasisitiza wananchi kutoa taarifa pale wanapoona bidhaa hizo zilizopitwa muda ili kunusuru mtumiaji.
Nae Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani Halali wa Biashara Alia Emannuel Juma amesema lengo la ziara hiyo ni kuangalia uwepo wa bidhaa na kuwekwa na kufuata bei elekezi iliyotolewa na Serikali.
Amesema kwa mujibu wa sheria namba 5 ya mwaka 2018 biadhaa zote ziwekwe au zibandikwe bei zionekane hivyo mfanyabiashara anatakiwa kuweka bei katika bidhaa yake ili kupata urahisi na kuondosha usumbufu kwa mteja anaetaka kununua bidhaa.
Mkuu wa Umoja wa Wafanyabiashara la Soko la Jumbi Faki Suleiman Khatib ameipongeza Tume ya Ushindani Halali wa Biashara kwa kutekeleza vyema majukumu ya kufuatilia bei za bidhaa katika masoko na kuiomba serikali kuwaunganishwa na mwekezaji ili kuliinua soko kwa kupatiwa mitaji na kujiinua kimaisha.
0 Comments